HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, January 9, 2019

WAZIRI AWESO AMSWEKA RUMANDE MHANDISI WA MAJI SHINYANGA, AAGIZA WAHANDISI KUTEMBELEA MIRADI


Naibu Waziri wa Maji Juma Aweso ameliagiza jeshi la polisi mkoani Shinyanga kumkamata mhandisi wa maji Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Sylivester Mpemba  kushindwa kusimamia kikamilifu utekelezaji wa mradi wa maji uliogharimu serikali kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni moja.
Agizo hilo amelitoa leo Januari 8,2019 wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Mwakitolyo kwenye mkutano wa hadhara ambapo wananchi waliopewa nafasi ya kuuliza maswali walijikita na changamoto ya upatikanaji wa maji kutokana na mradi uliopo kushindwa kutoa maji. Hata hivyo majibu ya mhandisi wa maji Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Sylivester Mpemba yalishindwa kujitosheleza licha ya serikali kutoa fedha kiasi cha shilingi bilioni moja,milioni mia nne na sitini na mbili.
Kufuatia kukosekana kwa majibu kuhusu namna pesa hizo zilivyotumika,Aweso alieleza kusikitishwa na ucheleweshwaji wa mradi huo akidai kuna uzembe wa Mhandisi huo hivyo kumwagiza Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Jasinta Mboneko na jeshi la polisi kumkamata mhandisi huyo.
“Mradi wa maji Mwakitolyo gharama yake ni shilingi bilioni 1.482 mpaka sasa serikali ya imelipa kiasi cha bilioni 1.462, sisi tunaumia sana wakati mwingine huyu angekuwa daktari si angeshaua watu, mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ita polisi peleka ndani mtu huyu” ,alisema Aweso.
Waziri Aweso pia alimuagiza kaimu mhandisi wa maji mkoa wa Shinyanga Julieth Payovela kuandika barua ya kujitathmini katika utendaji kazi wake,na kuwaagiza wahandisi wa maji nchini kutembelea na kukagua miradi ya maji iliyopo kwenye maeneo yao na kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo ili kufikia azma ya kumtua mama ndoo kichwani.
Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Solwa Ahmed Salum alisema wakazi wa jimbo hilo bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali za miundombinu ya barabara, elimu, umeme na huduma za afya na kuiomba serikali kuwatazama wakazi wa jimbo hilo kwani wanajihisi kutengwa licha ya baadhi ya wataalamu kukwamisha juhudi za serikali kuwapatia wananchi wake huduma bora za kijamii.
“Jimbo la Solwa ni miongoni mwa majimbo nchini yanayokabiliwa na changamoto lukuki hasa katika sekta ya afya,elimu na miundombinu ya barabara, wananchi hawa hawana pa kukimbilia zaidi ya serikalini kutokana na mapato wanayoichangia serikali katika huduma za kimaendeleo” ,alisema Ahmed. ANGALIA PICHA ZA MATUKIO HAPA CHINI
Naibu Waziri wa Maji Juma Aweso  akizungumza na wakazi wa kata ya Mwakitolyo kwenye mkutano wa hadhara ili kusikiliza kero zinazowakabili - Picha zote na Malaki Philipo- Malunde1 blog
Mhandisi wa maji halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Sylivester Mpemba(kushoto) akihojiwa na Naibu Waziri wa Maji Juma Aweso (kulia) kuhusu kushindwa kusimamia mradi wa maji kata ya Mwakitolyo.
Naibu Waziri wa Maji Juma Aweso akizungumza na kuagiza Mhandisi wa maji halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Sylivester Mpemba akamatwe na polisi .
Polisi wakitekeleza agizo la kumshikilia na kumuweka chini ya ulinzi mhandisi wa maji halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Sylivester Mpemba.
Mhandisi wa maji halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Sylivester Mpemba akiwa chini ya ulinzi.
Wakazi wa kata ya Mwakitolyo wakifuatilia matukio yaliyokuwa yanaendelea.
Tenki la maji Mwakitolyo,mradi wa maji ambao umeigharimu serikali kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni moja na mradi haujawanufaisha wananchi.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akizungumza na wakazi wa kata ya Mwakitolyo.
Mbunge wa jimbo la Solwa Ahmed Salum akizungumza kwenye mkutano wa hadhara wakati wa ziara ya Naibu waziri wa maji Mwakitolyo.
Wakazi wa Mwakitolyo wakiwa kwenye mkutano.
Awali Sada Khamis mkazi wa kijiji cha Mwakitolyo akieleza kero ya maji katika eneo hilo mbele ya Naibu waziri wa maji Juma Aweso.
Mwenyekiti wa kijiji cha Mwakitolyo Nuhu Nshomi akieleza changamoto za elimu,maji na umeme wakati wa mkutano.  Picha zote na Malaki Philipo- Malunde1 blog

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad