Na Said Mwishehe, Globu ya jamii
WAKAZI wa Kata ya Majohe kwa Ngosoma iliyopo Ukonga Gongo la mboto jijini Dar es
Salaam wameiomba Serikali kusaidia ujenzi wa Kituo cha Polisi kwenye kata hiyo ili
kudhibiti matukio ya uhalifu ambayo yamekuwa yakitokea mara kwa mara kiasi cha
kusababisha hofu.
Wakizungumza na Michuzi Blog jijini Dar es Salaam jana na leo kwa nyakati tofauti
wananchi wa kata hiyo wamesema matukio ya uhalifu yamekuwa yakitokea mara kwa
mara , hivyo wanaamini kikijengwa kituo cha polisi itaisaidia kupunguza matukio ya
uhalifu.
Wamesema Kata ya Majohe kwa Ngosoma inalo eneo kubwa na hivyo kuna idadi
kubwa ya wakazi lakini cha kusikitisha hakuna kituo cha polisi licha ya jitihada
mbalimbali kufanywa na Serikali za mitaa.
"Kumekuwa na matukio ya uhalifu huku kwetu na sasa tumechoka kuendelea
kushuhudia yakiendelea kutokea.
Tunaomba Serikali itusaidie kujenga kituo cha
Polisi hasa kwa kuzingatia tayari eneo lilishatengwa na baadhi ya hatua za awali
ziliasha. Tukiwa na kituo cha Polisi itasaidia kudhibiti uhalifu na wananchi tutakuwa
na sehemu ya kukimbilia kutoa taarifa na kupata msaada wa Polisi,"amesema
Shaban Said anayeishi mtaa wa Kichangani.
Ameongeza wiki mbili zilizopita saa mbili usiku , kuna watu wanaosadikiwa ni
majambazi walivamia maduka yaliyopo eneo la Kona na kabla ya kupora fedha
walijeruhi baadhi ya waliokuwamo kwenye maduka hayo na kisha kukimbia eneo la
tukio hilo.
"Tukio ambalo nimelizungumzia ni moja tu lakini kuna matukio ya aina hiyo
yamekuwa yakitokea huku kwetu, hivyo kilio chetu wananchi wa Majohe Kwasoma
tunaomba tujengewe kituo cha Polisi, tuko tayari kuchanga na nakumbuka kuna
kikao kiliitishwa na wananchi wote tukakubaliana kuchanga fedha ili kituo cha Polisi
kijengwe,"amesema Jumanne Joseph anayeishi Majohe Kona.
Kwa upande wa baadhi ya viongozi wa Kata ya Majohe kwangosoma wameiambia
Michuzi Blog kuwa , kuna hatua mbalimbali ambazo znaendelea kuhakikisha kituo
cha polisi kinajengwa hasa kwa kuzingatia eneo lipo na wananchi wanafahamu.
No comments:
Post a Comment