HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 27, 2018

SERIKALI YAWATAKA WATAFITI KUFANYA TAFITI ZENYE TIJA NA KUBORESHA SERA YA MAENDELEO

Na Cathbert Kajuna - Kajunason/MMG.
Serikali imewataka watafiti kote nchini kufanya tafiti katika maeneo ya vipaumbele vya serikali, badala ya kufuata matakwa ya wafadhili.

Amesema kufanya hivyo kutasaidia kuboresha sera na mipango ya maendeleo itakayowezesha kufikia malengo katika sekta mbali mbali ikiwemo afya na kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati ifikapo 2025

Akizungumza katika Kongamano la kuwasilisha tafiti za dawa za kulevya lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS), Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile amewataka watafiti kufanya tafiti zitakazozingatia takwimu sahihi ambazo zinachangia katika kuboresha sera na programu za afya.

"Natoa rai msifanye utafiti kwa sababu tu kuwa wafadhili wanatupatia fedha na msifanye tafiti na mkaridhika kwa vile tafiti zenu zimechapishwa kwenye majarida, bali mje na zile zitakazofanya mabadiliko ya sera mbali mbali hususani kuboresha upande wa afya," amesema.

Nae Makamu Mwenyekiti wa Chuo cha MUHAS Prof. Andrew Pembe amesema matokeo ya utafiti yanaonyesha tatizo la matumizi ya madawa ya kulevya bado ni kubwa na waathirika wa madawa ya kulevya hawawezi kushiriki katika shughuli za kuzalisha.

Ameongeza kuwa watumiaji wengi wa madawa ya kulevya wanajishughulisha katika vitendo vya uharifu, na wanauwezo mkubwa wa kupata magonjwa mbali mbali likiwemo UKIMWI.

Upande wake Naibu Makamu Mkuu wa Chuo cha MUHAS  anayeshughulikia Taaluma, Tafiti na Ushauri Prof. Appolinary Kamuhabwa amesema kuwa chuo kimejipanga kutoa taarifa inayotokana na matokeo ya tafiti ambayo itakuwa imeandikwa kwa lugha nyepesi na kuwapelekea wizara ya afya ambao badae wanaweza kuangalia ni mambo gani yanaweza kuwasaidia katika kuborsha sekta ya afya.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Faustine Ndugulile (ambaye alikuwa mgeni rasmi) akizungumza  katika Kongamano la kuwasilisha tafiti za dawa za kulevya lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS) na kufanyika jijini Dar es Salaam. Picha zote na Cathbert Kajuna- Kajunason/MMG.
Wageni waalikwa na  Wanafunzi wa MUHAS waliohudhulia kongamano hilo.
 Makamu Mwenyekiti wa Chuo cha MUHAS Prof. Andrew Pembe akitoa maneno ya kutambulisha Kongamano la kuwasilisha tafiti za dawa za kulevya lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi (MUHAS) na kufanyika jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad