HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, June 16, 2021

DK MPANGO AWAASA WATANZANIA KUJENGA TABIA YA KUASILI WATOTO, ATOA MAAGIZO SITA KWA WIZARA YA AFYA, TAMISEMI

 

Charles James, Michuzi TV

KATIKA kupunguza wimbi la watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu nchini, Serikali imetoa wito kwa watanzania kujenga tabia ya kuasili watoto kwani pia kufanya hivyo ni kujiongezea baraka mbele ya Mwenyezi Mungu.

Wito huo umetolewa leo jijini Dodoma na Makamu wa Rais Dk Philip Mpango wakati akizindua Makao ya Taifa ya Watoto katika eneo la Kikombo tukio ambalo limeenda sambamba na siku ya mtoto wa Afrika.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Makamu wa Rais Dk Mpango amesema ni vema jamii ikajijengea tabia ya kuasili watoto ili kuweza kupunguza wimbi la watoto wanaoishi mtaani ambao hujikuta wakizama katika changamoto ya kutumia dawa za kulevya na wengine kuingia kwenye biashara haramu.

Makamu wa Rais Dk Mpango ameitaka pia Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kushirikiana na Ofisi ya Rais-Tamisemi kusimamia huduma katika makao ya watoto ili yaweze kutolewa kwa sheria na taratibu zilizowekwa pamoja na takwa husika.

" Nitumie fursa hii kuwapongeza na kulishukuru Shirika hili la Abbott Fund kwa kutoa kiasi kikubwa cha fedha kusaidia ujenzi wa kituo hiki ambacho kinakwenda kuwa msaada kwa watoto wa Taifa hili.

Ni maelekezo yangu kwa Wizara za Afya na Tamisemi kuhakikisha makao ya watoto hayaanzishwi kiholela lakini pia kuhakikisha kwenye haya Makao kunakuepo na walezi wenye sifa zinazofaa katika kuwahudumia watoto wetu," Amesema Dk Mpango.

Ameongeza kuwa ni wajibu wa Wizara ya Afya na Tamisemi kuhakikisha inafuatilia maendeleo ya vituo hivyo ili kuweza kujua nini kinafanyika sambamba na kuhakikisha watoto wanalelewa katika maadili ya Kitanzania.

" Wizara zinapaswa kufuatilia maendeleo ya makao haya ya watoto, ufuatiliaji utatufanya tujue misaada inayotolewa na washirika wetu wakiwemo Abbott Fund.

Ni vema pia tuhakikishe watoto wetu hawa wanalelewa kwenye maadili yetu watanzania, kuna kituo kimoja nilitembelea badala ya watoto kucheza ngoma za Kigogo walikua wanacheza nyimbo za kihindi, Ni rai yangu kwenu kwamba watoto wetu hawa wanapaswa kulelewa katika maadili, mila na tamaduni zetu watanzania," Amesema Makamu wa Rais Dk Mpango.

Kwa upande wake Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima amesema kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ya Mtoto wa Afrika ni "Tutekeleze Ajenda 2040: Kwa Afrika inayolinda haki za Mtoto" ambapo ajenda 2040 ni matokeo ya mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika waliokutana nchini Ethiopia mwaka 2015 na kutathmini hali ya utoaji wa haki za watoto barani Afrika ikiwa ni sehemu ya kumbukumbu ya miaka 25 ya utekelezaji wa Mkataba wa Afrika wa Haki na Ustawi wa mtoto wa mwaka 1991.

"Ajenda 2040 inahimiza masuala mbalimbali yakiwemo ya utekelezaji wa Mkataba wa Afrika wa Haki na Ustawi wa mtoto wa mwaka 1991 kwa vitendo, kuweka mfumo rafiki wa sera na sheria kuhusu haki za mtoto pamoja na kuwezesha watoto kusajiliwa na kupata vyeti vya kuzaliwa.

Kuimarisha huduma za malezi na makuzi ya mtoto, kuhakikisha kila mtoto anapata elimu, kuimarisha ulinzi wa mtoto dhidi ya vitendo vya ukatili na kuhakikisha watoto wanapata fursa ya kushiriki katika masuala yanayowahusu," Amesema Dk Gwajima.

Nae Mkurugenzi wa Abbott Fund Nchini, Natalia Lebou ameipongeza Serikali ya Tanzania kwa mkakati wa kuhakikisha inalinda haki ya mtoto ambapo ameahidi Shirika lake kuendelea kushirikiana na Serikali katika kulinda haki na ustawi wa watoto.

Lebou amesema mradi huo wa Makao ya Taifa ya Watoto umegharimu kiasi cha Sh Bilioni 12 za Kitanzania ambapo pamoja na makazi ya watoto hao kuna miradi mbalimbali ikiwemo Zahanati, Karakana, Maktaba ya kujisomea, bustani ya mbogamboga na viwanja vya michezo na burudani.

Makamu wa Rais Dk Philip Mpango akikata utepe kuzindua Makao ya Taifa ya Watoto katika eneo la Kikombo jijini Dodoma leo.
Makamu wa Rais Dk Philip Mpango akizungumza katika uzinduzi wa Makao ya Taifa ya Mtoto katika eneo la Kikombo jijini Dodoma ambapo pia tukio hilo lilienda sambamba na maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika.
Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima akizungumza katika uzinduzi wa Makao Makuu ya Taifa ya Mtoto jijini Dodoma leo.
Mkurugenzi wa Shirika la Abbott Fund ambao ndio wafadhili wa Ujenzi wa kituo cha Makao ya Taifa ya Mtoto, Natalia Lebou akizungumza kwenye uzinduzi huo jijini Dodoma leo.
Muonekano wa juu wa Makao ya Taifa ya Mtoto yaliyojengwa jijini Dodom.
Makamu wa Rais, Dk Philip Mpango akiwa katika picha ya pamoja na Waziri wa Afya na Naibu wake pamoja na baadhi ya watoto wanaolelewa kwenye kituo cha Makao ya Taifa ya Mtoto katika eneo la Kikombo jijini Dodoma.
 


No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad