Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. January
Makamba amewakumbusha watendaji wa Wilaya ya Serengeti wajibu wao wa kipekee
wa ulinzi katika hifadhi ya mbuga ya Serengeti kwakuwa Wilaya yao imebeba jina
linalojulikana duniani kote ikiwa ni pamoja na eneo maalumu la wanyama aina ya
Nyumbu ambao huvuka kwenda upande wa pili na kuwa miongoni mwa vivutio vikubwa
vya utalii.
Waziri Makamba ameyasema hayo leo Wilayani Serengeti mara baada ya kufanya
ziara ya kikazi Wilayani hapo kujionea uzingatiaji wa Sheria ya Mazingira na
kutembelea eneo la mto Mara eneo ambalo ni muhimu sana ki-ikolojia.
Katika kikao na viongozi wa Wilaya hiyo, Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya
Serengeti Bw. Wiliam Mwakilema aliainisha kuwa mtiririko wa maji katika Mto Mara
kutoka chanzo chake kikuu katika Milima ya Mau nchini Kenya kimepungua kutokana
na shughuli za kibinadamu na matumizi mengine yasiyoendelevu jambo linalohatarisha
kupungua kwa mtiririko wa maji katika Mto Mara kwa kipindi kirefu, eneo ambalo ni
kivutio pekee cha wanyama wanaohama dunia.
Katika kutatua tatizo hilo Waziri Makamba amesema kuwa masuala ya mazingira ni
mtambuka hivyo Ofisi yake yenye dhamana na kusimamia hifadhi ya Mazingira nchini
itafanya ziara ya kikazi nchini Kenya kwa lengo la kujadiliana na kupata ufumbuzi wa
haraka juu ya jambo hilo.
“Sisi na wenzetu wa Kenya tumeingia mkataba mwaka 2013 wa matumizi sahihi ya
rasilimali katika Mto Mara na kutunza ikolojia yake, kwa kushirikiana na Mawaziri
wenzangu wa Maji na Maliasili na Utalii, tutafanya ziara nchini Kenya ili kwapamoja
tupate ufumbuzi wa jambo hili ikiwa ni pamoja na Ziwa Chala, Ziwa Jipe na Ziwa
Natroni ambayo yote yako pande mbili yaani Tanzania na Kenya.”
Waziri Makamba amesema Serikali itahakikisha maslahi ya Nchi yanalindwa kwa njia
za ki-diplomasia na kuhakikisha Mto Mara unatiririsha maji kipindi chote cha mwaka.
Waziri Makamba amehitisha ziara yake Mkoani Mara na amewasili Mkoani Arusha
ambapo atakuwa na vikao wa wadau wa hoteli mbalimbali na kambi za uwindaji kwa
lengo la kuweka mikakati ya kuhifadhi mazingira maeneo ya mbugani.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira January Makamba
akiwa amesimama pemebezoni mwa Mto Mara eneo la ‘Kogatendo’ na kupata maelezo
kutoka kwa Mhifadhi Mkuu wa Serengeti Bw. William Mwakilema juu ya kupungua kwa
maji katika Mto huo. Waziri Makamba ameahidi kuipatia ufumbuzi changamoto hiyo
mapema iwezekanavyo.
Bw. William Mwakilema (kushoto) akifafanua jambo kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya
Makamu wa Rais Muungano na Mazingira January Makamba mara baada ya
kutembelea Mto Mara eneo maalumu ambalo wanyama aina ya nyumbu huvuka kwa
makundi na kuwa kivutio kikubwa cha utalii.
Eneo la Kogatendo katika Mto Mara ni miongoni mwa maeneo ambayo wanyama aina
ya nyumbu huvuka kwa makundi na kuwa kivutio cha utalii. Waziri mwenye dhamana ya
usimamizi wa Mazingira January Makamba ametembelea eneo hilo ili kuhakikisha
hatua zinachukuliwa kurejesha ikolojia ya mto huo katika hali ya awali.
No comments:
Post a Comment