Na Mwandishi wetu, Simanjiro
AGIZO
la Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alilolitoa Julai 7 Mji mdogo wa Mirerani
Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, la shughuli zote za uuzaji na
uongezaji thamani wa madini kufanyika Mirerani linaendelea kutekelezwa.
Mkuu
wa Mkoa wa Manyara, Charles Makongoro Nyerere, ameyasema hayo wakati
akizungumzia na waandishi wa habari juu ya muelekeo wa uanzishwaji wa
soko la madini ya Tanzanite Mirerani Wilayani Simanjiro.
Makongoro
amesema agizo la Waziri Mkuu Majaliwa la shughuli zote za ununuzi na
uongezaji thamani wa madini ya Tanzanite, kufanyika Mirerani baada ya
siku 90 linaendelea kutekelezwa ambapo wafanyabiashara 49 wamefungua
ofisi Mirerani.
"Majengo
mawili yameshatengwa kwa ajili ya uuzaji wa madini hayo na yameshaanza
kutumiwa na wafanyabiashara 49 wa madini hayo," amesema Makongoro.
Amesema
hatua zinazoendelea ni upimaji wa eneo la kanda maalum ya kiuchumi
(Manyara Special Economic Zone) ili kuwagawia wafanyabiashara wa madini
waweke miundombinu yao na maeneo ya makazi.
Amesema
Serikali kwa upande wake inaendelea kuingiza miundombinu muhimu ya
kuwezesha huduma za maji, umeme, barabara na nyingine kama
itakavyohitajika.
Amesema
pia kupitia eneo hilo lililotengwa limepangwa kuwa na huduma muhimu za
kijamii zikiwemo hoteli, migahawa, kituo cha polisi na maegesho ya
magari.
"Nitumie fursa
hii kuipongeza Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais Samia
Suluhu Hassan la kuhamishia soko la madini eneo la Mirerani Wilayani
Simanjiro," amesema Makongoro.
Ametoa
rai kwa jamii kuhakikisha wanatumia fursa hiyo kujiongezea vipato
binafsu na wale wafanyabiashara wa madini amewakumbusha kulipa kodi na
maduhuli ya serikali kwa mujibu wa sheria za kodi zilizopo.
Hata
hivyo, Mkuu wa wilaya ya Simanjiro Dkt Suleiman Hassan Serera amesema
utekelezaji wa agizo hilo utasaidia kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja,
vikundi, wilaya, mkoa na nchi kwa ujumla.
"Jambo
hilo ni kubwa na muhimu hivyo wote tushirikiane kwa ajili ya
kuhakikisha kuanzishwa Tanzanite City katika eneo la Manyara special
economic zones linakamilishwa ipasavyo na kwa wakati uliopangwa,"
amesema Dkt Serera.
Amesema
wiki ijayo atakutana na wafanyabiashara hao 49 katika kuhakikisha
shughuli zote za uuzaji madini hayo yanafanyika Mirerani kama
ilivyoagizwa na Waziri Mkuu Majaliwa.
Amesema
Serikali ya wilaya ipo tayari na wataendelea kusimamia kikamilifu ili
watu waweze kuanza kunufaika moja kwa moja na amewasihi watumie fursa
hiyo vizuri ili serikali waweze kwenda pamoja kwani kukamilika kwa hilo
utasaidia kuimarisha uchumi.
Waziri
Mkuu Majaliwa, Julai 7 mwaka huu, akiwa kwenye ziara yake mji mdogo wa
Mirerani, aliagiza shughuli za uuzaji na uchakataji wa madini ya
Tanzanite, ambayo duniani yanapatikana Mkoani Manyara, ufanyike mji
mdogo wa Mirerani pekee.
No comments:
Post a Comment