HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, October 9, 2018

WAKULIMA WA MBAAZI NA CHOROKO KUNEEMEKA NA SOKO LA UHAKIKA LA MAZAO HAYO

Na Mwandishi wetu, Kondoa
WAKULIMA wa Mbaazi na Choroko hapa nchini wanatarajia kuondokana na adha ya mazao yao kukosa soko baada ya wawekezaji kadhaa kujitokeza kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya kuchakata mazao hayo katika mikoa ya Arusha, Dodoma, Dar es Salaam na Morogoro.

Kauli hiyo ya matumaini kwa wakulima hao imetolewa wilayani Kondoa mkoani Dodoma na Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. Omari Mgumba, wakati akitoa salaam kwenye Mkutano Mkuu Maalumu wa Chama cha Mapinduzi CCM, Jimbo la Kondoa, ambapo Mbunge wa Jimbo hilo, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, aliwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya chama hicho kwa kipindi cha miaka 3 ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.

" Kilimo kinategemewa na zaidi ya asilimia 65 ya watanzania, lakini zao la mbaazi limekuwa na matatizo ya soko ndio maana Serikali imeamua kuchukua hatua kwa kuwahamasisha wawekezaji kujenga viwanda vya kusindika mazao hayo hapa hapa nchini, jambo ambalo limeanza kutekelezwa" alisema Mhe. Mgumba

Alisema hivi sasa viwanda vitatu vya  kuchakata mbaazi vinajengwa mkoani Arusha, Dar es Salaam na Morogoro katika eneo la Mtego wa Simba, huku kiwanda kimoja na kusindika choroko kikijengwa mkoani Dodoma.

Alisema kuwa lengo la hatua hizo ni kujibu kero ya muda mrefu ya wakulima wa mazao hayo katika mikoa ya Manyara, Arusha, Dodoma na maeneo mengine yanayolimwa mazao hayo  kukosa soko la uhakika kwa kuongeza thamani ya mazao hayo hapa hapa nchini.

"Ukiongeza thamani ya hizi mbaazi unapanua soko katika dunia badala ya kutegemea soko moja tu la nchini India, ambapo sasa mbaazi zitauzwa nchi mbalimbali zikiwemo nchi za kiarabu, Ulaya na Marekani" Alisisitiza Mgumba.

Awali, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango na Mbunge wa Jimbo la Kondoa, Dkt. Ashatu Kijaji alimweleza Naibu Waziri huyo wa Kilimo kwamba Wilaya ya Kondoa ina wakulima wengi ambao wanahitaji kuboreshewa mazingira yao ya kilimo ili waweze kujikwamua kiuchumi

"Watu wanasema Kondoa ni vijijini kwa asilimia 100 lakini kwa kasi tunayokwenda nayo, baada ya miaka 5 Jimbo hili litakuwa miji mitupu katika kata zote 21 na kitakacho tuvusha kwenda kwenye miji hiyo ni kilimo" alisisitiza Dkt. Kijaji

Mbaazi imekosa soko katika miaka mitatu mfululizo ambapo bei hiyo ilishuka kutoka  shilingi 2,500 na 3,000 kwa kilo mwaka 2015 na kufikia bei ya shilingi 250 hadi 300 kwa kilo jambo linalowakatisha tamaa wakulima huku wafanyabiashara na baadhi ya wakulima wakiwa na shehena ya zao hilo kwenye maghala wakisubiri kupanda kwa bei.
Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. Omari Mgumba, akitoa salaam kwenye Mkutano Mkuu Maalumu wa Chama cha Mapinduzi CCM, Jimbo la Kondoa, ambapo Mbunge wa Jimbo hilo, ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, aliwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya chama hicho kwa kipindi cha miaka 3 ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano, katika Jimbo la Kondoa, uliofanyika katika Kata ya Pahi, Wilayani Kondoa.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad