HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, March 6, 2019

MKURABITA Yatajwa Kuchochea Maendeleo Endelevu

Na Frank Mvungi- Dodoma
Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) umetajwa kuchochea ustawi wa wananchi na kuendana na azma ya Serikali ya Awamu ya Tano kuwakwamua wananchi kiuchumi baada ya kurasimisha mashamba yao ili kufikia maendeleo endelevu.
Akizungumza wakati akifungua mafunzo kwa wakulima zaidi ya 100  wa Kijiji cha Mahama Wilayani Chamwino mbunge wa jimbo la Chilonwa Mhe. Joel Mwaka amesema kuna umuhimu mkubwa kwa wakulima waliorasimisha mashamba yao na kupata hati za hakimiliki za kimila kutumia fursa zitokanazo za urasimishaji huo .
“ Mpango wa matumizi bora ya Kijiji cha Mahama umewezesha mashamba 1000 yamepimwa na hatimiliki 500 zimeweza kuandaliwa ili ziweze kuwanufaisha wananchi kiuchumi kwa kuongeza tija katika uzalishaji” Alisisitiza Mhe. Mwaka
Akifafanua amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imewekeza fedha nyingi katika uwezeshaji wananchi kiuchumi katika Wilaya hiyo kupitia kuwajengea uwezo wakulima hao, miradi ya maji, elimu na afya, lengo likiwa kuhakikisha kuwa kila mwananchi anakuwa na maisha bora.
Pia aliwaasa wananchi hao kutumia mafunzo hayo vizuri na kutumia ujuzi watakaoupata kuleta mageuzi ya kweli yakiuchumi kupitia sekta ya kilimo, ufugaji na nyinginezo zilizopo katika Wilaya hiyo.
Kwa upande wake mratibu wa MKURABITA Dkt. Seraphia Mgembe  amesema kuwa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano kupitia mpango huo ni kuhakikisha kuwa inawawezesha wananchi kushiriki katika kujenga uchumi na kuwa na uwezo wa kumiliki rasilimali zilizopo katika maeneo yao.
“ Serikali inatambua umuhimu wa kuwezesha wananchi wake ndio maana imekuja kuwajengea uwezo ili mtumie hatimilki za kimila za kumiliki ardhi kujikwamua kiuchumi kwa kuchukua mikopo katika taasisi za fedha ili muweze kuboresha kilimo cha mazao ya biashara hasa alizeti.” Alisisitiza Dkt. Mgembe
Akifafanua Dkt. Mghembe  amesema kuwa wananchi wanapaswa kuunga mkono juhudi zinazochukuliwa na Serikali kupitia mpango huo  ili kujenga msingi  wa maendeleo endelevu yanayoendana na uchumi wa viwanda.
Naye Meneja Urasimishaji wa MKURABITA Bw. Antony Temu amesema kuwa wakulima hao watafundishwa kilimo bora cha alizeti na mahindi, utafutaji wa fursa na kuzitumia, ufugaji wa kuku wa kienyeji, utunzaji wa kumbukumbu, huduma zitolewazo na mabenki hususani kufungua akaunti za kuweka akiba na upatikanaji wa mikopo.
Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kupunguza tatizo la kuwepo kwa rasilimali vijijini zinazomilikiwa na katika mfumo usio rasmi ikiwemo ardhi.
 Mbunge wa jimbo la Chilonwa Wilayani Chamwino Mhe. Joel Mwaka akisisitiza umuhimu wa wananchi kutumia hatimilki za kimila za kimili ardhi kujikwamua kiuchumi baada ya kurasimisha mashamba yao katika Kijiji cha Mahama Wilayani humo leo.
 Mratibu wa Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) Dkt. Seraphia  Mgembe akisisitiza kuhusu dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano kuwalwawezesha wananchi,  Ameyasema hayo  wakati wa hafla ya ufunguzi wa mafunzo kwa wakulima zaidi ya 100 wa kijiji cha Mahama jimbo la Chilonwa wilayani Chamwino mkoani Dodoma mapema leo, mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo wakulima hao ili watumie hatimilki za kimila za kumiliki ardhi kujikwamua kiuchumi.
 Meneja Urasimishaji  Ardhi Vjijini kutoka Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) Bw. Antony Temu akieleza manufaa  ya mafunzo yakuwajengea uwezo wakulima wa kijiji cha Mahama Wilayani Chamwino.
 Mbunge wa jimbo la Chilonwa Mhe. Joel Mwaka akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya wananchi waliopatiwa hatimilki za kimila za kumiliki ardhi leo jimboni humo.
   Kwaya ya kijiji cha Mahama  ikitumbuiza wakati wa hafla ya Ufunguzi wa mafunzo yakuwajengea uwezo wakulima zaidi ya 100 ili waweze kutumia hati milki za kimila za kumiliki ardhi kujiletea maendeleo.
Mmoja wa wananchi wa kijiji cha Mahama  Wilayani Chamwino mkoani Dodoma Bi. Grace Mfereji akipoa hatimilki ya kimila kutoka kwa Mbunge wa jimbo la Chilonwa Mhe. Joel Mwaka leo wakati wa hafla ya kufungua mafunzo yakuwajengea uwezo wakulima zaidi ya 100 wa kijiji hicho, mafunzo hayo yameratibiwa na Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) kwa kushirikiana na Halmashuri ya Wilaya hiyo. (Picha zote na Frank Mvungi- Dodoma)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad