HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, October 7, 2019

MTENDAJI MKUU AMUELEKEZA MKANDARASI KUKAMILISHA HARAKA JENGO LA MAHAKAMA -MANYARA

Na Christopher Msagati, Mahakama ya Hakimu Mkazi-Manyara 
Mtendaji Mkuu- Mahakama ya Tanzania, Bw. Hussein Kattanga amefanya ukaguzi katika jengo jipya la Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara na kuridhishwa na  hatua ya jengo hilo lilipofikia. 

Akikagua jengo hilo mapema Oktoba 06, 2019, Bw. Kattanga alisema, “hatua ya jengo lilipofikia ni nzuri, hata hivyo natoa rai kwa Mkandarasi kukamilisha marekebisho madogo yaliyotolewa ili kazi za Mahakama ziendelee.”

Pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Wajumbe wengine walioambatana nae katika ukaguzi huo ni pamoja na Mhandisi Mkadiriaji Majengo kutoka Mahakama ya Tanzania, Bw. Raphael Bandiho, Wakandarasi wa jengo hilo kutoka Kampuni ya Vumwe General Services and Supplies Limited (VGSS),  Wakala wa Majengo Tanzania (TBA)- Mkoa wa Manyara.

Wengine ni Wasimamizi na washauri katika mradi huu, Tanzania Electrical, Mechanical and Electronics Services Agency (TEMESA-Mkoa wa Manyara) pamoja na wenyeji ambao ni Mtendaji wa Mahakama Mkoa wa Manyara, Bw. Jacob Swalle, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkoa wa Manyara, Mhe. Simon Kobero na Afisa Tawala wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara Bwana Christopher Msagati.

Kwa kipindi kirefu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara ilikuwa ikitumia jengo la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM- Manyara) wakati wakisubiri jengo hilo la Mahakama likamilike. 

Aidha; ilipofika mwezi Agosti mwaka huu shughuli za kuhamia katika jengo hilo jipya zilianza rasmi na walihamia katika upande mmoja wa Jengo ambao tayari ulikuwa umekamilika wakati Mkandarasi akiendelea kukamilisha upande mwingine wa jengo.

Inatarajiwa kuwa mradi wa jengo hili utakamilika hivi karibuni ndipo likabidhiwe rasmi kwa Mahakama kuendelea na shughuli zake kikamilifu.
 Mtendaji Mkuu, Mahakama ya Tanzania, Bw. Hussein Kattanga  (wa tatu kulia) akionyeshwa kitu na Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi, Manyara pindi alipokuwa akikagua jengo la jipya la Mahakama ya Hakimu Mkazi Manyara, Bw. Jacob Swalle pindi alipokuwa akikagua jengo jipya la Mahakama hiyo lililopo katika hatua za mwisho za ukamilishwaji wake.
 Muonekano wa jengo jipya la Mahakama ya Hakimu Mkazi-Manyara lililopo katika hatua za mwisho za ukamilishwaji wa marekebisho madogo madogo.
 Mtendaji Mkuu-Mahakama Hussein Kattanga   akizungumza jambo wakati wa ukaguzi wa jengo hilo

Mtendaji Mkuu-Mahakama ya Tanzania, Bw. Kattanga akiendelea na ukaguzi.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad