HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, November 12, 2018

WANAFUNZI 600 S/M VIKAWE KATA YA PANGANI, KIBAHA MJINI WASOMEA KATIKA MADARASA MANNE


NA MWAMVUA MWINYI,KIBAHA

SHULE ya msingi Vikawe ,kata ya Pangani ,Mjini Kibaha ,Mkoani Pwani ina upungufu wa vyumba vya madarasa hali inayosababisha ,wanafunzi 600 kusomea kwenye vyumba vinne vinavyotumika shuleni hapo .

Aidha wakazi wa Vikawe ,wanakabiliwa na adha ya ukosefu wa maji safi na salama hali inayosababisha kutumia maji ya visima ambayo sio salama kwao.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika mkutano wa hadhara wa wakazi wa Vikawe Bondeni, Vikawe Shule na Mtaa wa Miwale, ulioitishwa na mbunge wa jimbo la Kibaha Mjini ,Silvestry Koka , mkazi Amina Seif alisikitishwa kuona baadhi ya vyumba vya madarasa vina majani ya miba badala ya wanafunzi.Akizungumzia suala la ukosefu wa maji , Majawa Mtwana alisema ,hawapaswi kuwa na tatizo la maji kwakuwa bomba limepita kwenye eneo lao .Alisema wangefaidika na mradi huo ulioanzia Ruvu Chini -Vikawe Shuleni hadi Miwale ."Tunaomba utusaidie mbunge ,hatupaswi kuishi mjini wakati tunashida ya maji ,ndoa za watu zipo matatani kwa kukosa maji ,tunaoga maji ya visimani,tunataka ushughulikie suala hili ili tuondokane na kero hii" alielezea.

Kaimu afisa elimu msingi ,Ramadhani Lawoga alisema,shule ya msingi Vikawe ina jumla ya vyumba vya madarasa saba,kati ya vyumba hivyo viwili na ofisi ya mwalimu ni jengo la zamani ambalo limechakaa.Hata hivyo alisema ,nalo jengo jipya lililojengwa shuleni hapo nalo ni bovu .Lawoga alieleza, kutokana na hali hiyo ,vyumba vitatu kati ya saba vilivyopo ni vibovu na hivyo vinatakiwa kujengwa upya ,ambapo wanatarajia kuanza kujenga vyumba viwili kwa bajeti ya mwaka 2018/2019. Akijibu juu ya upungufu wa madarasa ,aliahidi kwenda kushauriana na mkurugenzi wa halmashauri ya Mji wa Kibaha Jennifer Omolo ili kuangalia namna ya kukarabati baadhi ya madarasa .

Kuhusu changamoto ya maji ,halmashauri ya mji huo imekiri kuwepo deni la bili walilokuwa wakidaiwa na DAWASA ya sh.milioni 4.8 ambapo imeshalipa kiasi cha sh.milioni 3.4 na imebakia deni la milioni 1.4 .Kutokana na ubovu pamoja na wataalamu kutofanya kazi ya usambazaji ipasavyo ya mradi huo ,Koka alisema kinachofuata ni hatua ya uchunguzi na mradi kurudishwa chini ya DAWASA ili kuondoa tatizo hilo .

Mbunge huyo alilazimika kuunda kamati ya watu sita akiwemo injinia wa DAWASA Kibaha, Injinia wa maji Halmashauri ya Mji Kibaha, Diwani wa Pangani ,katibu wa nbunge na wananchi wawili kwa ajili ya kwenda Bagamoyo ili kufuatilia jambo hilo na kutoa mrejesho ndani ya wiki moja .

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad