Charles James
WAZIRI
wa Katiba na Sheria George Simbachawene, amesema serikali ya Tanzania
ipo katika mchakato wa kurudi kuwa wanachama wa Mahakama ya Afrika baada
ya kujitoa kwa muda sasa kutokana na sababu mbalimbali.
Simbachawene,
alibainisha hayo juzi mara baada ya kikao cha pamoja na viongozi wa
Mtandao wa watetezi wa haki za binadamu Tanzania (THRDC) kilichofanyika
katika ofisi za wizara ya Katiba na Sheria Mtumba jijini Dodoma.
Alisema, suala la Tanzania kujitoa katika Mahakama ya Afrika, zilikuwepo sababu lakini haziwezi kuwa za kudumu.
Waziri Simbachawene, alieleza kuwa mazungumzo yanaendelea ndani ya serikali na anaamini nchi itarudi tena katika Mahakama hiyo.
"Mahakama
hii ipo Tanzania, inakuwa si vizuri sana kama tena sisi Watanzania
tutakuwa hatupo kwenye hii Mahakama tupewe muda, mchakato unaendelea
nina imani si muda mrefu maamuzi yatatolewa na serikali"alisema
Simbachawene
Aidha, alisema Tanzania ni nchi ambayo inatambua,
inaheshimu, inatunza na kulinda haki za binadamu, na itaendelea
kushirikiana na wadau wa masuala ya Haki za Binadamu.
“Katika
mwaka mmoja wa uongozi wa Rais Samia ameonyesha nia ya kutunza haki
maeneo ambayo yameonyesha kuwa na shida katika maeneo ya haki za
binadamu anafanya hivyo kwa vitendo, pamoja na nadharia.
“Wizara
ya Katiba na Sheria imefurahi kuona mpo na itaendelea kushirikiana na
nanyi katika kila jambo ambalo mtapenda tushirikiane." alisema
Simbachawene
Pia, aliwataka Watetezi wa Haki za Binadamu nchini
kuhoji na kuzungumza na wizara, kuliko kupeleka katika majukwaa ya
kimataifa na kuiondolea heshma nchi.
Vilevile, alisema Wizara
itashiriki kwa pamoja na AZAKI katika majukwaa ya kimataifa ili
kuhakikisha Tanzania inajengwa kwa mashirikiano thabiti na yenye tija
kati ya pande zote mbili.
Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa,
katika kikao hicho alitaja baadhi ya maeneo ambayo yanaweza kufanyiwa
maboresho na wizara ikiwemo kuwa na utataratibu mzuri wa kufahamu,
kuripoti na kutambua kazi za watetezi wa Haki za Binadamu kama wadau
muhimu wa wizara hiyo.
“Pia, kufanyika kwa maboresho katika
maeneo ya utoaji wa msaada wa kisheria,uboreshwaji wa mifumo ya utoaji
haki nchini,maboresho ya baadhi ya sheria ikiwemo sheria ya NGO, hasa
katika upatikaji wa vibali vya tafiti inayoyataka mashirika kupitia
TAMISEMI ili kupata pamoja na sheria zingine,ushiriki wa wizara katika
mikutano na majukwaa ya kimataifa,Tanzania kurudi katika mahakama ya
Afrika Mashariki”alisema
Pamoja na meneo hayo ya maboresho THRDC
pia imetoa mapendekezo ya kufanyiwa kazi na wizara katika kuboresha
shughuli za utetezi wa Haki za Binadamu nchini.
Mapendekezo
hayo ni pamoja na kuboreshwa kwa mfumo wa utekelezaji (Human Rights
Enforcement Mechanism - BRADEA) sheria iliyokuwa inaweka utaratibu wa
kulinda haki za kikatiba.
Olengurumwa, alisema mabadiliko
yaliyofanyika yameweka vikwazo vingi kwa mtanzania mmoja mmoja au
taaisisi zao kutekeleza agizo la ibara ya 26/2 ya kulinda katiba.
“Kumekuwa
na vigingi vingi ambavyo tunaweza kufanya majadiliano na maboresho
kupitia wizara hii ambavyo yatatoa fursa ya watanzania kwenda moja kwa
moja na Taasisi za Haki za Binadamu kwenda mahakamani kulinda na kutetea
haki za Binadamu kupitia mlango wa kikatiba.
“Kuwepo kwa
National human rights Action plan (Mpango wa Taifa wa Haki za Binadamu,
serikali iangalie namna ya kuharakisha kukamilika kwa mchakato huo ili
kuwa na andiko litakalotoa mwongozo utawaunganisha wadau wa haki za
Binadamu na serikali."alisema Olengurumwa
Hata hivyo, alisema
kuwepo na Sera ya Haki za Binadamu ambayo inaweza kutoa mwongozo kwa
taasisi binafsi na serikali kuhusiana na masula ya haki za binadamu.
“Sera
hii itawatambua na kuwalinda watetezi wa Haki za Binadamu. Hii ni
kuwawezesha Wadau pamoja na serikali wawe na uelewa wa pamoja wa maswala
ya utetezi na Watetezi wa Haki za Binadamu nchini.
“Kumekuwa
na changamoto za utekelezaji wa maamuzi wa Mahakama za ndani na nje hasa
katika maeneo ya access to justice katika kesi za Haki za Binadamu,
lazima uje Dar es Salaam. Tunapendekeza serikali iruhusu kila high kort
yenye hadhi ya Mahakama Kuu iwe na uwezo wa kusikiliza kesi hizo katika
Mikoa kesi hizo ziliporipotiwa." Alisema Olengurumwa.
Waziri wa Katiba na Sheria George Simbachawene akikabidhiwa mapendekezo na Viongozi wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania, THRDC ofisini kwake Mtumba Jijini Dodoma.
Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania THRDC, Onesmo Olengurumwa akizungumza katika kikao baina ya Mtandao huo na Waziri wa Katiba na Sheria, George Simbachawene jijini Dodoma.
Waziri wa Katiba na Sheria, George Simbachawene akiwa katika picha ya Pamoja na Viongozi wa Wizara hiyo ofisini kwake Mtumba jijini Dodoma.
No comments:
Post a Comment