HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, March 6, 2019

Kamati ya Bunge ya Bajeti yafanya ziara katika kiwanda cha Transfoma na kupongeza uzalishaji

Na Teresia Mhagama
Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti wakiongozwa na Mwenyekiti wa Kamati, George Simbachawene wametembelea kiwanda cha kuzalisha transfoma cha TANELEC kilichoko jijini Arusha ili kukagua masuala mbalimbali ikiwemo uwezo wake katika uzalishaji wa transfoma lengo likiwa ni kuhakikisha kuwa nchi inakuwa na vifaa vya umeme vya kutosha.

Katika ziara hiyo waliambatana na Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani na watendaji mbalimbali kutoka Wizara ya Nishati, Shirika la Umeme Tanzania ( TANESCO) na Wakala wa Nishati Vijijini (REA). Baada ya kukagua shughuli za uzalishaji wa transfoma katika Kiwanda hicho, Wajumbe hao kwa nyakati tofauti waliwapongeza watendaji wa Kiwanda hicho kwa kuzalisha transfoma nyingi ambazo ni 14,000  kwa mwaka huku mahitaji ya transfoma nchini kwa mwaka yakiwa ni 10,000.

Aidha Wajumbe hao walipongeza uamuzi wa Serikali wa mwaka 2017 ambao ulielekeza kuwa miradi yote ya umeme nchini itumie vifaa vya umeme vinavyopatikana nchini hali inayopelekea miradi hiyo kutekelezwa kwa kasi. Wajumbe hao pia walimtaka Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo kuongeza uzalishaji na kuwa mbunifu kwa kuangalia pia masoko mengine ya transfoma na si kulenga miradi ya umeme ya ndani ya nchi pekee.

Awali, Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani alisema kuwa, Serikali ilichukua uamuzi wa kusitisha kuagiza nje vifaa vya umeme vinavyopatikana nchini ili kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya umeme. Alitoa mfano kuwa upatikanaji wa transfoma nje ya nchi unaweza kuchukua hadi miezi 12  hali wakati transfoma zinazozalishwa ndani ya nchi zinachukua muda mfupi kufika katika eneo zinapohitajika.

Aidha Waziri wa Nishati alisema kuwa, uagizaji wa transfoma nje ya nchi ni gharama kubwa kwani transfoma moja kutoka nje ya nchi inauzwa kwa takriban shilingi milioni Tisa wakati zinazozalishwa nchini ni takriban shilingi milioni 6.5. Akitoa taarifa ya kiwanda hicho, Mkurugenzi Mkuu wa TANELEC, Zahir Saleh alisema kuwa kiwanda hicho kilichoanzishwa mwaka 1981 kwa sasa kinazalisha transfoma kiasi cha 14,000 kwa mwaka.

Alisema kuwa,  kiwanda kinazalisha transfoma za uwezo wa kvA 50 hadi kVA 5000 na kufanya matengenezo ya transfoma kutoka nchi mbalimbali za Afrika kama Rwanda, Burundi na Kenya. Aliongeza kuwa, uamuzi wa Serikali kuzuia kuagiza vifaa nje ya nchi umekinufaisha kiwanda hicho kwani kabla ya uamuzi walikuwa wakizalisha transfoma 7000 kwa mwaka lakini sasa wanazalisha transfoma 14,000.

Kuhusu ajira alisema kuwa, awali waliajiri wafanyakazi 30 lakini kwa sasa wafanyakazi walioajiriwa ni 70 na kwa mwaka huu wataajiri wafanyakazi wengine 40. Vilevile alisema kuwa, kutokana na uamuzi huo wa Serikali, Kiwanda kinafanya kazi kwa faida na wameanza kupeleka gawio serikalini la takribani shilingi milioni 500 kwa mwaka 2018 na wanategemea kuongeza kiasi cha gawio hilo kwa miaka inayokuja.
 Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani (wa pili kulia) na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, George Simbachawene (wa kwanza kushoto) wakiongoza Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Bajeti katika kukagua kazi zinazofanywa na kiwanda cha transfoma cha TANELEC kilichoko jijini Arusha.
 Wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Bajeti wakiwa katika kiwanda cha kuzalisha transfoma cha TANELEC kilichopo jijini Arusha. Wa Pili kulia ni Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani.
Mkurugenzi Mkuu wa kiwanda cha kuzalisha transfoma cha TANELEC, Zahir Saleh ( wa nne kulia) akiwaongoza wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Bajeti wakati walipotembelea kiwanda hicho kilichopo jijini Arusha. Wa Tatu kushoto ni Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani ambaye aliambatana na Wajumbe hao na wa Tano kushoto ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo, George Simbachawene.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad