HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, October 28, 2021

MKOA WA RUVUMA WATENGA EKARI 48,343 KWA AJILI YA MAZAO YANAYOZALISHA MAFUTA

 

Na Muhidin Amri, Songea

MKOA wa Ruvuma umetenga jumla ya  ekari 48,343.35 za ardhi kwa ajili ya kilimo cha zao la Alizeti,Ufuta na Soya ikiwa ni mkakati wake wa kutaka kujitosheleza kwa mafuta ya kula.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge amesema hayo jana,wakati akifungua Mkutano wa wadau  wa kilimo uliohudhuriwa na Wakuu wa wilaya,Wakurugenzi wa Halmashauri,maafisa ugani na taasisi za fedha.

Aidha amesema, mkakati huo unakusudia na utasaidia  Taifa kuepuka kutumia  fedha nyingi kuagiza bidhaa hiyo nje ya nchi na kuinua vipato vya wakulima na Nchi kwa jumla.

Ameishukuru Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kutenga Sh.bilioni 2.2 kwa ajili ya ununuzi wa mbegu bora za Alizeti ambazo awali zilikuwa zikiuzwa na wafanyabiashara kwa bei ya Sh.35,000 kwa kilo.

Ibuge amesema,kupitia mpango huo sasa mbegu za alizeti  zitauzwa kwa bei ya Sh.3,500 kupitia wakala wa mbegu(Asa) sawa na asilimia kumi ya  bei ya awali  na kuwasihi wananchi wa mkoa wa Ruvuma kutumia fursa hiyo kuwekeza katika kilimo cha zao hilo.

Amesema,katika mkoa wa Ruvuma mahitaji ya mbegu za alizeti,soya na ufuta ni  kilo 310,222 na mbolea ni tani 1,662 ambapo kwa msimu wa kilimo 2021/2022 Halmashauri za mkoa huo zimepanga kulima ekari 12,570 kati ya ekari 48,343 zilizotengwa.

Amesema, ekari hizo zitahitaji tani 112  ambapo zao la ufuta mahitaji ni tani 21,soya tani 77 na alizeti tani 14,na kuzielekeza Halmashauri kuhakikisha zinawezesha upatikanaji wa mbegu na pembejeo hizo kwa wakati ili wakulima wasikwame.

Pia amesema, katika msimu wa kilimo 2021/2022 mkoa huo umejipanga kutekeleza mfumo wa kilimo cha pamoja na kilimo cha mkataba(Block Farming& Contract Farming) kwenye Halmshauri ambacho kinahusisha utengaji wa maeneo  kwa wakulima hulima eneo moja.

Amesema, kilimo hicho wakulima watapata huduma za ugani na urahisi wa upatikanaji wa pembejeo na masoko ambapo wahusika wa mpango huo ni Vyama vya Ushirika,wakulima,vikundi,taasisi mbalimbali za umma na binafsi na makampuni ya ndani nan je ya Nchi.

Kwa mujibu wa Jenerali Ibuge,Serikali ya mkoa imeridhia kilimo hicho cha mktaba kwa wakulima kinachohusisha makubaliano baini ya mkulima na kampuni au mtoa huduma ambaye atahusika kutoa pembajeo,huduma ya ugani na ununuzi wa mazao  kwa lengo la kuinua kipato.

Katika kikao hicho, Ibuge ameziagiza Halmashauri kwenda kuviwezesha vikundi vitakavyohitaji kuwekeza katika mazao hayo, na kuhakikisha wanatenga eneo angalau moja  kwa ajili ya taasisi ya utafiti wa kilimo(Tari) ambalo litatumika  kama shamba darasa na kuzalisha mbegu bora kwa mazao ambayo Halmashauri itaanza nayo.

Kwa upande wake Katibu Tawala msaidizi uchumi na uzalishaji Jeremiha Sendoro amesema, manufaa ya kilimo cha pamoja ni kutumia rasilimali  kidogo kama maafisa ugani wachache kuwafikia wakulima wengi na kalenda ya kuhudumia shamba huandaliwa kwa pamoja.

Sendoro ametaja faida nyingine, ni  usambazaji wa pembejeo hufanywa  kwa urahisi kwa kuwa mashamba yote yapo kwenye uelekeo mmoja na upatikanaji wa masoko ni rahisi kwa sababu mazao ukusanywa kwenye maghala au soko moja.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Brigedia Jenerali Wilbert Ibuge akiongea katika kikao cha wadau mbalimbali wa kilimo wa mkoa huo,kushoto kwake Katibu Tawala wa mkoa Stephen Ndaki.Wadau mbalimbali wa kilimo wakiwemo maafisa ugani, maafisa ushirika na kilimo kutoka wilaya za mkoa wa Ruvuma wakimsikiliza Mkuu wa mkoa huo(hayupo pichani)wakati kikao kazi cha wadau wa kilimo kilichofanyika  wilayani Songea.Wakurugenzi watendaji wa Halmashauri za wilaya za mkoa wa Ruvuma wakifuatilia taarifa juu utekelezaji wa kilimo cha mazao ya alizeti,soya na ufuta katika kikao kazi cha wadau wa kilimo kilichofanyika katika ukumbi wa Manispaa ya Songea wilayani Songea. Picha zote na Muhidin Amri

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad