HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Thursday, September 27, 2018

Pinda ajitosa kuinua lishe Kagera

Na Mwandishi Wetu, Pugu
WAZIRI Mkuu mstaafu, Mizengo Peter Pinda, amesema asasi zisizo za kiserikali zitachochea vikubwa maendeleo ya uchumi na ustawi wa jamii nchini endapo zitahamasisha ushiriki wa vijana na wanawake kwenye sekta za kilimo, uvuvi na biashara.

Akizungumza na ujumbe wa Agri-Thamani Foundation ya Mkoa wa Kagera uliomtembelea nyumbani kwake Pugu, Dar es Salaam ili kumshukuru kwa kuwa mlezi wa asasi hiyo, Waziri Mkuu mstaafu ameeleza thamani na nguvu asasi zizizo za kiserikali duniani kote katika kusaidiana na serikali kuneemesha maendeleo ya wananchi na akaahidi kutumia asasi hiyo kuinua lishe katika Mkoa wa Kagera.

“Mimi pia ni mkulima na nina uzoefu wa muda mrefu katika kilimo. Kwa sababu hii naamini nitaweza kuchangia vyema katika kuiongoza taasisi hii kufikia malengo yake na kwa kuunga mkono azma ya serikali ya awamu ya tano kujenga uchumi wa kati na viwanda…Ni matumaini yangu ni kwamba tutashirikiana kuinua lishe Mkoa wa Kagera. La muhimu ni ushirikiano na uaminifu wa hali ya juu, ameasa Bw Pinda.

Ametumia fursa hiyo kuwaeleza Watanzania kwamba ili asasi zisizo za kiserikali zifikie malengo yake, ni lazima zihamasishe ushiriki wa vijana na wanawake katika sekta za kilimo, uvuvi na biashara na kufafanua kwamba, ni muhimu kuthaminisha mazao ya wakulima ili waweze kunufaika. Uzalishaji wa mazao ukiongezeka, ameeleza, uhitaji wa viwanda kuchakata mazao hayo yataongezeka pia.

Kiongozi huyo ameeleza kuwa tatizo la unyafuzi limesababishwa na kukosekana lishe bora, kwani lishe bora ni muhimu kwa afya njema na kumwezesha mtu kujikinga na magonjwa mbalimbali na kuahidi kwamba yeye binafsi atahakikisha asasisi hiyo inashirikiana na wizara ya afya na taasisi nyingine za afya ndani na nje ya nchi ili elimu ya lishe iwafikike walengwa kwa usahihi vijana na wanawake wa Mkoa wa Kagera kutambua umuhimu wa lishe na afya bora katika juhudi za kuleta maendeleo.

Naye Mwenyekiti na mwanzilishi Bi. Neema Lugangira ambaye ni mwanzilishi na mwenyekiti wa taasisi hiyo amesema sehemu pekee ambayo lishe bora inaweza kupatikana Ni kupitia Kilimo, ufugaji na uvuvi. Hivyo kuwaomba wananchi wa Kagera hasa vijana na wanawake wa Kagera ambao ndio wanufaika wakubwa wa taasisi hii kutoa ushirikiano wa kutosha na kujituma ili kujiendeleza kiuchumi na kutumia mazao hayo katika kujenga afya zao.

“Ili taifa liwe endelevu linahitaji kuwa na wananchi wenye afya nzuri, kimwili na kiakili pamoja na nguvu ya kufanya kazi. Nitoe wito kwa vijana na wanawake wa Kagera kutumia fursa hii kwa kushirikiana na taasisi yetu katika kutokomeza tatizo la utapia mlo na magonjwa mengine ya lishe mkoani Kagera,” aliongeza Bi.Neema Lugangira

Alisema Tanzania inategemea wananchi wake kutumia fursa zilizopo kuendelea. Na katika kutimiza hili, vijana wanategemewa kwa kiasi kikubwa. Na kwasababu kilimo ni uti wa mgongo wa taifa hawana budi kuwekeza juhudi zao katika kilimo.

“Ni matumaini yangu wananchi wa Kagera wataweza kuondokana na umaskini, kuimarisha hali ya lishe na ushiriki wenu katika mnyororo wa thamani wa kilimo, mifugo na uvuvi kuimarika.” Bi Lugangira alisisitiza.
WAZIRI Mkuu mstaafu Mizengo Peter Pinda(kushot) akizungumza na Mwenyekiti wa Asasi isiyo ya kiserikali Agri Thamani Foundation kutoka Kagera, Bi. Neema Lugangira (kulia). Mzee panda ni mlezi wa asasi hiyo alielezea umuhimu wa kutoa elimu sambamba na uboreshaji wa upatikaji wa lishe bora pamoja na kuwaunganisha vijana na wanawake katika sekta zingine za kimkakati hapa nchini ili kutokomeza unyafuzi na umaskini.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad