HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, September 2, 2020

VYUO VIKUU VYAPEWA WITO KUFANYA TAFITI ZA KUJENGA UCHUMI WA VIWANDA

 

  Katibu Mtendani wa TCU , Profesa Charles  Kihampa akizungumza wakati wa uzinduzi wa maonesho ya vyuo vikuu yanayoendelea katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam leo Septemba 2, 2020.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, sayansi na Teknolojia Dkt. Leonard Akwilapo, akizungumza na kufungua Maonesho ya 15 ya vyuo vikuu yanayifanyika katia viwanja vya Mnazi mmoja jijini Dar es Salaam, leo Septemba 2, 2020

 Mwenyekiti wa Tume ya Vyuo Vikuu nchini, Profesa Mayunga Nkunya akizungumza wakati wa uzinduzi wa maonesho ya vyuo vikuu yanayoendelea katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam leo Septemba 2, 2020
 Viongozi Mbalimbali wakitembelea mabanda katika maonesho ya 15 ya vyuo vikuu yanayoendelea kufanyika jijini.
Na Karama Kenyunko, Michuzi Tv
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Dk. Leonard Akwilapo, ametoa wito kwa vyuo vikuu na taasisi za utafiti kujielekeza zaidi katika kufanya tafiti zenye lengo la kujenga msingi wa uchumi wa viwanda .

Dk. Akwilapo amesema hayo Leo Septemba 2,2020 wakati akifungua maonesho ya 15 ya vyuo vikuu nchini  yanayoandaliwa na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), ambapo vyuo mbambali vimeshiriki maonesho hayo.

Amesema taasisi hizo za utafiti zinatakiwa zifanye utafiti katika maeneo mbalimbali, hususani utafiti wa madini, utalii,uvuvi, Kilimo, mifugo, teknolojia, maliasili za misitu na bidhaa za viwandani.

Aidha, amesema hadi sasa Serikali imeshatoa Sh. Trilioni 1.03 kwa ajili ya kugharamikia elimu bure ya msingi, ambapo hali hiyo imesababisha wanafunzi kuongezeka.

"Elimu hii bure imesababisha wanafunzi kuongeza kwa kasi kubwa kutoka Milioni 8.3 mwaka 2015 hadi kufikia milioni 10.9 mwaka huu, kwa hali hii vyuo vikuu vinatakiwa kupanua udahili wa wanafunzi," amesema Dk.Akwilapo

Katibu huyo, amesema udahili huo ukishatanuliwa utaweza kumudu idadi ya wahitimu watakaomaliza elimu ya bila malipo ngazi ya msingi na Sekondari kwa siku zijazo.

"Idadi ya wanafunzi wa kitado cha kwanza hadi cha nne  nayo imeongezeka kutoka Milioni 1.6, 2015 hadi kufikia Milioni 2.2 mwaka  2019, huku kidato cha sita wakiwa 153,000, ," 

"Kutokana na  idadi hii tunatambua kuwa kutakuwa na ongezeko kubwa la  wanafunzi watakaomaliza elimu ya Sekondari na kuingia vyuo vikuu, hivyo vyuo vinapaswa kuangalia namna ambavyo vitapanua udahili ili kuweza kumudu idadi hii," amesema

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa TCU, Profesa Mayunga Nkunya amesema tume hiyo imeendelea kushirikiana vyuo vikuu kwa kuvishauri vitoe elimu na kuandaa mitaala inayoendana na vipaumbele vya maendeleo ya kitaifa.

Pia, amesema tume hiyo imeimarisha mifumo yake ya utoaji elimu kwa umma na hivyo kuweza kuwafikia wadau wengi zaidi.

"Kwa mara ya kwanza tume imeweza kusajili jumla ya kampuni 14 zinazohusika na udahili wa wanafunzi, 

lengo la usajili huu ni kuwalinda watanzania wanaokwenda kusoma nje ya nchi dhidi ya mawakala wasio waaminifu," amesema 

Amesema TCU imeendelea kutekeleza majukumu yake ya kuwatumikia watanzania katika sekta hiyo ya elimu ya juu ili kuhakikisha wanapata elimu yenye kukidhi viwango vya ubora vya kitaifa, kikanda na kimataifa.

Naye, Katibu Mtendaji wa TCU, Profesa Charles Kihampa amesema katika maonesho hayo jumla ya taasisi 67 zimeshiriki na kuongeza kuwa kati ya hizo 58 ni zile zinazotoa elimu ya juu.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad