HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, December 14, 2020

Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda apongeza uwezeshaji unaofanywa na Benki ya CRDB kwa Wanawake


 
Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda akipata maelezo kutoka kwa Meneja Mahusiano Tawi la Oysterbay, Witness Kileo kuhusu uwezeshaji unaofanywa na Benki yetu kwa Wanawake kupitia CRDB Malkia wakati wa Mkutano Mkuu wa Pili na Madirisha uliofanyika jumamosi hii katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar es Salaam. 
 
Waziri Mkuu Mstaafu Mheshimiwa Mizengo Pinda amepongeza jitihada zinazofanywa na Benki ya CRDB katika kuwawezesha wanawake wajasiriamali nchini kupitia huduma ya CRDB Malkia. Mheshimiwa Pinda ametoa pongezi hizo wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Pili wa Jukwaa la Uwezeshaji Wanawake la MADIRISHA uliofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) ambapo Benki ya CRDB ilikuwa ni mdhamini mkuu. 
 
“Nimefurahishwa kusikia hapa tayari mmeshafanya uwezeshaji wa zaidi ya shilingi bilioni 600 kwa wanawake wajasiriamali kupitia CRDB Malkia. Uwezeshaji huu unaleta chachu ya wanawake wengi zaidi kushiriki katika shughuli za Maendeleo katika taifa letu. Hongereni sana,” alitoa pongezi Mheshimiwa Pinda.
 
Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Pinda akizungumza katika Mkutano Mkuu wa Pili na Madirisha uliofanyika jumamosi hii katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar es Salaam. 
 
Mheshimiwa Pinda aliipongeza Benki hiyo pia kwa ushiriki wake katika makangamano na semina mbalimbali za uwezeshaji akisema kwa kufanya hivyo kunasaidia kufikisha elimu ya ujasirimali na masuala ya fedha kwa wanawake zaidi. Tafiti zinaonyesha ni asilimia 60 tu ya Wanawake ndio waliofikiwa na huduma za kifedha huku wengi wao wakiwa nyuma katika shughuli za ujasiriamali kutokana na kukosa elimu.
 
“Leo hii mmetoa elimu nzuri sana juu ya fursa za uwezeshaji zinazotolewa na Benki hii. Niwapongeze lakini niwasihi mfikishe elimu hii kwa wanawake wengi zaidi mjini na vijijini,” aliongezea Mheshimiwa Pinda. 
 
Akizungumzia kuhusiana na huduma za uwezeshaji kwa Wanawake zinazotolewa na Benki ya CRDB, Mheshimiwa Pinda alipongeza hatua ya Benki hiyo kupunguza riba ya mikopo inayotolewa kwa wanawake wajasiriamali kutoka asilimia 24 hadi asilimia 14.
 
“.. Kupungua huku kwa riba na masharti mengine yaambatanayo kunatoa fursa kwa Wanawake wengi zaidi kunufaika na CRDB Malkia,” alisema Mheshimiwa Pinda huku akiwahamasisha Wanawake wote kujitokeza kwa wingi kuchangamkia fursa hizo zinazotolewa na Benki yao ya CRDB.
 
Akiwasilisha mada katika mkutano huo, Meneja Uwezeshaji Wanawake Benki ya CRDB, Rehema Shambwe alisema huduma ya CRDB Malkia imelenga katika kumtambua, kumpa nafasi na kumuwezesha mwanamke wa Kitanzania kufikia malengo yake kupitia mikopo ya biashara na ujasiriamali, kujiwekea akiba kwa akaunti ya Malkia na mafunzo ya uendeshaji biashara. 
 
“Mpaka kufikia mwishoni mwa mwezi June mwaka huu, Benki yetu tayari ilikuwa imekwisha toa mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 600 kwa wanawake zaidi ya elfu 55,” alisema Rehema huku akibainisha kuwa zaidi ya wanawake 30,000 tayari wameshajiunga na akaunti ya Malkia. 
 
Rehema alisema pamoja na mafanikio ambayo Benki ya CRDB imeyapata katika kumuwezesha mwanamke, bado idadi ndogo ya wanawake wamekuwa wakijitokeza kupata huduma kutokana na changamoto ya riba, masharti magumu ya dhamana na kukosa uelewa wa huduma za kifedha.
 
“Tukiwa Benki ya kizalendo inayothamini mchango wa wanawake katika maendeleo ya taifa letu, tukasema ni vyema tukatafuta suluhisho la changamoto hizi ili kuweza kumsaidia mwanamke kufankisha malengo yake zaidi,” alisisitiza Rehema. 
 
CRDB Malkia sasa hivi inawawezesha wanawake kupata mikopo kwa riba ndogo ya asilimia 14 kulinganisha na asilimia 24 iliyokuwa ikitozwa mwanzo huku masharti ya upatikanaji wa mikopo yakirahisishwa kwa kiasi kikubwa. 
 
“Kupungua kwa riba kuna maana wanawake sasa wanaweza kukopa zaidi na kwa gharama nafuu kulinganisha na mwanzo hivyo kusaidia kufanikisha malengo yao kwa uharaka zaidi,” alisema Rehema.  
 
Rehema alibainisha kuwa kupitia CRDB Malkia, Benki ya CRDB pia imeanzisha huduma ya Malkia Rafiki katika mitandao wake wa matawi ambao watakuwa wanawasidia wanawake kupata huduma stahili kwa uharaka na elimu juu ya huduma hizo ili kuwawezesha kufikia lengo.
 
Naye Muanzilishi na Mwenyekiti wa Jukwaa la MADIRISHA, Fatma Kange aliishukuru Benki ya CRDB kwa udhamini iliyoutoa kufanikisha Mkutano Mkuu huo ambao kwa mara ya kwanza umeweza kuhudhuriwa na wanawake zaidi 1,000.
 
“.. Wanawake sasa tumepata Benki kimbilio na sehemu ya kuelezea mahitaji yetu. Tuishukuru Benki ya CRDB kwa kutushika mkono na kwa kutuheshimisha Wanawake kupitia CRDB Malkia,” alisema Fatma Kange huku Akitoa rai kwa Wanawake wote kuchangamkia fursa zinazotolewa na Benki hiyo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad