HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, January 26, 2022

DKT. GWAJIMA, MENEJIENTI YA MAENDELEO YA JAMII WAZIDI KUNOGESHA MBINU KUKABILIANA NA UKATILI

 Na WMJJM, Dodoma

WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima, amewaasa Wadau wote kushirikiana kuhakikisha changamoto za watoto wanaoishi na kufanya kazi mtaani zinapatiwa ufumbuzi.

Mhe. Gwajima ametoa rai hiyo leo Januari 25, 2022 alipotembelea makao ya kulea watoto yatima na Wazee wasiojiweza, yanayoendeshwa na Watawa wa Upendo yaliyopo Hombolo, mkoani Dodoma.

Amesema bado kuna watoto wengi wanaoishi na kufanya kazi Mitaani na Serikali kwa kushirikiana na Wadau bado inatafuta ufumbuzi.

"Tukumbuke watoto wanaoishi Mitaani wanakutana na changamoto nyingi ikiwemo ukatili, ukatili wa majumbani ni sababu na matokeo yake wanakutana na mazingira hatari zaidi hii haikubaliki" amesema Mhe. Waziri Gwajima.

Akifafanua kuhusu takwimu, Dkt. Gwajima, amesema. asilimia 70 ya watoto wanaoathirika na ukatili ni watoto wa kike, huku Idadi wanawake ikitajwa kufikia
asilimia 96.

"Ili tuweze kupunguza kadhia hii, silaha ya kwanza ya jamii ni uelewa wa pamoja na kukataa kwa Nguvu moja, kuweka mifumo madhubuti ya kuzuia vitendo vya ukatili" amesema Mhe. Gwajima.

Kwa upande wake, Naibu Waziri Mhe. Mwanaidi Ali Khamis akizungumza na walezi wa makao hayo, amewataka Maafisa Maendeleo ya Jamii kuamka na kufanya kazi yao waliyokusudiwa.

Akizungumza wakati wa Ziara hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara Dkt. Zainab Chaula ameitaka jamii kutumia rasilimali zilizopo maeneo yao kutatua changamoto zinazowakabili ikiwemo kuongeza kipato na kuwasaidia wahitaji, huku akitolea mfano Bwawa la Hombolo na wewe jinsi linavyoweza kuwa mkombozi.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo mpya, Amon Mpanju ametoa rai kwa wananchi kuwa na moyo wa kujitolea kuwasaidia wahitaji kwa namna mbalimbali.

Wakati wa Ziara hiyo Diwani kata ya Hombolo,Mhe. Mathayo Ndajiro hakuacha kuipongeza Wizara kwa mikakati iliyoamua kuja nayo ikiwepo kutokomeza ukatili kwa mbinu Shirikishi kwa Makundi yote.

Awali akiwasilisha taarifa ya makao hayo kwa Mhe. Waziri, msimamizi msaidizi wa makao hayo Mtawa Radienince MC, amesema makao hayo yana uwezo wa kuhudumia watoto 40 na waliopo ni 23. Aidha Wazee wanaohudumiwa kwa sasa ni 58.

Sista Radienince ameongeza kwamba, kwa mwaka 2021 watoto wapatao 10 wameunganishwa na familia zao.

Viongozi na Menejimenti ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi maalum, wapo katika ziara endelevu yakujifunza na kutafuta afua zakutatua changamoto ya Matukio ya ukatili na Ustawi wa Jamii.


Picha mbalimbali za viongozi wa Wizara wakati wa Ziara ya Wizara hiyo katika kituo cha Hombolo.
Dkt. Dorothy Gwajima, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, akiongea wakati wa Ziara ya Waziri hiyo kwenye kituo cha Kulelea Wazee na watoto Hombolo.
Dkt. Zainab Chaula Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum wakti wa ziara hiyo.
Mhe. Mwanaid Ally Khamis, alipokuwa akiongea wakati wa Ziara Uongozi wa Wizara hiyo katika Makao ya kule wazee na watoto Hombolo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad