HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Saturday, October 31, 2020

NMB yatoa vifaa vya Afya Iringa, Kagera

 

Katika kuadhimisha mwezi wa huduma kwa wateja, Benki ya NMB kupitia Mameneja wake wa huduma kwa wateja wa Kanda ya Dar es Salaam, Nyanda za Juu na Kanda ya Ziwa imetoa vifaa mbalimbali vya Afya vyenye thamani ya sh. milioni Tisa, katika mikoa ya Iringa na Kagera ikiwa ni sehemu ya kurudusha kwa jamii.

Mbali na vifaa hivyo, wafanyakazi wa NMB Tawi la Iringa wametoa vifaa vya shule kwa wanafunzi wa shule za msingi Mapinduzi, Wilolesi na Saint Dominic na baadae kuwapa wanafunzi wa shule hizo elimu juu ya masuala ya kifedha. 

Katika Mkoa wa Iringa, vifaa vilivyokabidhiwa kwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ni; mashuka, vitanda vya kujifungulia kwa akina mama, na vitu mbalimbali kama pampasi, mafuta ya kujipak na sabuni kwa ajili ya watoto.
Mkuu wa Idara ya Huduma kwa Wateja wa NMB - Abella Tarimo (mwenye rasta) akikabidhi sehemu ya msaada wa vitu mbalimbali kwa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Rufaa Iringa (kushoto kwake) Dk. Robert Salim na Mganga Mfawidhi Dk. Alfred Mwakalebela (kulia)
Mkuu wa Idara ya Huduma kwa Wateja wa NMB - Abella Tarimo (mwenye rasta) akikabidhi sehemu ya msaada wa vitu mbalimbali kwa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Rufaa Iringa (kushoto kwake) Dk. Robert Salim na Mganga Mfawidhi Dk. Alfred Mwakalebela (kulia) 

Akimkabidhi vifaa hivyo Mganga Mkuu wa Mkoa Dk. Robert Salim, Mkuu wa Idara ya Huduma kwa Wateja wa NMB - Abella Tarimo alisema, Benki ya NMB imejiwekea utaratibu maalum wa kurejesha kwa jamii asilimia moja ya faida wanayoipata ikiwa ni sehemu ya shukrani kwa wadau wa Benki hiyo lakini pia na wafanyakazi hua wanajipanga kwa sehemu yao na kutoa walichonacho kwa jamii. 

Akipokea msaada huo Mganga Mkuu wa Mkoa alishukuru Benki hiyo kwa msaada huo akieleza kuwa umefika wakati muafaka kwani kumekuwa upungufu wa baadhi ya vifaa kulingana na idadi ya wagonjwa wanaohudumiwa hospitalini hapo kutoka ndani na nje ya mkoa.

Dkt. Salim alisema kuwa hospitali hiyo inategemewa na mkoa mzima na mkoa wa jirani hivyo upungufu wa vifaa hivyo upo kwani wagonjwa ni wengi lakini kuna upungufu wa vitanda, mashuka na vitendea kazi hivyo kitendo cha NMB kuleta baadhi ya vifaa hivyo imefanikiwa kutatua changamoto hizo. 

Katika Mkoa wa Kagera, Benki hiyo imekabidhi vifaa vyenye thamani ya shilingi milioni tano katika kituo cha Afya Rubale - Wilaya ya Bukoba Vijijini, ambapo vifaa vilivyotolewa ni vitanda sita na magodoro yake pamoja na mashuka.

Akikabidhi vifaa hivyo Meneja wa Benki hiyo Kanda ya Ziwa Baraka Ladislaus, alisema kuwa NMB imechangia vifaa vya shilingi milioni 25 tangu mwezi Januari mwaka huu kwa ajili ya kuboresha huduma za afya Mkoani Kagera kama sehemu ya jitihada za benki hiyo kuunga mkono hatua za Serikali za kuboresha sekta ya afya nchini. 

Akipokea vifaa hivyo Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo Dkt. Bandiati Gangole alisema kuwa msaada huo utapunguza adha iliyowapata wagonjwa waliofika kupata huduma katika kituo hicho ikiwa ni pamoja na sehemu ya wajawazito kujifungua ambayo kabla ya msaada huo haikuwa na kitanda chochote.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad