Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM,) Mkoa wa Dar es Salaam Kate Kamba akiweka shada la maua na kusali katika kaburi la Hayati. Askofu Getrude Rwakatare mara baada ya kumalizika kwa ibada maalumu ya kuenzi maisha yake iliyofanyika katika kanisa la Mlima wa Moto Mikocheni, Mkoani Dar es Salaam.
*********************
Ni mwaka mmoja tangu afariki dunia, familia yasema ipo imara kuendeleza maono yake bila kuacha
Watanzania washauriwa kukumbuka kauli ya Hayati JPM "Tumtegemee Mungu" kila siku IKIWA umetimia mwaka mmoja tangu kifo cha Askofu wa kanisa la Mlima wa Moto na Muasisi wa shule za St. Mary's Hayati.Dkt. Getrude Rwakatare familia, waumini pamoja na viongozi mbalimbali wa siasa na serikali wamemuenzi kwa kusherekea maisha yake pamoja na maono aliyoyabeba kwa jamii ya watanzania ambayo yataenziwa kizazi hadi kizazi.
Akizungumza mara baada ya ibada maalumu ya kumuenzi askofu Rwakatare iliyofanyika katika kanisa la Mlima wa Moto Mikocheni, Mkoani Dar es Salaam Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM,) Mkoa wa Dar es Salaam Kate Kamba amesema, Askofu Rwakatare anakumbukwa kwa ujasiri na kujituma katika kuhakikisha jamii inapata huduma muhimu ikiwemo elimu na ibada.
"Kwa miaka 70 aliyoishi Mama Rwakatare alitumia vyema muda wake kwa kuwekeza kwenye vitu vinavyoendelea ikiwemo nyumba za ibada, redio, na shule..Tunamshukuru Mungu kwa ya Mama Rwakatare amethibitisha kuwa wanawake tunaweza." Amesema.
Amesema, wakati wa uhai wake Askofu Rwakatare alikuwa na mchango mkubwa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alilolitumikia kwa vipindi kadhaa na amewapongeza watoto wake kwa kumuenzi Mama yao kwa kushirikiana na kushirikisha kanisa katika kuhakikisha maono yake yanazidi kuangaza kizazi kwa kizazi.
Kuhusiana na Taifa kutokumbwa na kimbunga Jobo kama ilivyotangazwa na Mamlaka ya hali ya hewa (TMA,) Bi. Kamba amesema ni Mungu pekee ambaye daima amekuwa akisikia maombi ya watanzania kwa nyakati tofauti ikiwemo kipindi cha mlipuko wa virusi vya Corona vilivyoikumba dunia na amewakumbusha watanzania kuendelea kuenzi, kukumbuka na kufanyia kazi neno kubwa lililoachwa na aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Joseph Magufuli la kumtegemea Mungu katika nyakati zote.
Kwa upande wake mtoto wa Hayati Askofu Rwakatare Dkt.Rose Rwakatare amemuelezea Mama yake kupitia barua aliyoiandika kwa mwaka mmoja ambao hawakuongea, na kueleza kuwa kanisa, familia na watanzania bado wanayaenzi maono yake bila kuyaacha.
"Mchango wa Askofu Rwakatare umewagusa wengi na kila alichoanzisha kinaendelea vizuri na mbegu alizopandikiza kwa watoto, wasimamizi wa shule na waumini zinazidi kuwa nuru katika kuhakikisha maono yaliyobebwa na Mama yetu kipenzi yanaendelezwa.....Kanisa na matawi yake, redio na shule zinaendelea vizuri tumefanya maboresho aliyokuwa anataka na ufaulu umekuwa ukipanda kila mwaka." Amesema Dkt.Rose.
Pia amesema wataendelea kutoa huduma hizo kwa jamii ya watanzania katika kuhakikisha wanajenga taifa imara la vijana makini kupitia elimu wacha Mungu na wenye kuleta tija kwa jamii.
Kwa upande wake Mutta Rwakatare ambaye pia ni diwani wa Kata ya Kawe amesema Askofu Rwakatare amewawekeza kiroho na kutanguliza maombi kwa kila jambo na kuwaomba waumini na watanzania wa ujumla kushirikiana katika kuhakikisha ndoto na maono ya Hayati. Askofu Rwakatare yanagusa wengi zaidi.
"Hakuna binadamu mkamilifu, tunaanguka mara nyingi nawaomba tusameheane kama Mama alivyokuwa anatufundisha." Amesema.
Awali Askofu wa kanisa hilo Rose Mgeta amewataka waumini wa kanisa hilo kuendelea kumuenzi Mama Rwakatare kwa kusoma na kusikiliza maandiko yake ambayo yatadumu na kuenziwa kizazi hadi kizazi.
Askofu Mgeta amesema, umoja, mshikamano na maombi yana nguvu zaidi katika kuendesha gurudumu hilo ambalo aliyelianzisha alitwaliwa na Mungu Aprili 20, 2020.
No comments:
Post a Comment