HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, September 6, 2020

MAJALIWA: TUTAENDELEA KUKUZA SEKTA YA UTALII

 


Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimsikiliza Katibu Mkuu wa CCM Mstaafu, Abdulrahman Kinana ambaye aliwaomba wananchi wa Arusha wampigie kura, Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Wabunge na Madiwani wa CCM katika mkutano wa kampeni za CCM uliohutubiwa na Waziri Mkuu kwenye uwanja wa Relini jijini Arusha
Mgombea  ubunge wa CCM katika Jimbo la Arusha Mrisho Gambo (kulia)  akikumbatiana na Philemon Mollel (MONABAN) mmoja wa watia nia waliowania uteuzi wa CCM katika kugombea jimbo hilo . Walikuwa katika mkutano wa kampeni  uliohutubiwa na Mjumbe wa Kamti Kuu ya CCM Taifa na Waziri Mkuu, Kassim  Majaliwa kwenye uwanja wa Relini jijini Arusha, Septemba 5, 2020. Monaban alitamka hadharani kuwa hana kinyongo na Gambo na kwamba atashiriki kumpigia kampeni.
Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akimkabidhi Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020-2025 mgombea Ubunge wa CCM katika Jimbo la Arusha, Mrisho Gambo katika mkutano wa kampeni  kwenye uwanja wa Relini jijini Arusha
Wananchi wa jiji la Arusha wakimsikiliza Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  wakati alipohutubia mkutano wa kampeni kwenye uwanja wa Relini, . (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
………………………………………………………………
 *Asema lengo ni kuhakikisha Watanzania wanapata ajira
MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali itaendelea kuimarisha sekta ya utalii nchini kwa kusimamia ipasavyo mikakati ya kukuza vivutio ili kuhakikisha Watanzania wengi wakiwemo wakazi wa jiji la Arusha hususani vijana wananufaika kwa kupata ajira.
Amesema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli imeweza kupata mafanikio mbalimbali katika sekta ya utalii yakiwemo kuongeza idadi ya watalii kutoka 1,137,182 mwaka 2015 hadi kufikia 1,510,151 mwaka 2019, ambapo amewaomba wananchi wandelee kuiamini Serikali yao.
Aliyasema hayo jana jioni (Jumamosi, Septemba 5, 2020) alipohutubia mkutano wa kampeni uliofanyika katika uwanja wa Relini jijini Arusha baada ya kumuombea kura Rais Dkt. John Pombe Magufuli na mgombea ubunge jimbo la Arusha, Mrisho Gambo na wagombea udiwani wa CCM.
“Sekta ya utalii ina umuhimu mkubwa katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya wananchi hususani kwa vijana kwa sababu vijana wengi wameajiriwa na kujiajiri kupitia sekta ya madini. Serikali inawahakikisha kwamba itaendelea kuboresha mazingira ili kuweza kuvutia watalii wengi zaidi kuja nchini.”
Alisema kutokana na maboresho mbalimbali yaliyofanywa na Serikali katika sekta hiyo mapato yatokanayo na shughuli za utalii nchini yameongezeka kutoka Dola za Kimarekani milioni 1,901.95 mwaka 2015 hadi kufikia Dola za Kimarekani milioni 2,612.99 mwaka 2019.
Waziri Mkuu alisema mafanikio yote hayo yanatokana na uongozi thabiti na makini wa Rais Dkt. Magufuli, hivyo amewaomba wana Arusha na Watanzania kwa ujumla kumchagua tena ili aweze kutekeleza mikakati mingine ya kuongeza wigo wa utalii aliyoianzisha nchini.
“Ndugu wanaArusha na Watanzania wote sina shaka kwamba mtakubaliana na ombi langu la kuwataka tumchague tena Rais Dkt. Magufuli kwa sababu mnapenda maendeleo na kwa Tanzania mtu atakayewaletea maendeleo si mwingine bali ni Dkt. John Pombe Magufuli tujitokeze kwa wingi kumpigia kura.”
Akizungumzia kuhusu Ilani ya uchaguzi ya CCM ya 2020-2025 alisema inaielekeza Serikali ya Chama Cha Mapinduzi kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuboresha sekta ya utalii ikiwa ni pamoja na kukuza wigo wa bidhaa na mazao ya utalii.
Ilani imeelekeza Serikali ihakikishe inaongeza idadi ya watalii na  kufikisha watalii 5,000,000 kwa mwaka ifikapo 2025 na kuongeza mapato kutoka Dola za Kimarekani bilioni 2.6 mwaka 2020 hadi Dola za Kimarekani bilioni 6.0 mwaka 2025.
Pia kushirikisha sekta binafsi na kuandaa wataalam wa ukarimu na kuwatambua wataalam wenye ujuzi na weledi unaohitajika katika utoaji wa huduma za utalii ili kukuza sekta hiyo na kuongeza ajira kwa wananchi na pato la Taifa kwa kubuni na kutekeleza mikakati ya kuweka mazingira wezeshi ili sekta binafsi na umma zishiriki kikamilifu katika uwekezaji wa utalii.
Kadhalika, Waziri Mkuu alizungumzia kuhusu suala la bima ya afya, ambapo alisema Serikali iweka mikakati Madhubuti inayowawezesha wananchi kutibiwa ikiwa ni pamoja na kupitia Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ambapo wananchi wanachangia kiasi kidogo na Serikali inawaongeza na kuwawezesha kutibiwa bure wao na familia zao.
Pia, Waziri Mkuu aliongeza kuwa utaratibu mwingine ni kupitia Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) ambao ni maalumu kwa ajili ya watumishi wa umma kuchangia kiasi kidogo kupitia mishahara yao na mpango huo unawawezesha kutibiwa bure, hivyo hakuna tatizo la huduma ya bima ya afya nchini. Amewataka wananchi wasikubali kupotoshwa na waendelee kuiamini Serikali yao.
Aidha, katika ilani ya Uchaguzi ya 2020-2025 imeilekeza Serikali kuimarisha mfumo wa bima ya afya nchini ikiwamo mifuko ya bima za afya (NHIF na CHF) ili kufikia lengo la serikali la kuwa na bima ya afya kwa wananchi wote.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad