HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 27, 2021

MWANAMKE KIFUNGONI MWAKA MMOJA KWA KUMTUKANA MAMA YAKE MZAZI

 MAHAKAMA ya Wilaya ya Ilala imemuhukumu Zarina Mohamed Sadiki kutumikia kifungo cha mwaka mmoja gerezani baada ya kupatikana na hatia ya kumtukana mama yake mzazi matusi ya nguoni.


Hukumu hiyo imesomwa leo Agosti 26,2021 na Hakimu mfawidhi Martha Mpaze baada ya kuridhika na ushahidi uliotolewa na mashahidi wanne wa upande wa Jamuhuri walioweza kuthibitisha pasipo kuacha shaka kuwa mshtakiwa ametenda kosa hilo.

Akisoma hukumu hiyo Hakimu Mpaze amesema amezingatia hoja za pande zote mbili na ameona mshtakiwa ni mkosaji wa mara kwa mara hivyo kama angekuwa wakubadilika alivyotiwa hatiani asingerudia makosa.

Kabla ya kusomwa kwa adhabu mahakama iliuliza upande wa Jamuhuri kama walikuwa na lolote la kusema ndipo wakili wa serikali Nancy Mushumbusi aliomba mshtakiwa apewe adhabu kali ili iwe fundisho kwake na kwa wengine kwani ni mkosaji anayerudia makosa.

Wakili Nancy alidai mshtakiwa Zarina ameshawahi kutiwa hatiani mara mbili katika Mahakama ya Mwanzo Kariakoo kwa makosa kama hayo akaonywa na sasa hivi ana kesi nyingine inaendelea katika Mahakama ya Mwanzo Ukonga.

Ameiomba mahakama apewe adhabu kali kwani kaenda kinyume na mila na desturi za kitanzania , kamtukana mama yake mzazi ambaye alitoa ushahidi wake mahakamani hapo kwa uchungu huku akilia.

Katika utetezi wake mshtakiwa Zarina aliiomba mahakama impunguzie adhabu kwani yeye ni mama ana watoto wanamtegemea, hajaolewa, anapitia changamoto nyingi za kisaikolojia na hivyo akaomba apewe nafasi nyingine atajirekebisha.

"Ili iwe fundisho kwako na kwa wengine wanaotukana wazazi wao, Mahakama inakuhumumu kutumikia kifungo cha mwaka mmoja gerezani, amesema Hakimu Mpaze

Katika kesi hiyo Upande wa Mashtaka ulikuwa na mashahidi wanne akiwemo mama mzazi wa mshtakiwa huku mshtakiww mwenyewe akileta mashahidi watatu waliotoa ushahidi wa kumtetea.

Awali ilidaiwa, Novemba 29/2019 huko Kariakoo mtaa wa Uhuru na Nyamwezi ndani ya Wilaya ya Ilala mshtakiwa Zarina alimtukana mama yake mzazi aitwaye Rafika Hawa Mohamed Sadiki matusi mbali mbali ya nguoni na kumwambia 'wewe siyo Mama yangu Baba hajakuoa wewe, mwanaharamu,mwizi mkubwa sitaki kukuona hapa na utaondoka hutofanya biashara hapa nitahakikisha nimekuuwa kwa njia yoyote ile au nitakumwagia tindikali ufie mbali' kitendo ambacho kingeweza kusababisha uvunjifu wa amani.
Mshtakiwa Zarina Mohamed Sadiki mwenye asili ya Kihindi, akiingia kwenye chumba cha Polisi katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala jijini Dar es Salaam baada ya kuhukumiwa kifungo cha mwaka mmoja gerezabi kufuatia kupatikana na hatia ya kumtukana mama yake mzazi na matusi ya nguoni.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad