HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, September 6, 2020

MAJALIWA AHUTUBIA MKUTANO WA KAMPENI UWANJA WA MAJENGO MOSHI

 

Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimuombea kura mgombea ubunge wa CCM wa jimbo la Moshi Mjini, Priscus Tarimo katika mkutano wa kampeni kwenye uwanja wa Majengo mjini Moshi, Septemba 6, 2020. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).
Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akihutubia mkutano wa kampeni kwenye uwanja wa Majengo mjini Moshi, Septemba 6, 2020. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
*********************************

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli imeandaa mazingira mazuri ya kuwawezesha Watanzania kujikwamua kiuchumi wakiwemo wafanyabiashara wadogo.

Ameyasema hayo leo (Jumapili, Septemba 6, 2020) alipohutubia mkutano wa kampeni uliofanyika katika Kata ya Kirima Juu wilayani Moshi mkoani Kilimanjaro wakati akimuombea kura Rais Dkt. John Pombe Magufuli na mgombea ubunge wa Jimbo la Moshi Vijijini, Profesa Patrick Ndakidemi na wagombea udiwani.

“Nimekuja hapa kuwaomba sana kura yenu ya ndio kwa Rais Dkt. Magufuli kwani mkiwa sehemu ya Watanzania mnafahamu kazi kubwa ya kupeleka maendeleo aliyoifanya nchi nzima bila ya ubaguzi wa aina yoyote, tuhakikishe tunampigia kura nyingi ili akaendeleze kazi aliyoianza.”

Pia, Mheshimiwa Majaliwa amesema Serikali ya CCM imejenga miradi mingi ya kimkakati ikiwemo ya afya, maji, elimu, umeme, barabara, viwanja vya ndege kwa ajili ya kuboresha maendeleo ya Watanzaniaya. Serikali imetengeneza fursa katika maeneo mbalimbali zilizowezesha wananchi kujikwamua kiuchumi.

Akizungumzia kuhusu miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na Serikali katika halmashauri ya wilaya ya Moshi, Waziri Mkuu amesema jumla ya sh. bilioni 2.1 zimetumika kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha Afya Uru Kyaseni, Uru Kusini na Okaoni pamoja na upanuzi na ukarabati wa zahanati za Kahe, Kilema, Kisao, Chemchemi, Mowo, Kitowo na Kituo cha Afya Shimbwe. Pia sh bilioni 12.2 zilitolewa kwa ajili ya ununuzi wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi.

Kuhusu elimumsingi bila ada, Mheshimiwa Majaliwa amesema Serikali imetoa bilioni sh. 4.8 kwa ajili ya ukarabati, utawala, michezo, mitihani na posho kwa maafisa elimu kata na walimu wakuu katika shule za msingi 252 kwenye halmashauri ya wilaya ya Moshi.

“Serikali imetoa shilingi bilioni 10.2 kwa ajili ya fidia ya ada, chakula kwa shule za bweni na posho ya madaraka kwa Wakuu wa Shule katika shule za sekondari 59 kwenye halmashauri ya wilaya ya Moshi.”

Amesema shilingi bilioni 1.6 zimetumika kwa ajili ya ujenzi na ukamilishaji wa vyumba vya madarasa 18, matundu ya vyoo 109, bwalo moja, nyumba sita za walimu na jengo moja la utawala na ununuzi wa mashine ya kudurufu mitihani katika shule za msingi Maweni, Mahoma, Ngaroni na Saghana.

Pia, Waziri Mkuu amesema sh. bilioni 7.3 zimetumika kwa ajili ya ujenzi na ukamilishaji wa vyumba vya madarasa 26, matundu vyoo 45, maabara 14, mabweni sita na ujenzi wa nyumba za walimu katika shule za sekondari za Ashira, Umbwe, Sakayo Mosha na Muungano, Kisarika, Shimbwe na Kimochi.

Amesema Serikali imetoa sh bilioni 5.3 kwa ajili ya miradi mikubwa ya maji ya Lyamungo-Umbwe, Njiapanda, Tella Mande, Mamba-Mruma, Shimbi Mashariki, Leto na Ngareni. Pia imetoa sh. bilioni 6.3 kwa ajili ya miradi mingine ya visima virefu ya Mweka, Mamba Kusini, Mang’ana, Kyaronga, Kiwaya na Rudugai, Kaloleni, Mkashilingi, Vyanzo vya Kipure, Nikodemo na Mrusungu.

Aidha Mheshimiwa Majaliwa alitumia jukwaa hilo kuvunja makundi ya wanachama wa CCM waliogombea nafasi ya ubunge na kuwaeleza wananchi kuwa Chama Cha Mapinduzi kinautaratibu wakati wa mchakato wa ndani, ambapo baada ya uteuzi wa chama wanaCCM wote huungana na kuwa kitu kimoja.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad