Na. Paschal Dotto-MAELEZO
Kutokana
na ukuaji wa teknolojia, huduma ya habari imekuwa ni nyenzo muhimu ya
kuwaweka pamoja watu katika taifa lolote duniani. Teknolojia imeleta
thamani kubwa ya habari hasa katika ukuaji na upatikanaji wa habari
mitandaoni, ikihusisha Youtube, Facebook, Twitter, Instagram na mitandao
mingine ya kijamii. Mitandao hii inawajibu mkubwa wa kujenga jamii na
inapaswa kusimamiwa vyema na wamiliki hususan katika tukio muhimu la
kikatiba kwa wananchi wa Tanzania ambao watakuwa na Uchaguzi Mkuu wa
Rais, Wabunge na Madiwani mwezi Oktoba, 2020.
Ukuaji
huo wa habari mitandaoni uliilazimu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC)
ambayo ipo kisheria kwa kifungu cha 4C cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi
sura ya 343, ikiwa na jukumu kubwa la kusimamia na kuratibu shughuli
zote za uchaguzi wa Rais na Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
na Madiwani kwa upande wa Tanzania Bara kutoa elimu ya mpiga kura kwa
Watanzania wote wenye haki ya kufanya hivyo.
Hivi
karibuni NEC, ilikutana na wanahabari wanaotoa huduma ya habari
mitandaoni na kuwapa mafunzo juu ya kuwaelimisha wananchi makosa
mbalimbali yanayoweza kutokea na kuharibu mchakato mzima wa wananchi
kutekeleza haki yao ya kikatiba ya kuchagua viongozi katika ngazi zote.
Aidha,
NEC ilifafanua makosa matano ambayo wananchi wanapaswa kuyaepuka ili
kutekeleza vyema zoezi ya upigaji kura katika maeneo yao. Kwa kutambua
umuhimu na haki hiyo ya kutekeleza jukumu hilo, NEC walitoa elimu kwa
waandishi wa vyombo vya habari za mitandaoni ili waweze kuwaelimisha
wananchi kuhusu makosa ya uchaguzi.
Afisa
Elimu, Idara ya Habari na Elimu kwa Mpiga kura, Titus Mwanzalila
alibainisha makosa hayo kuwa ni makosa ya uandikishaji ambayo yanatokana
na mwananchi na mpiga kura kutoa taarifa za uongo kwa madhumuni ya
kujipatia kadi ya mpiga kura.
“Makosa
haya ni yale yanayotokea wakati wa uandikishaji na au uboreshaji wa
Daftari la Kudumu la Mpiga Kura na yanaambatana na kutoa taarifa za
uongo, kujiandikisha zaidi ya mara moja, kuomba kadi ya pili bila
maelezo maalum na kutoa tamko linalohusu kupotea kwa kadi ya mpiga
kura.Makosa haya yote yameainishwa katika kifungu cha Sheria ya Taifa ya
Uchaguzi na. 88(3)”, anaeleza Mwanzalila.
Alieleza
kuwa kupatikana na hatia ya makosa hayo kwa mwananchi kutamuondolea
sifa ya kutekeleza wajibu wake lakini pia adhabu yake ni faini
isiyopungua laki moja au tatu au kifungo cha miaka miwili au vyote kwa
pamoja
Mwanzalila
alibainisha makosa mengine kuwa yanaweza kutokea wakati wa uchaguzi,
uteuzi, daftari na makosa yanayohusu kadi ya mpiga kura, katika kifungu
namba 89A cha makosa ya wakati wa uchaguzi yameelezwa na kifungu namba
89(1) makosa ya uteuzi yameelezwa kwa hiyo mwananchi anapaswa kufuata
sheria ili kutekeleza majukumu yake kikatiba bila kuvunja sheria.
Makosa
yanayohusu daftari na kadi za wapiga kura katika Sheria ya Taifa ya
uchaguzi ambayo yako katika kifungu namba 90(1) (9), ambapo kinamtaka
mwananchi kutoghushi au kuharibu daftari la wapiga kura, lakini pia
kutoharibu na kuchafua kadi ya mpiga kura.Kifungu hicho kinaeleza kuwa
kufanya hivyo kutamsababishia mwananchi kupigwa faini ya shilingi laki
mbili au kifungo cha miaka miwili jela.
Aliongeza
kuwa makosa mengine ni yahusianayo na fomu za uteuzi au karatasi za
kura yaliyoelezwa kifungu namba 91 (1) (a), kumdhamini mgombea urais
zaidi ya mmoja kifungu namba 91(1) (b) kughushi au kutengeneza karatasi
bandia kifungu namba 91 (1) (c) na msimamizi wa uchaguzi kushindwa
kuweka alama rasmi katika karatasi ya kura imeelezwa katika kifungu
namba 91(1) (d). Makosa yote yanaepukika ikiwa mpiga kura atafuata
Katiba na Sheria katika kutekeleza wajibu wake.
Katika
kutekeleza wajibu wa mwananchi kikatiba Sheria ya Taifa ya Uchaguzi
inaeleza kuwa ni makosa kutangaza uongo kijitoa kwa mgombea yeyote kwa
wananchi ili kumsaidia mgombea mwingine kushinda. Kosa hili linaangukia
kwenye kifungu namba 102 (2) (c), ambacho kinampa mhusika adhabu ya
kupigwa faini ya shilingi laki mbili au kifungo cha miezi 12 au vyote
kwa pamoja, lakini pia masuala ya rushwa yamelezwa kwenye kifungu namba
91 B na adhabu yake ni kifungo kisichozidi miaka mitano.
Kosa
lingine ni pamoja na kutoa hongo au kushawishi kutoa hongo ambayo
yameelezwa katika kifungu cha 94 na adhabu yake ni faini isiyopungua
shilingi laki tano na isiyozidi shilingi milioni moja au kifungo
kisichopungua mwaka mmoja na kisichozidi miaka mitatu au vyote kwa
pamoja.
Kutokana
na elimu inayotolewa na NEC kwa njia mbali mbali kupitia kwenye vyombo
vya habari na mikutano mbalimbali, wananchi wanatakiwa kujiepusha na
makosa yanayoweza kuwafanya kushindwa kutekeleza wajibu wao wa kikatiba
wa kupiga kura au kwa kufahamu au kwa kutofahamu ili wajiepushe
kukumbana na kukumbana na mkono wa sheria na wakati mwingine adhabu
zilizotajwa na Tume.
No comments:
Post a Comment