HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, May 5, 2021

Benki ya CRDB yaingia mkataba wa makubaliano na NHIF kurahisisha upatikanaji wa Bima ya Afya kwa Wakulima

Ikiendeleza jitihada zake za kumkomboa mkulima nchini, leo, Benki ya CRDB imesaini mkataba wa makubaliano na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kurahisisha upatikanaji wa bima ya afya kwa wakulima. 

Akizungumza katika hafla hiyo ya utiaji saini mkataba wa makubaliano, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema ushirikiano huo utawawezesha wakulima kupata bima ya afya za NHIF kwa mkopo. Katika makubaliano hayo Benki ya CRDB kupitia itakuwa ikisaidia kulipa gharama za bima ya afya (premium) na wakulima kulipa mwisho wa msimu baada ya kuuza mazao.

Akielezea taratibu za upatikanaji wa huduma hiyo ambayo imepewa jina la “Ushirika Afya Premium Loan,” Nsekela alisema huduma hiyo itatolewa kwa wakulima ambao wapo katika vyama vya ushirika huku pia ikiwanufaisha wategemezi yao, kwa maaana ya mke/ mume na watoto.

“Mkopo hutolewa kulingana na kiwango cha gharama za malipo ya bima ya afya (premium) ambapo kwa mtu mzima ni shilingi 76,800 na mtoto shilingi 50,400,” aliongezea Nsekela huku akibainisha kuwa mkopo huo wa bima ya afya utatolewa bure bila ya makato wala riba yoyote.

Aidha, kupitia huduma hiyo ya “Ushirika Afya Premium Loan,” Mkulima pia anaweza kuchukua kifurushi cha familia cha malipo ya shilingi 355,200 ambapo atapata bima ya afya kwa watu 6 (watu wazima 2, watoto 4). Nsekela alisema wamefanya hivyo ili kutoa kuhamasisha wakulima kukata bima kwa familia zao.

“Dhumuni letu ni kusaidia jitihada za Serikali kuboresha afya za Watanzania kwa kuhakikisha watanzania wote wanapata bima ya afya kama ambavyo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa akisisitiza,” alisema Nsekela huku akibainisha kuwa wameanza na kundi la wakulima kwasababu ndio sekta inayoajiri watu wengi zaidi nchini.

 “…ukiboresha afya ya mkulima umeboresha afya ya Tanzania. Ni Imani yangu kuwa utaratibu huu wa bima ya afya ni suluhu kubwa ya kila mkulima kuipatia kaya yake uhakika wa matibabu wakati wowote,” alisema.

Akizungumza kwenye uzinduzi wa mpango huu, Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Bernard Konga aliweka wazi kuwa, Mfuko umejipanga kuhakikisha unawahudumia kikamilifu wakulima ili wawe na uhakika na shughuli zao za kilimo katika kipindi chote cha mwaka.

“Lengo kubwa la mpango huu ni kuwawezesha wakulima wawe na uhakika wa afya zao kwa maana ya kupata huduma za matibabu wakati wowote wanapozihitaji na kwa upande wa Mfuko tumeboresha zaidi huduma zetu ili mwanachama wetu asipate usumbufu wa aina yoyote,” alisema Konga.

Alisema kuwa endapo wakulima wataitumia fursa hiyo vizuri itawapa ufanisi katika uzalishaji mali kwani wakati wote mkulima anakuwa na amani lakini pia mapato yake yatatumika kwa maendeleo na sio kulipia huduma za matibabu.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (watatu kulia) na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Bernard Konga (wapili kushoto) wakikabidhiana hati za makubaliano ya kurahisisha upatikanaji wa bima ya afya kwa wakulima wa mazao ya kimkakati baada ya kusaini, mbele ya Mrajisi wa Vyama vya Ushirika Tanzania, Dkt. Benson Ndiege (watatu kushoto), wakati wa hafla fupi iliyofanyika Mei 5, 2021 jijini Dar es salaam. Wengine pichani ni Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Benki ya CRDB, Tully Esther Mwambapa (wapili kulia), Mwanasheria wa Benki ya CRDB, Pascal Mihayo (kulia) pamoja na Mwanasheria wa NHIF, Benjamin Mwalugaja.



No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad