HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, April 15, 2019

TRA YATANGAZA MAKUSANYO YAKE YA MIEZI TISA,YAKUSANYA TRILIONI 11.96

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), imefanikiwa kukusanya jumla ya Shilingi Trilioni 11.96 katika kipindi cha miezi Tisa ya mwaka wa Fedha 2018/19 ikiwa ni kuanzia Julai 2018 hadi Machi 2019. 

Katika robo ya tatu ya mwaka wa fedha 2018/19 TRA, ilifanikiwa kukusanya Shilingi Trillioni 1.30 kwa mwezi wa Januari, Shilingi Trillioni 1.23 kwa mwezi wa Februari na kiasi cha Shilingi Trillioni 1.43 kwa mwezi wa Machi, 2019.  

Mamlaka ya Mapato Tanzania inawashukuru walipakodi wote waliochangia makusanyo hayo kwa  kulipa kodi zao kwa hiari na kwa wakati na kuhimiza wale ambao bado wanasuasua kujitokeza kulipa kodi hizo kwa wakati. TRA inaendelea kuhimiza wananchi wote ambao wana changamoto za kikodi kutembelea ofisi za TRA na kuonana na mameneja wa mikoa na wilaya kwa ufumbuzi wa changamoto hizo.

Aidha, katika kuongeza wigo wa kodi, TRA kwa sasa imeweka utaratibu wa kurahisisha upatikanaji wa Namba ya Utambulisho wa Mlipakodi (TIN) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) ambapo TIN inaweza kutolewa katika ofisi zote za TRA katika ngazi ya Mkoa na Wilaya baada ya mwombaji kuwasilisha kitambulisho cha taifa au kwa kupata namba ya kitambulisho wakati kitambulisho kikiendelea kushughulikiwa . Sambamba na hilo TRA inaendelea kuhamasisha, kutoa elimu ya kodi na kusajili walipakodi wapya katika mikoa, wilaya na vitongoji mbalimbali nchini kote. 

Wakati huo huo, Mamlaka inapenda kuwakumbusha wamiliki wote wa majengo nchini kujitokeza kulipia kodi za majengo haraka kuepuka usumbufu wa kulipa mwishoni kwani kwa sasa viwango ni rafiki na vinalipika. Viwango hivyo kwa mwaka ni Shilingi 10,000 kwa nyumba ya kawaida, Shilingi 50,000 kwa kila sakafu nyumba ya ghorofa katika majiji, Manispaa na halmashauri za miji na Shilingi 20,000 kwa jengo la ghorofa katika maeneo ya halmashauri za wilaya.

Vile vile, TRA inawaasa wale wote wanaojishughulisha na vitendo vya kughushi risiti za kielektroniki za EFD nchi nzima kuacha mara moja kwa sababu wakibainika watachukuliwa hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani. Kila mwananchi na mfanyabiashara atambue wajibu wake wa kudai risiti kwa kila manunuzi na kutoa risiti kwa kila mauzo.

Tunaendelea kuwakaribisha wakazi wa Dar es Salaam kutembelea kituo cha ushauri kwa walipakodi kilichopo katika makutano ya mitaa ya Samora na Bridge katikati ya jiji, karibu na jengo TTCL. Pia wanaweza kupiga simu bure namba 0800 750075 au 0800 780078 na kwa upande wa barua pepe tafadhali tuandikie huduma@tra.go.tz. Vile vile, wanaweza kutuma ujumbe kupita namba ya Whatsapp 0744 233 333.
 Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa kodi TRA, Richard Kayombo akitangaza makusanyo ya yaliyopatikana kwa muda wa miezi 9  kwa waandishi wa habari ambapo kiasi cha Trilioni 11.96 kimepatikana ikiwa ni makusanyo ya kodi mbalimbali nchini mkutano huo umefanyika leo kwenye makao makuu ta TRA Stesheni jijini Dar es Salaam.(Picha na Emmanuel Massaka,MMG) 
 Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa kodi TRA, Richard Kayombo akifafanua jambo kwa wanahabari leo wakati akitangaza makusanyo  yaliyopatikana kwa muda wa miezi 9 ambapo kiasi cha Trilioni 11.96 kimepatikana.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad