HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, December 19, 2018

WAJASIRIAMALI 25,000 MKOANI TABORA WAANZA KUGAWIWA VITAMBULISHO VYA RAIS MAGUFULI

Na Tiganya Vincent, Tabora
WAJASIRIAMALI wadogo wadogo mkoani Tabora wameonywa kutotumia vitambulisho walivyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuuzia biashara za wafanyabiashara wakubwa na hivyo kuwa chanzo cha ukwepeji kodi.

Onyo hilo limetolewa leo na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri wakati akigawa vitambulisho 25,000 kwa Wakuu wa Wilaya saba za Mkoa huo na viongozi watatu wa Wajasiriamali wa Manispaa ya Tabora ikiwa ni uzinduzi wa zoezi hilo mkoani humo.

Alisema vitambulisho vilivyotolewa na Rais ni kwa ajili ya Wajasiriamali wadogo wadogo na sio vinginevyo na ambao ni wale biashara zao kwa siku zote 365 za mwaka mapato yao hayazidi shilingi  milioni nne.

Mwanri alisema ni kosa kuazimisha kitambulisho au kubeba bidhaa za wafanyabiashara wakubwa  na kuongeza kuwa atakayebainika atakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya Sheria ili achukuliwe hatua.

Aidha alisema Mkoa huo ulipatiwa vitambulisho 25,000 vilivyotolewa na Rais Magufuli hivi karibuni ambapo vimegawanywa kwa Halmashauri zote nane za Mkoa wa Tabora na kila moja imepata vitambulisho 3125.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa alizionya Mamlaka za Serikali za Mitaa Mkoani humo kuanzia sasa kutowabughuzi wafanyabiashara wadogo wadogo badala yake wanapaswa kuwashika mkono kama alivyofanya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwakumbuka rasmi kama watu muhimu katika mchango wa kuelekea uchumi wa kati.

Kwa upande wa Meneja wa Mkoa wa Tabora wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)  Thomas Masese alisema anayepaswa kupata kitambulisho hicho ni yule ambaye mwenye mauzo ghafi yasiyozidi milioni 4 kwa mwaka.

Alisema wanaotakiwa ni wafanyabiashara wasio katika sekta isiyo kama vile mama na baba lishe na machinga na atatakiwa kulipia kitambulisho shilingi 20,000/baada ya kujaza fomu maalumu inayopatikana kwa Mkuu wa Mkoa au Wilaya.

Aidha Meneja huyo wa Mkoa alisema kuwa kuanzia sasa vitambulisho vilivyokuwa vikitolewa na TRA kwa ajili ya Wajasiriamali vimesitisha na vitakavyoanza kutumika ni vile ambavyo vimetolewa na Rais Magifuli.

Akisomali risala ya Katibu Msaidizi wa Wajasiriamali wadogo wadogo  wa Manispaa ya  Tabora Ashura Rashid alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli kwa kuwakumbuka na kuwaondolea manyanyaso ambayo walikuwa wakipata wakati wa kufanya shughuli zao  na pia kwa  kuwatambua rasmi.

Alisema watavitumia vitambulisho hivyo kwa madhumuni ya kuanzishwa kwake na sio kwa kuvunja Sheria mbalimbali ili hatiamaye waweze kukuza mitaji yao na siku moja waje wawe walipa kodi wakubwa.

Aidha Ashura aliiomba Serikali kuwatengea maeneo ya kufanyia biashara zao na pia kuomba vitambulisho hivyo kupelekwa hadi ngazi za Vijiji ili kuwaondolea usumbufu wajasiriamali kufuatilia katika ngazi za Wilaya.
 Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri akiwahutubia Wajasiriamali mkoani humo kabla ya kuanza maandamano maalumu waliyoandaa ya kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwatambua rasmi ya kuwapatia vitambulisho.
 Baadhi ya Wajasiriamali wa Manispaa ya Tabora wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Tabora (hayupo katika picha)  kabla ya kuanza maandamano maalumu waliyoandaa ya kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwatambua rasmi ya kuwapatia vitambulisho.
 Maandamano maalumu ya kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwatambua rasmi ya kuwapatia vitambulisho yaliyoandaliwa na  Wajasiriamali wa Manispaa ya Tabora
 Maandamano maalumu ya kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwatambua rasmi ya kuwapatia vitambulisho yaliyoandaliwa na  Wajasiriamali wa Manispaa ya Tabora yakiingia kwenye viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora tayari kwa kugawiwa vitambulisho.
  Baadhi ya Wajasiriamali wa Manispaa ya Tabora na viongozi mbalimbali wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Tabora (hayupo katika picha)  kabla ya kuanza kugawa vitambulisho vilivyotolewa na  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa ajili ya Wajasiriamali.
 Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri akimvisha kitambulisho Katibu Msaidizi wa Wajasiriamali Manispaa ya Tabora Ashura Rashid baada ya aaandamano maalumu ya kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuwatambua rasmi ya kuwapatia vitambulisho yaliyoandaliwa na  Wajasiriamali wa Manispaa ya Tabora.
  Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri (wenye Tshirt ya Njano) akimkabidhi vitambulisho 6250 Mkuu wa Wilaya ya Nzega Godfrey Ngupula (kushoto) kwa ajili kwenda kuwagawia Wajasiriamali wilayani kwake. Picha na Tiganya Vincent

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad