Na WAMJW- ARUSHA
KATIBU
MKUU Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof.
Mabula Mchembe ametoa wito kwa wananchi kuwahi kwenda kupata matibabu
katika vituo vya kutolea huduma za afya kuliko kujitibia nyumbani jambo
linaloweza kuhatarisha maisha ya mtu kwa kiasi kikubwa.
Prof.
Mchembe ameyasema hayo leo wakati alipofanya ziara ya kukagua hali ya
utoaji huduma za afya, katika Hospitali ya Selian (Arusha Lutheran
Medical Centre) na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Arusha (Mount Meru)
ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya kikazi kukagua hali ya utoaji
huduma za afya nchini.
"Nitoe wito kwa wananchi pale inapotokea
matatizo ya kuumwa ni vizuri kwenda katika vituo vya kutolea huduma za
afya na kuonwa kuliko kusema kwamba unajitibia nyumbani jambo ambalo ni
hatari kwa afya yako, hospitali zimejengwa kwa ajili ya kutoa huduma."
amesema Prof. Mchembe.
Prof. Mchembe aliendelea kutoa rai kwa
wananchi kujitahidi kujenga tabia ya kuchunguza afya zao mara kwa mara
ili kufahamu hali zao na kuweza kuanza matibabu mapema endapo
itagundulika kuwa na tatizo la kiafya.
Aidha, amesisitiza kuwa,
sio kila tatizo ambalo analipata mgonjwa katika mfumo wa hewa ni Corona,
huku akiweka wazi kuwa wengi wana matatizo ya moyo, matatizo ya
kisukari na matatizo ya figo ambayo kwa kiasi kikubwa yanapelekea shida
katika upumuaji.
"Tujitahidi sana kupima Afya zetu, kwasababu
kuna wagonjwa wengi walio hospitali wana matatizo ya moyo, na kisukari
na matatizo ya figo, sio matatizo yote yanahusishwa na Corona, mengine
yanahitaji matibabu." Amesema Prof. Mchembe.
Akijibu swali
kuhusu taarifa za uzushi juu ya kujaa kwa wagonjwa katika hospitali hizo
Prof. Mchembe amesema kuwa, ni vizuri kwa wanasiasa kujiridhisha kwa
kutembelea katika maeneo ya kutolea huduma za afya kabla ya kutoa kauli
zao ambazo hazina ukweli wowote, huku akisisitiza vitanda vipo wazi na
hospitali hizo zinaendelea kutoa huduma kwa wananchi.
Kwa upande
wake Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre
(Serian) Dkt. Paul Kisanga amesema kuwa, shida ya wagonjwa kuchelewa
kwenda kupata matibabu katika vituo vya kutolea huduma za afya, ni jambo
linaloweza kupelekea kupoteza maisha kwa mgonjwa.
"Tatizo kubwa
ambalo tunalipata katika hospitali sasahivi ni watu kuja wakiwa
wamechelewa, sio tu kwa matatizo ya kifua, hata matatizo ya upasuaji,
sasahivi pia tunapata shida ya watu kuwa na tabia ya kujitibu nyumbani
hata wanapokuwa na matatizo mengine kama kisukari na moyo," amesema.
Aliendelea
kwa kutoa rai kwa wananchi, kuwahi kwenda kupata matibabu ili wataalamu
wapate nafasi ya kuwarudisha katika mzunguko wa kawaida wa afya zao na
kuendelea na ujenzi wa Taifa, huku akisisitiza kuwahi kupata huduma
kutasaidia kupunguza gharama kwa mtu binafsi, hospitali na Taifa kwa
ujumla.
Nae Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa
Arusha (Mount Meru), Dkt. Alex Ernest amesema kuwa, Hospitali ya Mount
Meru imejipanga vizuri kutoa huduma bora kulingana na miongozo
inayotolewa na Wizara ya Afya.
KATIBU MKUU Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe
No comments:
Post a Comment