HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, November 2, 2020

SHEREHE YA KUAPISHWA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI DK.HUSSEIN ALI HASSAN MWINYI

 

Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu(kushoto) akimuapisha Dk.Hussein Ali Mwinyi kuwa rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, hafla iliyofanyika uwanja wa Amani Unguja.(PICHA NA MARYAM CHARLES AKZ).

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi, akiwahutubia wananchi mara baada ya kuapishwa kuwa rais huko Amani Unguja leo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi,akikagua gwaride maalum la kumuapisha rais huko katika uwanja wa Amani Unguja.

RAIS mstaafu wa awamu ya saba Dk.Ali Mohamed Shein, akiwapungia mkono wananchi ikiwa ni ishara ya kuwaaga baada ya kumaliza muda wake wa kuongoza nafasi ya kiti cha urais wa ZanZibar.


Jaji Mkuu wa Zanziibar, Omar Othman Makungu akimuapisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Hussein Ali Haasan Mwinyi (kulia) kuongoza Zanzibar kwa awamu ya 8 kuanzia 2020-2025 sherehe za kiapo zilizofanyika leo katika uwanja wa Amaan Studium Jijini Zanzibar.
[Picha na Ikulu.]

NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi, amesema serikali atakayoiunda itashirikiana na vyama vya upinzani vilivyokubali na kuridhishwa na matokeo ya urais yaliyotokana na uchaguzi mkuu uliofanyika octoba 28,mwaka huu.

Ahadi hiyo aliitoa wakati akiwahutubia wananchi mara baada ya kuapishwa kuwa rais wa awamu ya nane wa serikali ya Mapinduzi Zanzibar, katika hafla iliyofanyika uwanja wa Amani Unguja.

Alisema anawapongeza wagombea wa vyama vya upinzania waliokubali matokeo ya uchaguzi na kuheshimu maamuzi ya wananchi na ninatoa ahadi ya kushirikiana nao katika serikali atakayounda.

"Ndugu zangu ninawapongeza wagombea wenzangu kwa nafasi ya urais ambao wameyakubali matokeo ya uchaguzi na kuheshimu maamuzi ya wananchi na ninatoa ahadi ya kuwa nitashirikiana nao katika serikali nitakayoiunda katika kuwatumikia wananchi na kuijenga Zanzibar,"alisema.

Katika hotuba hiyo Dk Mwinyi alisema amepata imani kubwa kutokana na maelezo yaliyotolewa na mgombea urais wa chama cha ADA-TADEA Juma Ali Khatib, Oktoba 29 mwaka huu wakati wa kutangaza matokeo ya urais  Maruhubi ambaye alitoa neno la shukurani kwa niaba ya vyama vya mbalimbali vya siasa vilivyoshiriki kinyanganyiro cha hicho.

 

Alisema ahadi na kauli zao zimempa matumanini makubwa ya kushirikiana katika kuendelea kuijenga Zanzibar mpya yenye neema tele kama alivyowahidi wananchi kwa upande wa Unguja na Pemba wakati wa kampeni.

"Kama nilivyozungumza wakati napokea matokeo ya uchaguzi pale Maruhubi na leo naomba nirejee tena lengo letu ni kuijenga Zanzibar na Zanzibar mpya itajengwa na sisi sote bila ya kujali tofauti zetu za kiitikadi nina waahidi nipo tayari kuyaridhia maridhiano yaliokatika katiba yetu ya Zanzibar na kushirikiana na nyinyi kuijenga Zanzibar mpya na Zanzibar ni muhimu kuliko tofauti zetu,"alisema.

Katika maelezo yake Dk.Hussein alisema Serikali atakayoiunda itaongoza katika misingi ya haki,uwajibikaji,uwazi,usawa kwa wananchi wote bila ya kumbagua mtu yeyote kutokana na itikadi ya jinsia,siasa,dini ama eneo analotoka.

Alisema Wazanzibar wote ni wamoja na wana haki ya kunufaija na rasilimali zilizopo  kwa misingi ya usawa"Ninachowaahidi ni kuunda serikali makini,"alisema.

Alisema katika serikali atakayoiunda atazingatia nidhamu, maadili ya viongozi,watumishi wa umma,utendaji kazi wenye viwango bora,kasi ya kimaendeleo ya kiuchumi,kuimarisha huduma za kijamii kwa kuzitumia vyema rasilimali zilizopo kwa manufaa ya Wanzanzibar.

Aliahidi kuwa katika kipindi cha uongozi wake atahakikisha anashirikiana na viongozi atakaowateua pamoja  na wananchi katika kufanikisha utekelezaji wa mipango mikuu ya maendeleo ikiwemo muongozo uliomo katika  ilani ya uchaguzi ya (CCM) ya mwaka 2020/2025, dira ya maendeleo ya Zanzibar ya mwaka 2020-2050,malengo ya maendeleo endelevu ya kimataifa pamoja na ahadi alizozitoa kwa wananchi wakati wa kampen.

"Nawashukru wote mliojitokeza katika sherehe hii muhimu ya kihistoria wakiwemo viongozi wa staafu na mabalozi wa mataifa mbalimbali ,"alisema.

Aliwashukuru  wananchi kwa kujitokeza kwa wingi kupiga kura  Oktoba 28  hii ni kielelezo cha kuonyesha namna mlivyokomaa kisiasa,kidemokrasia na kutambua kuwa uchaguzi ndio njia sahihi kuwapata viongozi wa Zanzibar kwa misingi ya sheria.

"Sote tunathamini sana heshima mliotupa ambao ni kielelezo cha upendo wenu kwa CCM na sisi tutahakikisha tunatekeleza wajibu wetu ipasavyo kwa kuwatumikieni katika kuziinua hali za wananchi ili ziwe bora zaidi,"alisema.

Katika hotuba yake hiyo Dk.Hussein aliyoitoa mara baada ya kuapishwa na Jaji mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, kuwa Rais wa awamu ya nane wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, alisema aliwambia wananchi kuwa atatekeleza ufanisi ahadi zote alizotoa wakati wa kampeni za uchaguzi.

Wakizungumza kwa wakato tofauti baadhi ya wazee wa CCM  Zanzibar, wamesema wana matumaini makubwa na Rais wa Zanziba DK. Hussein Ali Mwinyi katika kufanya mageuzi ya kiuchumi na mabadiliko makubwa katika visiwa vya Zanzibar kama anavyofanya Dk. John Pombe Magufuli kwa upande wa Tanzania bara.

Wamesema, wanaimani kwamba DK. Mwinyi ataunda baraza la Mawaziri amalo atafanya nalo kazi vizuri katika kuwatumikia wananchi na sambamba na kusimamia suala la rushwa na ubadhilifu wa mali za umma ili Zanzibr iendelee kuwa na maendeleo.

Alisema Dk. Mwinyi aliahidi mbele ya wanzanzibar atakapoingia madarakani atasimamia kwa nguvu zote suala la rushwa wabadhilifu wa mali za umma na wazembe.

Aidha alisema mategemeo mengine kwa kiongozi huyo kama alivyoahidi wananchi kupita katika ngazi za chini na kutoa nafasi kwa wananchi kusikiliza changamoto zao.

"Kuna changamoto za wananchi ambazo zitakiwa zimfikie mwenyewe kiongozi ili aweze kutekeleza vyema majukumu yake vizuri nategemea sana Dk mwinyi atakuwa rais wa mfano na aina yake hata akimaliza muda wake rais anaekuja atafata nyanyo zake,"alibainisha.
     
Naye mjumbe wa baraza la wazee wa CCM Zanzibar Mzee Haji Machano, alisema CCM imepata ushindi wa kishindo usiokuwa na manunguniko kutokana na wananchi wengi kumkubali Dk. Hussein Mwinyi.

Alisema CCM imepata ushindi kutokana na ilani na sera zake zilizotolewa kwa wananchi na hata viongozi waliopita akiwemo Dk. Ali Mohammed Shein na Dk. John Pombe Magufuli kutekeleza ilani ya CCM mwaka 2015/2020 kwa kiwango kikubwa.

"Magufuli na Dk. Shein wamefanya mambo ambayo yamesababisha wananchi kuvutika ikiwemo ujenzi wa barabara, elimu, afya, maji, umeme na miundombinu nyengine muhimu," alisema.

Sababu nyengine iliyosababisha CCM kupata ushindi alisema ni pamoja na Rais Mteule Dk. Hussein Ali Mwinyi kushuka kwa wananchi kusikiliza kero zao na kuyaahidi makundi mbalimbali.

"Zanzibar sio masikini tuna kipato kikubwa kutokana na wananchi wake tulivyo na mapato tunavyokusanya ni mengi tunaaimini Zanzibar itaendelea kubadilika kimaendeleo," alisema.

Kwa uade wake, Khadija Jabir Mohammed, alisema wazee, vijana, wanawake na watoto wana matumaini makubwa na kiongozi huyo kwani ni muadilifu na nia thabit ya kuwaletea maendeleo wananchi wake.

Alisema, wanawake wana imani kubwa sana juu ya uongozi wa DK. Mwinyi na hiyo ni kutokana na busara zake na maneno aliyokuwa akiyasema wakati wa Kampeni.

Mapema octoba 29,mwaka huu Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) ilimtangaza Dk. Hussein Ali Mwinyi wa CCM kuwa mshindi kiti cha Urais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar baada ya kupata kura 380,402 sawa na asilimia 76.27 ya kura zote.

Akitaza matokeo hayo Mwenyekiti wa ZEC Jaji mstaafu Hamid Mahmoud alisema wagombea uraisi walikuwa 17 waliopigiwa kura 498,786 sawa na asilimia 88.07 ya wapiga kura 566,352 waliojiandikisha amesema kura zilizoharibika 10,944 sawa na asilimia 2.19.

Kwa mujibu wa kifungu cha 96 (2 na 3)ya sheria namba 4 ya 2018 namtangaza rasmi Dk.Hussein Ali Mwinyi wa CCM kuwa amechaguwaliwa na wananchi wa Zanzibar kuwa mshindi wa kiti cha uraisi wa Zanzibar katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 28,2020 amesema.

NAMNA DK.MWINYI ALIVYOWASILI UWANJANI

Baada ya kuwasili uwanjani hapo Dk.Mwinyi aliambatana jopo la majaji lilokuwa likiongozwa na Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu na viongozi wengine akiwemo Spika wa Baraza la Mapinduzi Zubeir Ali Maulid,Katibu Kiongozi wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee wakiwa wanaelekea katika jukwaa la kiapo.

Wengine waliokuwa katika maandamano hayo ni Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar(ZEC) Jaji mstaafu Hamid Mahmud, Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar ,viongozi wa dini pamoja na wazee wawili ambapo kati yao mmoja akitokea Unguja na mwingine akitokea Pemba.  

Baada ya kufika kwenye jukwaa hilo la kiapo Dk.Mwinyi alikula kiapo

DK.SHEIN ALIVYOAGWA

Baada ya kuwasili uwanjani hapo Rais Dk.Ali Mohamed Shein alipewa heshima ya kwa kupigiwa mizinga na kupata fursa ya kukagua gwaride kwa mara ya mwisho lenye umbile la omega ambapo wakati akikagua gwaride hilo helikopta ilipata kwenye juu kwenye uwanja huo ikiwa ishara ya kuagwa.

Mbali na hilo,Dk.Shein pia alipata fursa ya kuwaga wananchi waliojitokeza uwanjani hapo kwa kupanda gari maalum lilokuwa wazi kuelekea kwenye jukwaa la kiapo lilokuwa likisukumwa na viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama vya Zanzibar kupitia mbele ya jukwaa kuu ikiwa ni ishara ya kukamilika rasmi serikali ya awamu ya saba.

VIONGOZI WALIVYOWASILI

Miongoni mwa viongozi waliohudhuria uwanjani hapo ni Rais mstaafu wa awamu ya pili ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ali Hassan Mwinyi,rais mstaafu wa awamu ya nne Jakaya Kikwete,Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama Jenerali venance Mabeyo.

Wengine waliohudhuria kwenye sherehe hizo ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd,Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa,Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Samia Suluhu Hassan na Makamu wa rais mstaafu Dk. Mohammed Gharib Bilal

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad