HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, August 14, 2018

SERIKALI YAKABIDHI BOTI YA DORIA NA KITUO CHA POLISI WILAYANI CHATO

 Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni (kulia), akiwaongoza viongozi wengine kutembelea eneo la mwambao wa Ziwa Victoria  baada ya kuikabidhi boti hiyo ya doria kwa Jeshi la Polisi, kutoka kushoto  ni Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Daniel Shilla, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Gabriel na Diwani wa Chato, Richard Bagolele . Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
 Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Daniel Shilla akimshukuru Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni baada ya kumkabidhi Kituo cha Polisi kinachohamishika wilayani Chato.Katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Robert Gabriel.
 Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni (aliyeshika koti), akishuka katika boti maalumu aliyowakabidhi Kikosi cha Polisi wilayani Chato ikiwa ni mkakati wa Serikali kupambana na uhalifu katika ukanda wa Ziwa na Bahari nchini.
Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi  Robert  Gabriel, akishuka  katika boti maalumu iliyokabidhiwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni(hayupo pichani) kwa   Kikosi cha Polisi Wanamaji  wilayani Chato, ikiwa ni mkakati wa Serikali kupambana na uhalifu katika ukanda wa Ziwa na Bahari nchini.

Na Mwandishi Wetu
Serikali imejipanga kuimarisha Ulinzi na Usalama katika Ukanda wa Ziwa na Bahari kote nchini ili kuweza kudhibiti uhalifu unaotekelezwa majini ikiwepo uvuvi haramu, usafirishaji wa magendo na uhalifu mwingine unaotokea katika maeneo ya ziwa na bahari.
Akizungumza wakati wa makabidhiano ya boti maalumu ya doria na ufunguzi wa Kituo cha Polisi Wanamaji, wilayani Chato, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni amesema lengo la Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha inadhibiti uhalifu katika Ukanda wa Ziwa na Bahari kwa kutumia Vyombo vya Ulinzi na Usalama vilivyopo chini ya serikali, ili kuhakikisha wananchi wanafanya shughuli za kuchumi bila ya kuwa na wasiwasi juu ya usalama wao
Alisema moja ya changamoto kubwa aliyoelezwa wakati alivyofanya ziara ya awali wilayani Chato ni kuwepo kwa matukio ya uhalifu ziwani yaliyopelekea baadhi ya wananchi kusitisha shughuli za kiuchumi katika mwambao huo wa Ziwa Victoria.
“Serikali ya Awamu ya Tano imedhamiria kuleta maendeleo katika nyanja zote na kuwawekea mazingira mazuri wananchi wake kujishughulisha na shughuli za kiuchumi, hivyo basi tutahakikisha tunaimarisha ulinzi katika sehemu zote ambazo wananchi wanafanya shughuli zao ikiwepo ukanda wa ziwa na bahari na leo hii tunaanzia hapa wilayani Chato.
“Pia nawasihi askari polisi kufanya kazi kwa maadili na agizo hili nalitoa kwa nchi nzima na serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi aitomvumilia askari yoyote atakaebainika kuwabambikia kesi wananchi,hatua kali zitachukuliwa kwa atakaebainika” alisema Masauni ambae pia ni Mbunge wa Kikwajuni
Naye Diwani wa Kata ya Muungano, wilayani Chato,Johnson Kilimokwanza alisema anaishukuru serikali kwa kuleta boti hiyo na ufunguzi wa kituo cha polisi kwani moja ya changamoto iliyokuwa inawasumbua wavuvi katika mwambao huo ni masuala ya uhalifu unaotokea ziwani huku akiweka wazi uwepo wa kituo na boti ya doria vitapunguza masuala ya uhalifu.
Mmoja wa askari polisi ambae hakupenda  jina lake litajwe  alisema wao wanaishukuru serikali kwa kuwaletea boti na  kituo ambavyo vitawarahisishia kupambana na uhalifu
“Muhimu naomba serikali pia waweze kutuletea gari ambalo litasaidia pia katika mapambano hayo ya uhalifu kama unavyoona tayari tuna kituo hapa cha wanamaji naibu waziri amekizindua,muhimu sasa tuletewe usafiri utakaowezesha kupeleka mahabusu mahakamani,” alisema askari polisi huyo.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad