Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani amelitaka Shirika la Umeme
Tanzania (TANESCO) kuendelea kusambaza umeme vijijini mara
wakandarasi wa umeme vijijini wanapomaliza kazi kwa mujibu wa mkataba.
Dkt. Kalemani aliyasema hayo wakati alipofanya ziara ya kukagua kazi
ya usambazaji umeme vijijini katika Wilaya za Mpwapwa na Bahi mkoani
Dodoma ambapo aliambatana na Wawakilishi wa wananchi katika maeneo
hayo, Watendaji wa Wizara ya Nishati, TANESCO na Wakala wa Nishati
Vijijini (REA).
Yapo maeneo ambayo yalishasambaziwa umeme kutoka zamani kupitia
miradi ya usambazaji umeme vijijini hivyo kazi ya TANESCO ni kuendelea
kusambaza umeme kwenye maeneo hayo kwa muda wote badaala ya kuyaacha
tu yakikosa umeme.” alisema Dkt Kalemani.
Akiwa kwenye Wilaya hizo, Dkt Kalemani aliwasha umeme katika Kijiji
cha Igoji na Chinoje vya wilayani Mpwapwa, pia aliwasha umeme katika
Kijiji cha Chikola kilichoko wilayani Bahi na kuahidi umeme utawaka
tarehe 12 Mei, 2019 katika Kijiji cha Chipanga wilayani Bahi.
Akizungumzia kazi za usambazaji umeme katika Wilaya hizo mbili alisema
kuwa, Wilaya ya Bahi ina vijiji 59 ambapo vijiji 19 tayari
vimeshambaziwa umeme na vijiji 40 vilivyosalia vinasambaziwa umeme
kupitia mradi wa REA wa Awamu ya Tatu.
Aidha kwa Wilaya ya Mpwapwa alisema kuwa, Wilaya hiyo ina Vijiji 113
ambapo Vijiji 78 tayari vimesambaziwa umeme huku kazi ya usambazaji
umeme ikiendelea kwenye Vijiji vilivyosalia.
Akizungumza na wananchi katika Vijiji hivyo, Dkt Kalemani aliwaagiza
Mameneja wa TANESCO kwenye Wilaya hizo kuhakikisha kuwa wanafungua
vituo kwa ajili ya kuhudumia wananchi badala ya wananchi kusafiri
umbali mrefu kwenda kutafuta huduma TANESCO.
Kuhusu wakandarasi wa umeme vijijini wanaosuasua katika kazi zao, Dkt
Kalemani alisema kuwa Serikali itachukua hatua kali dhidi yao hivyo ni
vyema wakaongeza kasi katika utekelezaji wa kazi walizopewa na
Serikali.
Kwa upande wake, Mbunge wa Kibakwe, George Simbachwene pamoja na
kupongeza Wizara ya Nishati kwa ufuatiliaji wa karibu wa miradi ya
umeme vijijini alitoa ombi kwa Serikali kuhakikisha wakandarasi wa
umeme vijijini wanasambaza umeme kwa wigo mkubwa na pale mkandarasi
anapomaliza muda wake TANESCO waendelee na kazi ya kusambaza umeme kwa
wananchi.
Vilevile alisema kuwa, kazi ya upangaji wa vijiji au vitongoji
vinavyopaswa kupelekewa umeme ushirikishe wawakilishi wa wananchi ili
kuboresha utaratibu wa usambazaji umeme na hivyo kuepusha malalamiko
yanayoweza kutokea kwa baadhi ya vijiji au vitongoji kuona kuwa
vimerukwa bila sababu za msingi.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akikata utepe kuashiria uzinduzi wa umeme katika Kijiji cha Chinoje wilayani Mpwapwa. Wa kwanza kulia ni Mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene. Kulia kwa Waziri ni Mbunge wa Mpwapwa, George Lubeleje.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akikata utepe kuashiria uzinduzi wa umeme katika Kijiji cha Chikola wilayani Bahi. Kulia kwa Waziri ni MKuu wa Wilaya ya Bahi, Mwanahamisi Munkunda na kushoto kwa Waziri ni Mbunge wa Bahi, Omary Badwel.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani akizungumza katika Kijiji cha Chinoje wilayani Mpwapwa kabla ya kuwasha umeme katika Kijiji hicho. Wa kwanza kulia ni Kaimu Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga na wa kwanza kushoto ni Mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene.
Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (mwenye shati ya bluu)
akizungumza na baadhi ya wananchi katika Kijiji cha Chikola wilayani
Bahi mara baada ya kuzindua huduma ya umeme kijijini hapo. Kulia kwa
Waziri ni Mkuu wa Wilaya ya Bahi, Mwanahamisi Munkunda.
No comments:
Post a Comment