HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, November 30, 2021

NSEKELA ATUNUKIWA TUZO YA KIONGOZI BORA WAKATI BENKI YA CRDB IKITUNIKIWA TUZO YA HUDUMA BORA KWA NJIA YA KIDIJITALI AFRIKA MASHARIKI

Mkurugenzi wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela akipokea Tuzo ya Huduma Bora za Fedha kwa njia ya kidijitali Afrika Mashariki kutoka kwa Mkurugenzi wa Idara ya Diplomasia ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi, Edwin Rutegaruka katika hafla ya tuzo za ‘Consumer Choice Awards’ iliyofanyika katika Ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es Salaam siku ya Jumapili. Wengine pichani ni wafanyakazi wa Benki ya CRDB. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela ametunukiwa tuzo ya kiongozi bora katika tuzo zilizoandaliwa na kampuni ya Consumer Choice Awards Africa. Tuzo hiyo ambayo imemtambua Nsekela kama kiongozi mahiri na mwenye ushawishi mkubwa hapa nchini kwasasa, ilitolewa katika hafla iliyofanyika siku ya Jumapili 28 Novemba 2021 katika ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es Salaam.

Katika tuzo hizo Benki ya CRDB pia ilitunikiwa tuzo ya Huduma Bora za Fedha kwa njia ya kidijitali Afrika Mashariki ambayo imetokana na uwekezaji mkubwa ambao benki hiyo umeifanya katika mifumo ya kidijitali ya utoaji huduma. Mapema mwaka huu Benki hiyo ilizindua huduma ya SimBanking ambayo imeboreshwa zaidi na kuwawezesha wateja kupata asilimia 90 ya huduma za kibenki kupitia simu ikiwamo kujifungulia akaunti wenyewe.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hizo, Nsekela aliwashukuru wateja na wadau wa benki hiyo kwa heshima waliyompa ya kumchagua kiongozi bora huku akiahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii kwa maslahi ya wateja na Watanzania. Nsekela pia aliwashukuru kwa kuwa sehemu ya mafanikio ya utekelezaji wa mkakati wa mageuzi ya biashara kwa njia ya kidijitali ambao kwa kiasi kikubwa umesaidia kupata tuzo hiyo. 

“Tunajivunia kupata tuzo hii. Niwashukuru wateja, wanahisa na washirika wetu wa biashara kwa kuendelea kutuamini na kutufanya kuwa bora zaidi. Hizi sio tuzo za Benki ya CRDB peke yake, ni tuzo za Watanzania wote,” alisema Nsekela. “Teknolojia na ubunifu vimeiwezesha benki yetu kutoa huduma bora kwa haraka, urahisi na kufikia watu wengi zaidi pale walipo,” aliongeza. 

Aidha Abdulmajid aliwasisitiza na kuwahamasisha wateja na Watanzania kwa ujumla kuendelea kutumia huduma za kidijitali kupata huduma mbalimbali za kibenki nchini na kuachana na matumizi ya pesa taslimu ili kuendana na mabadiliko ya kiuchumi pia kupunguza utumiaji wa muda mrefu katika kufuata huduma za kibenki.

Aidha aliishukuru Serikali kwa kuendelea kuimarisha mazingira ya biashara nchini ambayo kwa kiasi kikubwa yamekuwa na mchango katika kuimarika kwa biashara nyingi ikiwamo sekta ya fedha. Nsekela alisema benki hiyo imeendelea kuunga mkono serikali katika jitihada zake za kuimarisha uchumi hususani katika kufanikisha utekelezaji wa miradi ya kimkakati ikiwamo ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) na Maradi wa Umeme wa Maji wa Nyerere (Stieglers).


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad