Mtendaji Mkuu wa Shirika lisilo la kiserikali la Empower Society
Transform Lives (ESTL), Joshua Ntandu, akizungumza katika kikao kilicho
wakutanisha wadau mbalimbali wa Kata ya Kinyagigi katika Wilaya ya
Singida Vijijini kwa ajili ya kuunda kamati za vijiji za kupinga vitendo
vya ukatili wa kijinsia mwishoni mwa wiki. Kutoka kulia ni Afisa
Maendeleo ya Jamii wa wilaya hiyo, Veronika Mure na Afisa Maendeleo ya
Jamii wa Kata ya Kinyagigi, Nives Mapunda.
Afisa Maendeleo ya Jamii wa wilaya hiyo, Veronika Mure, akizungumzia majukumu ya Mtakuwwa.
Wadau wakipitia mwongozo wa Mtakuwwa.
Afisa Maendeleo ya Jamii wa Kata ya Kinyagigi, Nives Mapunda, (katikati) akizungumza katika kikao hicho.
Afisa Mtendaji wa Kata ya Kinyagigi, Hamisi Mohamed, akizungumza katika kikao hicho.
Mwakilishi wa vijana wa kata hiyo, Alfred Mohamed, akizungumza kwenye kikao hicho.
Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Mitula, akichangia jambo kwenye kikao hicho.
Majadiliano yakifanyika.
Kiongozi wa Dini ya Kikristo, Emanuely Ng'eni, akizungumza kwenye kikao hicho.
Mmoja wa Wajumbe wa kikao hicho, Jackline Alute akizungumza.
Na Dotto Mwaibale, Singida
SHIRIKA lisilo la kiserikali la Empower Society Transform Lives
(ESTL)limewakutanisha wadau mbalimbali wa Kata ya Kinyagigi katika
Wilaya ya Singida Vijijini kwa ajili ya kuunda kamati za vijiji za
kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia.
Wadau waliokutanishwa na shirika hilo ili kupata mafunzo ya kupinga
ukatili wa kijinsia na kuunda kamati hiyo ni wakunga wa jadi, walimu wa
afya mashuleni, wahudumu wa afya ngazi ya jamii, waganga wa tiba asilia,
mangariba na watu wenye mahitaji maalumu.
Kikao hicho kilicho keti mwishoni mwa wiki katika kata hiyo kililenga
kuunda kamati za vijiji zitakazokuwa zikifuatilia vitendo vya ukatili
katika wilaya hiyo pamoja na kupitia mpango kazi wa Taifa wa kutokomeza
ukatili dhidi ya wanawake na watoto (MTAKUWWA 2017/18 hadi 2021/22.
Akizungumza katika kikao hicho, Mtendaji Mkuu wa Shirika hilo, Joshua
Ntandu alisema shughuli hiyo inafanyika kwa ufadhili wa Ubalozi wa
Finland Dar es Salaam kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi
Halmashauri ya Wilaya ya Singida vijijini kwa kutekeleza mradi huo
katika Kata tano ambazo ni Maghojoa, Mwasauya, Merya, Munghunga na
Kinyagigi.
Alisema
shughuli ambazo kamati hiyo itazifanya kwa kushirikiana na shirika hilo
ni kukutana na kina mama wanaohudhuria kliniki na kuwapa mafunzo, kutoa
mafunzo kwa viongozi wa dini, vijana walio nje ya shule,wanafunzi
mashuleni na kuimarisha klabu za wanafunzi (KLABU JUU)
Alitaja shughuli nyingine ni kuandaa midahalo ya wazi ya kujadili
namna ya kutokomeza mila potofu na kufanya mikutano ya hadhara.
Kwa
upande wake Afisa Maendeleo ya Jamii wa wilaya hiyo, Veronika Mure
alisema majukumu ya kamati hiyo nikuhakikisha utekelezaji wa mpango kazi
huo na shughuli za hutoaji huduma kwa makundi yaliyo katika mazingira
hatarishi unaendana na mikataba ya Kikanda na Kimataifa ya haki na
ustawi wa Wanawake na Watoto pamoja na Sera, Sheria na Miongozo ya
Serikali.
Washiriki wa kikao hicho walisema vitendo vya ukeketaji na matukio
ya ukatili wa kijinsia bado ni changamoto na kwamba maovu hayo
hufanyika kwa siri kubwa.
“Matukio
ya vitendo vya ukeketaji na ukatili wa kijinsia bado vinafanyika na
kibaya zaidi watuhumiwa wakikamatwa na kufikishwa polisi au mahakamani
huachiwa hivyo kuleta sintofahamu miongoni mwa jamii" alisema mmoja wa
wajumbe hao Jackline Alute.
Alute alisema suala la ukeketaji, mimba na ndoa za umri mdogo
yamekuwa ni matukio ya kawaida na hakuna hatua zozote zinazochukuliwa
hata baada ya kumbaini mtuhumiwa walalamikaji na ndugu wa mtuhumiwa
hukutana na kuyamaliza kiaina.
Katika kikao hicho wajumbe hao walijifunza mbinu za kuibua vitendo
vya ukatili wa kijinsia na jinsi ya utoaji wa taarifa kwa vyombo husika
kwa kushirikiana na ESTL.
Washiriki hao walipata fursa ya kukaa katika makundi na kutengeneza
mpango kazi utakaowaongoza katika kutekeleza majukumu yao dhidi ya vita
ya matukio ya ukatili wa kijinsia na ukeketaji ambapo kila baada ya
miezi mitatu watakuwa wakifanya kikao cha tathmini.
“Lengo la mpango kazi wetu huu ni kutusaidia kuanza kuibua matukio
yote ya ukatili, kuhamasisha jamii kuacha kufanya vitendo hivyo na
kufanya ufuatiliaji na hatimaye kutoa taarifa kwa MTAKUWWA na kwenye
mfumo wa Tehama uliobuniwa na ESTL ili kutoa taarifa za matukio ya
ukatili kwa kutumia namba 0710567003, “ alisema Alfred Mohamed.
No comments:
Post a Comment