HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, February 5, 2019

MADIWANI MOSHI KUCHUNGUZA TUHUMA ZA UBADHILIFU WA FEDHA KITUO CHA AFYA PASUA

Na Dixon Busagaga wa Globu ya Jamii, Kanda ya Kaskazini
BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi limeeleza kufanyia kazi tuhuma za ukiukwaji wa taratibu katika mradi wa ukarabati wa Kituo cha Afya cha Pasua unaotajwa kupelekea upotevu wa fedha .

Kauli hiyo imetolewa na Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi,Raymond Mboya wakati wa ziara ya Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi walipotembelea kituo cha Afya cha Pasua kujionea ukarabati unavyoendelea.

“Kuna matatizo na hayo matatizo nimesema nije kwanza kuangalia ,kwa kuwa bado hili swala liko kwenye vikao vya ndani tutatoa taarifa yakikamilika kwenye vikao  kwanza, ni kwamba kuna taratibu hazijakaa vizuri kwenye mchakato mzima wa ukarabati wa kituo cha afya.”alisema Mstahiki Mboya .

Alisema fedha zilizotumika katika ukarabati wa kituo hicho ni fedha za serikali zinazotokana na kodi inayokusanywa kutoka kwa wananchi na kwamba zinapotumika ni lazima baraza la Madiwani kufuatilia na kujiridhisha kama zimetumika kwa utaratibu uliokusudiwa.

“Hizi fedha ni kodi zetu ,ambazo wakati mwingine zinaitwa fedha za serikali sasa zinapotumika hapa ni lazima tuhakikishe zinatumika kwa utaratibu uliokusudiwa na kwa utaratbu ambao hauta leta mashaka wala tatizo kwa hiyo tusubiri mchakato na taratibu za vikao zitakapo kamilika tutawajulisheni”alisema Mboya

Akizungumzia kuhusu ukarabati wa Kituo hicho ,Mstahiki Mboya alisema hakuna mradi unaofanyika mahala popote  bila ya kupitishwa katika vikao halali vya baraza la Madiwani na kwamba hadi kuanza kwa ukarabati kwa kituo hicho taratibu zilifuatwa.

“Tangu mwaka 2013 tulikuwa tunatenga fedha kwenye Bajeti ya ujenzi wa vituo vya Afya kikiwemo kituo cha Afya cha Pasua ,na ilikua ni sehemu ya upasuaji ,wodi ya kujifungulia kina mama,chumba cha mionzi ya X-ray na chumba cha kuhifadhi maiti”alisema Mboya .

“Tumekuwa tukitenga na kwa kuwa ukarabati ulitakiwa uwe mkubwa ,tumeendelea kutenga miaka yote na ilivyoingia serikali ya awamu ya tano ikaingia na mkakati wa kuboresha vituo vya Afya na manispaa ya Moshi tulifanikiwa kwa sababu ilikuwa kwenye mpango”alisema Mboya.

Alisema katika ukarabati huo serikali imetoa kiasi cha Sh Mil 400 ikiwa ni mchango wake huku fedha nyingine zikitakiwa kutolewa na Halmashauri hali iliyowalazimu kubadilisha matumizi ya fedha kwa baadhi ya vifungu ili zikamalizie maeneo ambayo bado hayajakamilika katika kituo hicho.

“Kukamilika kwa kituo hichi kutawezesha wananchi wa maeneo ya kata ya Bomambuzi ,Pasua ,Matindigani na Kaloleni waweze kupata huduma ambayo ni ya kiwango na hasa tuilenga kwe nye eneo la wodi ya wazazi.”alisema Mboya .

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Pasua ,Juma Raibu alisema ukarabati wa vituo vya Afya ni mpngo mkakati wa taifa kwa ajili ya kuwasaidia wananchi na kupunguza changamoto zilizokuwa zikiikabili sekta ya Afya nchini.

“Mimi kama Diwani nilipewa maelekezo kwa barua kwamba niunde kamati mbalimbali za kuweza kusaidia ukarabati wa kituo hiki uweze kuendelea ,kamati ya kwanza niliambiwa niunde ya manunuzi,kamati ya mapokezi na kamati ya ujenzi ili wazawa wa eneo hili wawe ni sehemu ya wasiamamizi wa mradi huu”alisema Raibu.

Katika   ziara hiyo Globu ya Jamii ilishuhudia wanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wakiwa wamoja katika kukagua maeneo mbalimbali ya kituo hicho .

Mstahiki Meya ,Raymond Mboya(Chadema)  akazungumzia hali hiyo na kuungwa mkono na Diwani wa kata ya Kilimanjaro ,Priscus Tarimo wakieleza kuwa linapofika suala la maendeleo itikadi za kisiasa huwekwa pembeni.

“Hii inaashiria Moshi tumekomaa ,nah ii inaashiria kwamba kwa nini inaitwa Moshi ,kwamba baada ya uchaguzi kauli yetu ni maendeleo ,anayeleta siasa huwa hatumpia nafasi ,na ndio maana mimi kama Meya kwenye baraza nawaambia tunaongea lugha ya maendeleo”alisema Mboya.

Naye Diwani Tarimo akaeleza juu ya hali hiyo “Mazingira ya ya kisiasa katika mkoa wa Kilimanjaro hasa katika manispaa ya Moshi ni tofauti sana kutokana na uelewa mkubwa wa watu na inawezekana kabisa madiwani wa pande zetu tukakaa pamoja na jambo linalohusu maendeleo tukalisimamia kwa pamoja.
Mstahiki Meya wa manispaa ya Moshi,RAymond Mboya akiwa aameongozana na Madiwani wa Halmashauri hiyo kukagua shughuli za ukarabati unaoendelea katika kituo cha Afya cha Pasua mjini Moshi.
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi,Raymond Mboya akijaribu kuzungusha moja ya vitanda vilivyowekwa katika wodi ya wazazi katika kituo hicho.
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi ,Raymond Mboya akizungumza mara baada ya kutembelea kituo cha Afya cha Pasua kujionea shughuli za ukarabati wa kituo hicho zinavyoendelea.
Baadhi ya wanachama wa chama cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Demokrasia na maendeleo (Chadema) wakiwa katika kituo hicho kuunga mkono shughuli za maendeleo .
Diwani wa kata ya Bomambuzi ,Juma Raibu kilipo kituo hicho cha Afya akizungumza mara baada ya ukaguzi .
Moja ya jengo la kituo hicho likiwa katika hatua za mwisho kukamilika.
Shughuli za upakaji rangi ikiendelea kwa baadhi ya majengo katika kituo hicho.
Baadhi ya majengo mapya yaliyoongezwa katika kituo hicho cha Afya Pasua.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad