* Wanafunzi waiomba serikali kutambua na kuunga mkono jitihada za FEMINA nchini kote.
Na Leandra Gabriel, Blogu ya Jamii
SHIRIKA lisilo la kiserikali la FEMINA linaloshughulika na masuala ya vijana hasa kwa kutoa elimu ya afya ya uzazi na ujinsia pamoja na shughuli ya ujasiriamali limetimiza miaka 20 tangu kuanzishwa kwake kwa kuwakutanisha vijana kutoka klabu zote nchini na kutoa elimu kuhusiana masuala ya afya na fursa za kiuchumi.
Akizungumza katika maadhimisho hayo Meneja wa idara ya uhamasishaji jamii kutoka FEMINA Nashivai Mollel amesema kuwa licha ya kusherekea miaka 20 ya FEMINA wamewakutanisha vijana hao kwa lengo la kutoa mafunzo kama vile elimu ya afya ya uzazi na fursa za kijasiriamali bila kutegemea kuajiriwa pekee.
Amesema kuwa malengo ya mkutano huo ni kuleta mabadiliko chanya pamoja na kutatua changamoto hizo kwa vijana kwa kushirikiana na walimu walezi wa klabu hizo.
Pia ameishukuru Serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wa Rais Dkt. John Magufuli pamoja na viongozi mbalimbali akiwemo Waziri wa afya, maendeleo ya jamii, wazee, jinsia na watoto Ummy Mwalimu kwa jitihada wanazoonesha katika kuwasaidia vijana. Na amehaidi kuwa wataendelea kuwasaidia vijana katika nyanja mbalimbali kwa kuwasaidia vijana wengi zaidi.
Kuhusiana na mchango wa klabu za FEMA katika kuchangia ufaulu wa wanafunzi mashuleni, mlezi wa klabu ya Mnyuzi, Charles Mayombo amesema kuwa klabu hizo zimekuwa chachu kubwa kwa wanafunzi katika kufanya vizuri katika masomo yao, hiyo ikiwa ni pamoja na sifa mojawapo ya kuwa mwanaklabu ya FEMA lazima mwanafunzi afanye vizuri katika masomo yake na hiyo imedhihirika kwa matokeo ya kidato cha pili yaliyotoka hivi karibuni kwa walezi wote wa klabu za FEMA kuleta mrejesho mzuri kuhusiana na matokeo hayo ambapo wanafunzi wengi walionekana kufanya vizuri.
Baadhi ya wanafunzi walioshiriki mkutano huo wameeleza kuwa klabu hizo zinasaidia sana kwa kuwa wanapata elimu ya kujitambua, nidhamu pamoja na kupambana na changamoto wanazopitia katika masuala ya ukuaji na wameiomba Serikali kuzitambua na kuunga mkono jitihada zinazofanywa na FEMINA.
Meneja
idara ya uhamasishaji jamii Nashivai Mollel akizungumza na wanafunzi
kutoka katika Mikoa mbalimbali nchini katika mkutano huo uliowakutanisha
katika kusherekea miaka 20 tangu kuanzishwa kwa shirika hilo, leo
jijini Dar es Salaam.
Walimu
walezi wa klabu za FEMA, (Walioketi) wakiwa katika picha ya pamoja na
viongozi wa FEMINA mara baada ya kukabidhiwa zawadi zao kwa kuonesha
mchango chanya katika klabu hizo mashuleni.
Mkurugenzi
wa Habari wa FEMINA Amabilis Batamula (katikati) akizungumza katika
mkutano huo wa kuadhimisha miaka 20 ya FEMINA uliofanyika leo jijini Dar
es salaam, kushoto ni Meneja idara ya uhamasishaji jamii kutoka FEMINA,
Nashivai Mollel.
Walimu
kutoka Mikoa mbalimbali nchini wakiwa na vyeti walivyotunukiwa katika
mkutano wa kuadhimisha miaka 20 ya FEMINA uliofanyika leo jijini Dar es
Salaam na hiyo ni kutokana na kuonesha juhudi za ziada katika
kutekeleza majukumu ya kuwasaidia vijana.
Meneja
idara ya uhamasishaji Jamii, Nashivai Mollel akizungumza na waandishi
wa habari kuhusiana na maadhimisho ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa
shirika hilo leo jijini Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment