HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, December 23, 2020

BODI YA BARABARA PWANI YAOMBA TARURA KUONGEZEWA NGUVU ILI KUBORESHA BARABARA ZA VIJIJINI

 

NA MWAMVUA MWINYI, PWANI

WAJUMBE wa kikao cha bodi ya barabara mkoani Pwani ,wameazimia kuiomba Serikali kuangalia namna ya kuunganisha wakala wa barabara (TANROADS ) na TARURA na kuwa chini ya Wizara moja ili kuboresha huduma za mjini na vijijini ama kuongeza mgawanyo wa fedha kwa TARURA kutoka asilimia 30 na kufikia asilimia 40.

Mabadiliko hayo yatasaidia TARURA kuongeza ufanisi wa kutatua changamoto ya ubovu wa miundombinu ya barabara na kuboresha barabara hasa maeneo ya vijijini ambapo wananchi wanapata kero zaidi.

Akizungumza wakati akifunga kikao hicho,mkuu wa mkoa wa Pwani ,mhandisi Evarist Ndikilo alieleza, TARURA inapaswa ipewe nguvu kwa kuongezwa fedha za utekelezaji kutoka asilimia 30 hadi 40 na TANROADS itoke kwenye asilimia 70 na kuwa 60 ili kuiongezea ufanisi TARURA.

"TANROADS inafanya kazi kubwa na TARURA inafanya kazi kubwa lakini kwasasa TARURA inahemewa na barabara nyingi za vijijini huku ikiwa na bajeti ndogo ya utekelezaji .

Aidha TARURA inashindwa kupandisha hadhi baadhi ya barabara zake kwani ni lazima ipige hodi kwa waziri mwenye dhamana anaeshughulika na TANROADS .
"Utekelezaji wake ni mgumu kidogo ,wanakwama kiutendaji ,huku wananchi wa vijijini wakiendelea kupata shida na wakibakia kuziba mashimo na kufanya ukarabati zaidi kuliko kujenga barabara mpya kutokana na bajeti ndogo" alieleza Ndikilo.

Mbunge wa jimbo la Chalinze ,Ridhiwani Kikwete alisema ,jimbo la Chalinze ni miaka minne mfululizo haijabahatika miradi inayotekelezwa kwa fedha za TARURA .

Kutokana na hilo ,mkuu wa mkoa Ndikilo alielekeza apelekewe taarifa ya ufafanuzi wa kila halmashauri ,jumla ya miradi mipya na ya zamani ,mgawanyo wa fedha ili kujiridhisha.

Mkuu wa wilaya ya Mkuranga,Filberto Sanga aliomba Serikali kuangalia namna ya kuunganisha wakala hizo ama kuiongezea fedha TARURA kwani kipindi kilichopita wakulima wa korosho walishindwa kufikisha korosho zao barabarani kutokana na barabara za vijijini kuwa mbovu .

Nae meneja wa TANROADS Mkoani Pwani, Yudas Msangi alieleza bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021 ni bilioni 35.318 ambapo bilioni 24.297 ni ya matengenezo na bilioni 11.021 ni ya miradi ya maendeleo.

Alifafanua pia ,tatizo walilonalo ni fedha kushindwa kusainiwa kwa wakati hivyo fedha zinachelewa na kushindwa kutekeleza majukumu yao .

Hata hivyo alibainisha,wananchi wanadai fidia ya bilioni 57 ,ambako wanatakiwa wapishe ujenzi wa barabara mbalimbali katika mkoa huo.

Kwa upande wake TARURA Mkoa bajeti ni bilioni 11.243 ambapo matengenezo ni bilioni 6.993, huku bilioni 2.95 miradi ya maendeleo na bilioni 1.3 miradi maalum.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad