HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, May 24, 2019

Naibu Waziri wa Nishati, aagiza TANESCO na REA kutatua sintofahamu ya nguzo mkoani Morogoro

Na Teresia Mhagama
Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, ametoa Wiki Moja kwa wasimamizi wa mradi wa usambazaji umeme vijijini mkoani Morogoro kutoka Wizara ya Nishati, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na TANESCO kuhakikisha kuwa wanatatua changamoto ya nguzo za umeme mkoani Morogoro.

Naibu Waziri alitoa agizo hilo, tarehe 23 Mei, 2019 mkoani Morogoro wakati alipofanya ziara ya kukagua kazi ya usambazaji umeme vijijini wilayani Mvomero na Gairo na kuwasha umeme katika Kijiji cha Dibamba wilayani Mvomero na Kijiji cha Sanganjeru wilayani Gairo.

Agizo la Naibu Waziri limekuja baada ya sampuli ya nguzo za mkandarasi wa umeme mkoani Morogoro kupimwa na wataalam wa TANESCO na kuonekana kuwa hazina vigezo huku mkandarasi huyo akidai kuwa sehemu ya nguzo zake zinafaa kwa matumizi ya umeme.

" Hatutaki kuona mivutano kati ya wakandarasi na wasimamizi wa miradi ya umeme vijijini kwani inachelewesha upelekaji umeme kwa wananchi hivyo nawaagiza mtatue suala hili kwa kupima nguzo zote na Wizara ipate taarifa ndani ya Wiki Moja."alisema Naibu Waziri

Kuhusu kasi ya mkandarasi anayesambaza umeme vijijini mkoani Morogoro, kampuni ya State Grid, alisema kuwa, bado haridhishwi na kasi ya mkandarasi huyo na kutoa onyo kuwa Serikali itamchukulia hatua endapo hatatekeleza kazi kwa mujibu wa mkataba.

Aidha alitoa agizo kwa wazalishaji wa vifaa vya umeme, wasambazaji na wakandarasi wa umeme vijijini kutatua changamoto zao kwa haraka mara zinapojitokeza ili kutochelewesha miradi ya umeme vijijini.

Akieleza kuhusu hatua zilizofikiwa na Serikali katika kazi ya usambazaji umeme vijijini, alibainisha kuwa hadi sasa asilimia 57 ya vijiji nchini tayari vimesambaziwa umeme kati ya Vijiji 12,268 huku kazi hiyo ikiendelea na kwamba Tanzania ndiyo inayoongoza katika nchi za Afrika Mashariki kwa usambazaji umeme vijijini.

" Wakati Serikali ya Awamu ya Tano, inaingia madarakani ilikuta vijiji 8783 havina umeme kati ya Vijiji 12,268, ndio ikaanza safari ya kufikisha umeme kwenye vijiji hivyo kupitia miradi mbalimbali ikiwemo huu wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza, mradi wa ujazilizi Awamu ya Pili mzunguko wa kwanza na miradi mingine," alisema Mgalu

Kuhusu bei ya umeme aliendelea kusisitiza agizo la Serikali kuwa ni elfu 27,000 tu, awe anasambaza mkandarasi wa umeme vijijini au TANESCO ili kuleta usawa wa utoaji huduma kwa wananchi.
 Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, akiwasha umeme katika Kijiji cha Dibamba wilayani Mvomero, Mkoa wa Morogoro.
 Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (katikati) akizungumza na wananchi katika Kijiji cha Tabuhoteli wilayani Gairo Mkoa wa Morogoro wakati alipofika kukagua kazi ya usambazaji umeme vijijini. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Siriel Mchembe na kulia ni Msimamizi wa mradi wa usambazaji umeme vijijini kutoka Wizara ya Nishati, Mhandisi Ahmed Chinemba.
 Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (kulia) akikata utepe kuashia uwashaji umeme katika Kijiji cha Sanganjeru wilayani Gairo Mkoa wa Morogoro. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Siriel Mchembe.
 Waziri wa Nishati, Subira Mgalu, akitoa maelezo kuhusu kifaa cha Umeme Tayari (UMETA) kwa wananchi wa Kijiji cha Sanganjeru wilayani Gairo Mkoa wa Morogoro wakati alipofika kijijini hapo kukagua kazi ya usambazaji umeme na kuwasha rasmi umeme.
Wataalam kutoka Wizara ya Nishati, TANESCO na Wakala wa Nishati Vijijini (REA), wakimsikiliza Naibu Waziri wa Nishati, Subira Mgalu (hayupo pichani) wakati akizungumza na wananchi katika Kijiji cha Tabuhoteli wilayani Gairo, Mkoa wa Morogoro.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad