HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 14, 2020

BAGAMOYO YAKEMEWA KWA KUKITHIRI MIGOGORO YA ARDHI-RC NDIKILO

 


Na Mwamvua Mwinyi, Bagamoyo
MKUU wa mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo, amewajia juu maafisa tarafa, watendaji wa vijiji na kata, wilayani Bagamoyo kuhakikisha wanatimiza wajibu wao wa kazi na kutatua kero za wananchi ikiwemo migogoro ya ardhi, ndani ya mwezi mmoja kabla hajachukua maamuzi mazito dhidi yao.

Aidha ameeleza ,wilaya hiyo imehemewa na migogoro ya ardhi hali inayosababisha baadhi ya wananchi badala ya kukimbizana na maendeleo wanakimbizana na mashauri ya migogoro hiyo katika mabaraza ya ardhi na mahakamani.

Akizungumza katika ziara yake aliyoianza mkoani Pwani, kusikiliza kero za wananchi, akianzia Bagamoyo, Ndikilo ameshtushwa kupokea malalamiko 88 ambayo mengi yapo ndani ya uwezo wa kutatuliwa ngazi ya chini.

Ndikilo alielezea, mabaraza ya ardhi kata pia hayafanyi kazi kiufanisi na ni chanzo cha migogoro hali inayosababisha baraza la ardhi Kibaha kuhemewa na mashauri.

"Hii inaashiria watendaji wa chini hawawajibiki, naweza kuandika mapendekezo muondoke wote na nawapa salamu msipokaa sawa mtaondoka."

Hata hivyo Ndikilo alibainisha, idara ya ardhi ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Bagamoyo wasichelewe kufanya maamuzi ya mashauri ya wananchi kwani inasababisha kero.

"Mchukue hatua haraka kulingana na mashauri yao, malizeni kwa muda mfupi." Wananchi wanataka haki zao, teteeni wanyonge kama hana haki ijulikane kuliko kuzungushwa." Alisisitiza Ndikilo.

Pamoja na hilo ,mkuu huyo wa mkoa alivitaka vyombo vya dola kushughulikia vikundi vya kiuhalifu vinavyolalamikiwa na wauzaji ardhi wanaotumia mabavu ili kulinda raia na mali zao .

Nae mkuu wa wilaya ya Bagamoyo ,Zainab Kawawa alieleza kero zinazohusu kushughulikiwa na ofisi ya mkuu wa wilaya atazifanyia kazi na zipo ambazo kishaanza kuzishughulikia .

Kwa upande wa wananchi akiwemo Swaiba, mzee Hussein Mfaume, Asha Mwambala na Amina Ramadhani wanakabiliwa na migogoro ya ardhi miaka mingi na tatizo lipo katika kuchelewesha mashauri wanayoyapeleka.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad