HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, October 4, 2021

Coca-Cola yazindua mwonekano wa chupa mpya ya Sprite nchini Tanzania

 

Kampuni ya Coca-Cola Tanzania kwa mara ya kwanza imezindua mwonekano mpya wa kinywaji chake pendwa cha Sprite, ambapo sasa itaonekana kwenye chupa ya plastiki isiyo na rangi.


Mabadiliko ya kutoka chupa maarufu iliyozoeleka ya rangi ya kijani yanamaanisha kuwa sasa chupa za kinywaji cha Sprite zitaweza kuokotwa, kurejelezwa, na kutumika tena kutengenezea chupa mpya, hatua hii ni sehemu ya ‘World Without Waste’ ambayo ni dhamira ya Coca-Cola kuhakikisha dunia bila taka ikiwa inalenga kukusanya na kurejeleza kiwango sawa cha chupa au kopo kinachouza na kutumia asilimia 50 (50%) ya malighafi zilizorejelezwa katika vifungashio vyake vyote kufikia mwaka 2030.

“Huu ni mwanzo mpya kwa wateja wetu nchini Tanzania kwa kuwa sasa wataweza kuburudika na kinywaji chao pendwa cha Sprite huku chupa ikiweza kurejelezwa kwa urahisi na kutumika tena kutengenezea bidhaa mpya. Chupa mpya isiyo na rangi pia itakuwa na mchango kiuchumi kwani itakuwa na thamani zaidi kwa warejelezaji wa taka Tanzania ambao wanategemea kukusanya na kuuza taka zinazotokana na vifungashio vya plastiki kujiingizia kipato,” alisema Unguu Sulay ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Coca-Cola Kwanza, Tanzania.

“Tunayofuraha kubwa kutambulisha chupa isiyo na rangi ya kinywaji cha Sprite nchini Tanzania na kuunga mkono jitihada endelevu za mazingira zinazofanywa na serikali zinazoendana na sera za mazingira na mkakati wa maendeleo wa kitaifa. Kwa hakika, mabadiliko kutoka chupa ya kijani ya Sprite iliyozoeleka kwa miaka mingi inaonyesha kujizatiti kwa Coca-Cola katika kulinda mazingira kwa kutumia ubunifu ambao ni rafiki kwa mazingira,” aliongezea Salum Nassor, Mkurugenzi wa Masuala ya Umma na Mawasiliano wa Coca-Cola Kwanza, Tanzania.

Mkakati wa Dunia Bila Taka ‘World Without Waste’ unaonyesha kujizatiti kwa Coca-Cola katika kufanya biashara endelevu ambayo inapambana na changamoto ya taka zinazotakana na vifungashio vya plastiki. Chupa mpya isiyo na rangi inaweza kutumika kutengenezea bidhaa mpya mbalimbali kama vile mito ya kulalia na sehemu za ndani za foronya, pia na chupa mpya, hivyo kuifanya kuwa yenye thamani zaidi kuliko ya kijani ambayo ina matumizi machache.

Akizungumza wakati wa uzinduzi mgeni rasmi, Mheshimiwa Seleman Jafo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais (Muungano na Mazingira) amesema kuwa, “Naipongeza Coca-Cola kwa hatua hii kubwa iliyoichukua na kuongoza njia kwa kuamua kutumia malighafi za vifungashio ambazo zinaweza kutumika na kurejelezwa tena. Kama wizara, tunatambua kuwa jitihada hizi hazitawahusisha nyinyi pekee kama wazalishaji, bali pia na wadau wengine katika mnyororo mzima wa thamani wakiwemo wateja katika kufanya mazingira tunayoishi kuwa bora, safi, na salama.”

“Nadhani wote mnatambua kwamba, dunia imekuwa katika vita na taka za plastiki ambapo baadhi ya mijadala imechukua sehemu kubwa ya mikutano ya mazingira na inahamasisha kuona Coca-Cola imechukua hatua kuainisha changamoto hii na jitihada za kutafuta suluhisho. Kama serikali, jukumu letu pekee si tu kuhakikisha wazalishaji wote wanafuata sheria na kanuni zilizowekwa bali pia kuwahamasisha kuja na njia za kibunifu ambazo zitakuwa na manufaa kwa wateja na mazingira. Ni nadra sana kuona kampuni ikichukua hatua yenyewe bila ya maagizo kutoka kwa mamlaka husika. Ningependa kuwathibitishia kuwa serikali iko tayari kushirikiana nanyi muda wowote ili kuhakikisha kuwa kwa pamoja tunauboresha uchumi wa Tanzania,” aliongezea Mheshimiwa Jafo.

Ikiwa imeenea katika nchi zaidi ya 200, ikiwemo Tanzania, mwonekano mpya wa Sprite unajumuisha chupa isiyo na rangi, pamoja na maboresho ya mwonekano wa kuvutia kwenye chapa yake.

“Tunayofuraha kubwa kuwaletea wateja muonenako mpya wa kusisimua wa Sprite nchini Tanzania. Siku chache zijazo, tunatarajia kuja na matukio kadhaa nchi nzima ambayo yatatuwezesha kukutana na wateja wetu na kuwapatia fursa ya kujionea mwonekano wa chupa mpya ya Sprite,” alisema Kabula Nshimo, Meneja Mwandamizi wa Chapa ya Coca-Cola Tanzania.

Tanzania ni nchi ya 5 barani Afrika kutambulishwa kwa mwonekano wa chupa mpya ya Sprite ambapo tayari imeshazinduliwa katika nchi za Afrika ya Kusini, Nigeria, Ethiopia, na Kenya.

Kinywaji cha Sprite kikiwa kwenye mwonekano wa chupa mpya kitaanza kupatikana katika maduka yote mwezi huu wa Oktoba kwenye maduka ya rejareja na wasambazaji wa Coca-Cola nchi nzima.

Hafla hiyo fupi ya uzinduzi wa mwonekano wa chupa mpya ya Sprite ilihudhuriwa na wawakilishi kutoka Coca-Cola Tanzania, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Shirikisho la Viwanda Tanzania, washirika katika ukusanyaji na kurejeleza taka za plastiki, mabalozi wa serikali wa mazingira, mashirika ya serikali na binafsi yanayojihusisha na mazingira, na vyombo vya Habari.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais, Muungano na Mazingira, Mh. Seleman Jafo (wa tatu kushoto) pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Coca-Cola Kwanza Tanzania, Unguu Sulay (katikati) wakitazama mwonekano mpya wa chupa ya Sprite iliyozinduliwa nchini ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo. Wakishuhudia uzinduzi huo uliofanyika jijini Dar es Salaam, kutoka kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Samuel Gwamaka, Meneja Mwandamizi wa Chapa ya Coca-Cola Tanzania, Kabula Nshimo na Mkurugenzi wa Masuala ya Umma na Mawasiliano wa Coca-Cola Kwanza Tanzania, Salum Nassor.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais, Muungano na Mazingira, Mh. Seleman Jafo akitoa hotuba kwa wageni waalikwa (hawako pichani) wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite nchini Tanzania ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais, Muungano na Mazingira, Mh. Seleman Jafo (kulia) akishiriki mdahalo kuhusu mustakabali wa taka za plastiki nchini Tanzania wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo.
Msanii Idris Sultan ambaye pia ni balozi wa kuteuliwa wa masuala ya mazingira akifurahia jambo na Mkurugenzi wa Masoko na Mauzo Coca-Cola Kwanza Tanzania, Josephine Msalilwa wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite nchini ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo.
Meneja Mwandamizi wa Chapa ya Coca-Cola Tanzania, Kabula Nshimo akitoa hotuba kwa wageni waalikwa (hawako pichani) wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite nchini Tanzania ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais, Muungano na Mazingira, Mh. Seleman Jafo (aliyeshikilia mbao amevalia suti) akiwa ameshikilia mbao iliyotengenezwa kutokana na chupa za plastiki zilizorejelezwa kutoka kwa miongoni wa makampuni yaliyoalikwa wakati wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite nchini Tanzania ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo.



Mkurugenzi Mtendaji wa Coca-Cola Kwanza Tanzania, Unguu Sulay (kushoto) akishiriki mdahalo kuhusu mustakabali wa taka za plastiki nchini Tanzania wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo.


 Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dkt. Samuel Gwamaka akitoa hotuba kwa wageni waalikwa (hawako pichani) wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite nchini Tanzania ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Coca-Cola Kwanza Tanzania, Unguu Sulay akitoa hotuba kwa wageni waalikwa (hawako pichani) wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite nchini Tanzania ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo.
 Mkurugenzi wa Masuala ya Umma na Mawasiliano wa Coca-Cola Kwanza Tanzania, Salum Nassor akitoa hotuba kwa wageni waalikwa (hawako pichani) wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite nchini Tanzania ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo.

Wafanyakazi wa Coca-Cola Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Rais, Muungano na Mazingira, Mh. Seleman Jafo (waliokaa mstari wa mbele katikati) wakati wa uzinduzi wa mwonekano mpya wa chupa ya Sprite nchini Tanzania ambayo ni rafiki kwa mazingira na rahisi kurejelezwa pindi itumikapo.


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad