HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, February 4, 2019

KESI YA MALINZI NA WENZAKE YAPANGIWA HAKIMU MWINGINE

HAKIMU Mkazi wa Mahakama ya Hakimu  Mkazi Kisutu,  Maira Kasonde aliyepangwa kuendelea kusikiliza kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili  aliyekuwa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi na  wenzake Wanne ameomba kupewa muda wa kupitia jalada la kesi hiyo ili kuangalia ushahidi na vielelezo vilivyotolewa na upande wa mashtaka katika shauli hilo kabla ya kutoa maamuzi. 

Hakimu Maira ambaye amepangwa kusikiliza kesi hiyo baada ya hakimu aliyekuwa akisikiliza shauri hilo, Wilbard Mashauri kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania ametoa ombi hilo leo Februari 4, 2019 wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kutolewa maamuzi. 

Mapema wakili wa Serikali kutoka Takukuru, Leornard Swai amedai, kesi hiyo leo imekuja kwa ajili ya uamuzi na kueleza kuwa imepata hakimu mpya baada ya Mashauri kuteuliwa kuwa Jaji hivyo kutokana na hali hiyo washtakiwa wanapaswa kukiri kama wanataka waanze upya au waendelee walipoishia. 

Hakimu Kasonde amesema kuwa ni kweli kesi hiyo ilikuwa kwa Hakimu Mashauri ambaye kwa sasa ameteuliwa kuwa Jaji,  hivyo anahitaji kupata muda wa kupitia jalada, kusoma ushahidi pamoja na kuangalia vielelezo vilivyotolewa katika kesi hiyo ili awe katika nafasi nzuri ya kujua kitu gani anatakiwa kufanya.

"Ninahitaji nipate muda wa kupitia na kuangalia ushahidi kama unaeleweka na vielelezo vilivyotolewa pia hivyo kwa sasa sipo katika nafasi nzuri ya kuendelea kuisikiliza, " alisema. 

Kesi hiyo imeahirishwa hadi Februari 19, mwaka huu.  

Mbali na Malinzi, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Katibu Mkuu wa TFF, Mwesigwa  Selestine(46) na Mhasibu wa TFF,  Nsiande  Mwanga(27), Meneja wa  Ofisi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF),Miriam Zayumba na Karani wa TFF, Flora Rauya.

Washtakiwa hao Kwa pamoja  wanakabiliwa na mashtaka 30 katika  kesi ya jinai namba 213 ya mwaka 2017 yakiwamo ya kula njama, kughushi, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na utakatishaji wa fedha wa USD 173,335 na Sh 43,100,000.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad