HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, September 24, 2018

MGALU AMETHIBITISHA GATI LA NYAMISATI HALIHAMISHWI,LINATARAJIWA KUGHARIMU BIL.14

  Naibu waziri wa nishati, Subira Mgalu akizungumza na wananchi wa Nyamisati wilayani Kibiti.
Naibu waziri wa nishati, Subira Mgalu (wa pili kutoka kulia)  akimuelekeza jambo meneja wa ujenzi wa mradi wa gati la Nyamisati kutoka mamlaka ya usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Mhandisi Erick Madinda (kushoto) kabla ya waziri huyo kuzungumza na wananchi wa Nyamisati wilayani Kibiti.

NA MWAMVUA MWINYI, KIBITI 
NAIBU Waziri wa Nishati ,Subira Mgalu amethibitisha kuwa serikali inaendelea kujenga gati la Nyamisati, Kibiti, mkoani Pwani na haina mpango wa kulihamisha ambapo linatarajiwa kugharimu sh. bilioni 14 hadi kukamilika kwake. 
Amewatoa shaka hiyo wananchi ambao walikuwa wakidai ujio wa ujenzi wa mradi mkubwa wa uzalishaji umeme katika maporomoko ya mto Rufiji, Hydro Power (Stigilers Gorge )unaweza kusababisha athari za ujenzi wa gati hilo kwenda kisiwa cha Mafia. 

Subira aliyasema hayo, wakati akizungumza na wananchi wa Nyamisati,  mara baada ya kutembelea ujenzi wa gati hilo .

Alisema  mradi wa ujenzi wa gati hilo umefanyiwa utafiti wa kina na kubaini  hautakuwa na athari zozote za kimazingira .

Subira alieleza, baadhi ya watu wanadai kuwa eneo hilo la gati kina cha maji kitapungua suala ambalo sio la kweli .

"Wataalamu wa mradi wa Hydro Power na gati walikaa kubadilishana uzoefu, na ripoti yao inaonyesha hakutakuwa  na athari za kimazingira "

" Wataalamu walifanya upembuzi yakinifu na hakujaonyesha kuwa kutakuwa na athari ya kimazingira," alisisitiza Subira .

Alisema ,miradi yote hiyo ina faida kubwa kwa wananchi na Taifa na serikali imetumia wataalamu kufanya utafiti ili kujiridhisha .

Hata hivyo, Subira alieleza serikali imedhamiria kuufungua ukanda wa Kisiwa cha Delta kwa kupeleka nishati ya umeme ambapo inatarajia kuanza na umeme wa jua. 

Pia imetengwa kiasi cha sh. bilioni. Nne kwa ajili ya ujenzi wa daraja Mbwera na mil. 400 imetengwa kwa kujenga kituo cha afya Mbwera.  

Nae meneja wa ujenzi wa mradi wa gati la Nyamisati kutoka mamlaka ya usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), Mhandisi Erick Madinda alisema maji hayawezi kupungua mara litakapojengwa bwawa kubwa la uzalishaji umeme la Stigilers Gorge.

Alieleza,  eneo hilo ni sehemu ambapo kuna mwingiliano wa mto na bahari hivyo maji hayawezi kupungua na kuleta athari kwenye gati.

Mbunge wa Kibiti Ally Ungando, aliomba kasi ya ujenzi wa gati iongezeke kwakuwa imekuwa ndogo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad