HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, June 25, 2019

MANAMUZIKI STEVE WONDER MLEMAVU WA MACHO ANYETAMBA USA

Na Moshy Kiyungi
Baashi watu hukata tamaa pindi wanapojikuta wamezaliwa wakiwa na ulemavu wa aina yeyote ama kupatwa na ulemavu ukubwani. Kwa upande wa Steve Wonder ni tofauti kabisa, akiwa jukwaani kamwe huwezi kubaini kwamba anayepiga muziki ni mlemavu wa macho.

Ni pande na baba lenye upenzi wa kufuga nywele ndefu ‘rasta’ aliye na sauti ya juu na nyororo. Kila umuonapo hakosi kuwa na kuwa ni miwani mieusi usoni kwake. Wasifu wa Steve Wonder unaonesha kuwa alizaliwa Mei 13, 1950 mjini Saginaw, Michigan nchini Marekani.

Jina lake halisi ni Steveland Hardaway Judkins. Muziki anaopiga unatambulika na kukubalika Kimataifa, umletea sifa tele duniani kote. Talanata za mwanamuziki huyo ni mtunzi, mwimbaji wa nyimbo na pia ni mtayarishaji muziki.

Steve ana talanta za ziada za kupiga ala tofauti zikiwemo za upigaji wa ngoma, piano, gitaa, Kongas vilevile ni maarufu kwa kupiga Kinanda na Harmonica. Amekuwa miongoni mwa wasanii wakubwa wenye mafanikio wanaojulikana katika studio maarufu ya kurekodia ya Motown.

Wonder ni mwanaharakati wa haki za binadamu wa Kimarekani, ni kielelezo tosha kwamba ulemavu si kigezo cha kubweteka katika maisha. Kupitia nyimbo zake ameweza kuwa mmoja kati ya wanamuziki matajiri duniani, licha ya kuwa ulemavu huo.

Nguli huyo amekwisha rekodi zaidi ya albamu 23 na kutoa vibao vingi vilivyo maarufu, alizotunga na kuzirekodi. Baadhi ya nyimbo zake aliwashirikisha wanamuziki wengine wenye sifa kubwa katika muziki.

Machi 26, 1985 Serikali ya Afrika Kusini ilitangaza kutopiga miziki ya Steve Wonder kwa sababu ya kitendo alichokifanya wakati akipokea tuzo ya Oscar. Steve Wonder alishinda tuzo ya Oscar katika Category ya wimbo bora wa filamu 'I Just Called To Say I Love You' ulioandikwa kwenye filamu, 'The Woman In Red'.

Katika sherehe hizo Wonder alitamka kuwa anapokea tuzo hiyo kwa Jina la Nelson Mandela. Mandela wakati huo alikuwa bado mfungwa mweusi aliyetaka kuipindua serikali ya Wazungu. Nelson alikuwa wakili pekee aliyeanza kutetea haki za watu weusi wa Afrika ya Kusini.

Katika harakati zake hizo zilipelekea kuhukumiwa kifungo cha maisha mwaka 1964, kwa mashtaka ya kutaka kupindua serikali. Mwaka 1963 Wonder alitoka na wimbo "Fingertips” sehemu ya pili, na mwaka 1966, aliachia nyimbo za "Uptight (Everything's Alright)", "Blowin' in the Wind" na "A Place in the Sun".

Mwaka 1967 alikuja na wimbo wa "I Was Made to Love Her". Steve Wonder amekwisha tunga na kuimba nyimbo nyingi ambazo orodha yake ni ndefu mno. Msomaji wa makala haya nakuomba nikujuze baadhi ya nyimbo zake za karibuni zikiwemo za "From the Bottom of My Heart", "Shelter In The Rain", na So What The Fuss"

Nyimbo hizo zikiwa ni sehemu ya juhudi za Umoja wa Mataifa, kwa kushirikiana na Wasanii wa Kimataifa katika uwanja wa muziki. Katika kusisitiza umuhimu wa furaha katika maisha ya kila siku, Steve Wonder alizindua kampeni na ombi kwa raia wa duniani kuteua wimbo au muziki unaoweza kuleta tabasamu kwa kila mtu. Kampeni hiyo ililenga kuhamasisha matumaini bora.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wakati huo Ban Kin Moon, aliteua wimbo wenye ujumbe wa amani wa Steve Wonder , ambao kwake, unasikika kama sauti za furaha katika uwepo wa makubaliano mapya juu ya malengo ya maendeleo endelevu, katika yote ajenda za viongozi wa Kimataifa zilizoandaliwa kujadiliwa.

Alishiriki kutunga na kuimba wimbo uliowajumuisha magwiji wote wa kuimba Ulimwenguni, uliopewa jina la “We are The World” . Wakati huohuo mkongwe huyo Steve Wonder, amemkaribisha mtoto wake wa tisa ndani ya familia yake baada ya mpenzi wake kujifungua mtoto wa kike waliyempa jina la Nia.

Nia ni mtoto wa pili kwa mpenzi wake huyo anayejulikana kwa jina la Tomeeka Bracy. Kwa sasa Steve Wonder ni baba wa familia ya watoto tisa kutoka kwa wanawake tofauti tofauti aliowahi kuwa nao kipindi cha nyuma.

Bravo Steve Wonder, Mungu akupe maisha marefu.

Mwandishi wa makala haya anapatikana kwa namba: 0784331200, 0713331200, 0736331200 na 0767331200.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad