HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Friday, August 3, 2018

Waziri wa Madini Angellah Kairuki (katikati) akipita katika maeneo mbalimbali ya kiwanda cha God Mwanga Gems Ltd kuona namna shughuli mbalimbali za uchakataji wa madini ya Kinywe zinavyofanyika.

Na Asteria Muhozya, Simanjiro

Waziri wa Madini Angellah Kairuki amesema anaona fahari kutokana na uwekezaji wa Kiwanda cha Kuchakata madini ya Kinywe (Graphite) uliofanywa na Kampuni ya wazawa ya GOD Mwanga Gems Ltd iliyopo Kata ya Endiamtu, Wilayani Simanjiro Mkoa wa Manyara. Waziri Kairuki ameyasema hayo leo tarehe 2 Agosti, alipotembelea kiwanda hicho kwa lengo la kujionea shughuli zinazofanywa na kiwandani hapo.

Amesema Serikali imekuwa ikihamasisha waombaji wa leseni za madini kuwekeza katika maeneo mbalimbali hivyo, jambo lililofanywa na kiwanda hicho ikiwemo malengo ya kiwanda husika kufungua viwanda vingine katika mikoa ya Tanga na Manyara ni jambo la kujivunia na fahari kwa Tanzania.

“Nimefurahishwa sana namna kampuni hii inavyofanya kazi. Serikali kupitia wizara yangu imekuwa ikihamasisha uwekezaji. Tuko tayari kuwasimamia na kuwasaidia katika hili. Tunataka kutengeneza ajira zaidi, kukuza uchumi kupitia madini lakini pia serikali kupata kodi,” amesisitiza Kairuki. Akijibu ombi la kampuni hiyo kupata kibali cha kuuza madini hayo nje, Waziri Kairuki ameahidi kampuni hiyo kuwa mara baada ya taratibu za utoaji vibali kukamilika Wizara kupitia Tume ya Madini itatoa kibali kwa kampuni husika iendelee na taratibu zake za kuuzwa nje ya nchi madini hayo.
Waziri wa Madini Angellah Kairuki (katikati) akitembelea maeneo mbalimbali katika kiwanda cha Kuchakata Madini ya Graphite cha GodMwanga Gems Ltd. Wa kwanza kulia ni Mmiliki wa kiwanda hicho Godlisten Mwanga na wa kwanza kuli kwa waziri ni Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro, Tumaini Magesa.

Kufuatia hali hiyo, Waziri Kairuki amewataka wenye leseni za madini kutozitumia leseni hizo kuziweka rehani kwa kuwa Sheria ya Madini inakataza jambo hilo badalayake zinatakiwa kutumiwa katika malengo yaliyokusudiwa.

“Wapo baadhi ya wawekezaji wamepewa leseni lakini hawajafanya chochote wengine wanaweka rehani leseni hizi. Nafurahi kuona mzawa mwenzetu amefanya jambo kubwa kama hili, leo nimejionea uhalisia katika jambo hili,” amesema Waziri Kairuki.

Pia, Waziri Kairuki ameishauri kampuni husika kuendelea kuitumia Maabara ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti Tanzania (GST) kwa ajili ya shughuli za utafiti na pia kuwatumia wahitimu wa Chuo Cha Madini Dodoma (MRI) katika suala la ajira. Katika hatua nyingine, Waziri Kairuki amesema Wizara imewachukulia hatua watumishi 40 kutokana na kwenda kinyume na maadili ya utumishi wa umma katika suala zima la usimamizi katika sekta husika.

Mmiliki wa kampuni ya God Mwanga Gems Ltd.Godlisten (kulia) Mwanga akimwonesha Waziri wa Madini Angellah Kairuki madini ya Grahite ambayo tayari yamechakatwa. 

“Wapo tuliowahamisha vituo vya kazi, wengine tumewasimamisha. Tunachotaka ni kuendana na kasi na huku wakizingatia maadili ya utumishi,” amesema Waziri Kairuki. Aidha, amesisitiza suala la wawekezaji kuendelea kutoa taarifa za uzalishaji ili serikali iweze kupata kodi zake huku akisisitiza suala la ulipaji kodi kwa serikali na wenye leseni zao kuzitumia na kuzalisha kwa viwango vinavyohitajika.

Kwa upande, Meneja wa Kiwanda hicho Henry Mbando ameiomba serikali kukisaidia kiwanda hicho kupata kibali kwa ajili ya kuuza madini hayo nje ya nchi ambayo yana masoko katika nchi za Marekani, Kanada, China na ulaya.

Ameongeza kuwa, madini hayo yanatumika kutengeneza bidhaa mbalimbali za viwandani vikiwemo vipuri vya magari, betri za magari na mitambo mengine. Ameongeza kuwa, soko la madini hayo ni katika nchi za Akizungumzia idadi ya wafanyakazi waliopo kiwandani hapo amesema kiwanda kina jumla ya watumishi 80 huku waanawake wakiwa 2 na wanaume 78.

Naye, Mmiliki wa kampuni hiyo, Godlisten Mwanga ameishukuru Serikali kwa msamaha wa kodi katika baadhi ya mitambo aliyoinunu kwa ajili ya kiwanda hicho na pia kumshukuru waziri Kairuki kwa kuona umuhimu wa kutembelea kiwanda husika. Amesema kiwanda hicho kimezalisha tani zaidi ya 2,000 na zilizotayari kwa ajili ya kuuzwa ni tani 200.

Akizungumzia suala la kibali kwa kampuni husika Kamishna wa Madini Mhandisi David Mlabwa amesema kuwa, awali kampuni hiyo ilikuwa haijakidhi vigezo vya kupata kibali lakini baada ya kukidhi viwango hivyo itapatiwa kibali.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad