HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 1, 2021

KALEMANI AZINDUA KIWANDA KIPYA CHA KUZALISHA NGUZO ZA UMEME CHA QWIHAYA

 DENIS MLOWE, NJOMBE

WAZIRI wa Nishati Dk.Medard Kalemani amezindua kiwanda kipya cha kuzalisha nguzo cha Qwihaya na kuvitaka viwanda vya vingine nchini kuzalisha nguzo zenye ubora na kutoa wito kwa mameneja wa Tanensco kutumia nguzo hizo zinazozalishwa hapa hapa Tanzania.

Akizungumza hivi karibuni wakati wa uzinduzi wa kiwanda kipya cha kuzalisha Nguzo za Umeme cha Qwihaya kilichopo kijiji cha Mtwango mkoani Njombe, Kalemani alisema kuwa uzalishaji wa nguzo bora utasaidia kwa kiasi kikubwa miundo mbinu ya umeme kuwa imara.

Alisema kuwa kuzinduliwa kwa kiwanda hicho ni fursa kwa wakazi wa maeneo hayo ya jirani kwa kuwa kimeweza kuzalisha ajira za vijana mbalimbali na kutumia nafasi hiyo kuzalisha miti ya kutosha kwa kuwa soko la mazao ya miti ipo.

Dk. Kalemani alisema kuwa zamani kulikuwa na tabia ya kuagiza nguzo hizo kutoka Afrika Kusini hali ambayo ilimlazimu mwananchi kulipia gharama kubwa kuweza kupata nguzo na kutoa wito kwa mameneja kuacha kuwauzia nguzo wananchi.

Alisema kuwa serikali imefanikiwa kutoa sh. Bilioni 2. 7 kwa kila meneja wa mkoa kwa ajili ya kununua nguzo hivyo wananchi wasiuziwe nguzo ambazo zimegharamiwa kwa kiasi kikubwa na serikali na kuwataka wananchi kulipia sh.27,000 tu kwa ajili ya kupata huduma ya umeme.

Aliongeza kuwa viwanda kwa sasa nchini viko 11 ambavyo vinazalisha nguzo hivyo serikali iko tayari kuingia ubia na kiwanda ambacho kinauwezo za kuzalisha nguzo za kutosha sio zinaagizwa nguzo leo kesho hazipo hivyo muhimu viwanda kuendelea kuzalisha nguzo nyingi kwa kuwa soko lipo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa kiwanda cha Qwihaya General Interprises LTD., Leonard Mahenda alsiema kuwa hicho kitakuwa kiwanda cha tatu vilivyoko katika kampuni hiyo kikitangaliwa na kiwanda mama cha Mafinga na kingine kilichoko Kasulu na kiwanda hicho kinatarajia kuwapunguzia gharama za kusafirisha malighafi inayozalishwa kiwandani hapo.

Alisema kuwa kiwanda hicho hadi sasa kina akiba ya nguzo zipatazo 400,000 ambazo bado hazijasambazwa na kufanya kuwa na akiba kubwa ya nguzo za kuzalisha umeme katika viwanda vilivyoko katika kampuni hiyo.

Alisema kuwa wamefanikiwa kuzalisha ajira za vijana mbalimbali zaidi ya 350 ambao wamegawanyika katika vitengo mbalimbali na wenye elimu kuanzia msingi hadi chuo kikuu ambapo kwa kupitia kiwanda hicho wanazalisha nguzo za umeme kufikia nguzo 1500 kwa siku.

Mahenda alisema kuwa kampuni hiyo inahitaji mazao ya magogo aina ya Mkaratusi kwa nguzo zinazotengenezwa kwa ajili ya miradi ya umeme nchini na nje ya nchi kwa kuwa inatagemewa na kuwaomba wananchi kulima miti hiyo kwa wingi.


WAZIRI wa Nishati Dk.Medard Kalemani akizungumza wakati wa a kiwanda kipya cha kuzalisha Nguzo za Umeme cha Qwihaya kilichopo kijiji cha Mtwango mkoani Njombe
Mkurugenzi wa kiwanda cha Qwihaya General Interprises LTD., Leonard Mahenda akizungumza wakati wa uzinduzi huo


 


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad