HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Sunday, October 13, 2019

RC MNYETI AAGIZA WALIONYANG'ANYWA ARDHI KITETO WAPEWE MAENEO MENGINE

 MKUU wa Mkoa wa Manyara, Alexander Pastory Mnyeti ameagiza wakazi wawili wa Wilaya ya Kiteto walionyang'anywa maeneo yao na kujengwa  taasisi za Serikali wapewe maeneo mengine. 

Mnyeti alitoa agizo hilo kwenye mkutano wa hadhara wakati akizungumza na wananchi wa kata za Matui na Bwawani, wilayani Kiteto kwenye ziara yake ya siku tano ya kukagua miradi ya maendeleo, kusikiliza kero na changamoto za wananchi, kuyapatia majawabu na kuzungumza na wananchi. 

Alisema kutokana na maeneo ya wananchi hao kuchukuliwa na taasisi za serikali na kujengwa shule ingetakiwa wapewe maeneo mengine ili kufidia maeneo yao. 

"Mkurugenzi nakuagiza utoe maeneo mengine wapewe hawa wananchi waliochukuliwa maeneo yao kwa ajili ya kufidiwa kwani japo ni suala la maendeleo lakini wanapaswa kupata haki zao. 

Alisema baadhi ya kero ambazo hazina sababu ya kuachwa zinapaswa kutatuliwa kwani wananchi wengine wataichukia serikali yao bila sababu ya msingi. 

Awali, mkazi wa kijiji cha Matui Juma Masare alilalamikiwa kuporwa eneo lake ekari 12 na serikali ya kijiji kisha ikajengwa shule ya msingi. 

"Baada ya kupora eneo langu serikali ya kijiji ilijengwa shule lakini hawakunifidia sehemu nyingine japokuwa maeneo mengine yapo," alisema Masare. 

Kwa upande wake, mkazi wa kijiji cha Wezamtima kata ya Bwawani, Endeni Kilangi alitoa malalamiko kwa mkuu huyo wa mkoa kuwa alinyang'anywa na serikali ya kijiji hicho ekari zake 70 na kujengwa shule ya msingi. 

"Shamba hilo lilichukuliwa na serikali ya kijiji lakini sikufidiwa eneo lingine sehemu nyingine ili hali kuna maeneo mengine wangeweza kunipa haki yangu," alisema Kiangi. 

Baada ya uamuzi huo wananchi hao walimpongeza Mnyeti kwa kusimamia haki zao kwani ilikuwa ni haki yao kupatiwa maeneo mengine. 

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad