HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Monday, August 13, 2018

DOKTA ASHATU KIJAJI AINYOOSHEA KIDOLE WAKALA WA MAJENGO-TBA

 Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (kushoto), akiwasili kukagua mradi wa Ujenzi wa Jengo la Ofisi mpya za Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Mkoani Kigoma, katikati ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Bi. Fatina Hussein Laay, na kulia ni Mhandisi wa mradi huo Bw. Abubakari Basuka.
 Mhandisi wa mradi wa Ujenzi wa Jengo la Ofisi mpya za Halmashauri ya Mji wa Kasulu Mkoani Kigoma  Bw. Abubakari Basuka (aliyevaa kofia) akisoma taarifa fupi ya Mradi kwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), wa tatu Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Kasulu, Kanali Simon Anange.
 Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu Bi. Fatina Hussein Laay (kushoto), akieleza umuhimu wa kukamilika kwa ujenzi wa jengo la Ofisi za Halmashauri yake ya Mji kwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (katikati) kwa kuwa ofisi zinazotumika sasa hazikidhi mahitaji, wa pili kulia ni Kamishna wa Kodi za Ndani wa Mamlaka ya Mapato Tanzania - TRA, Bw. Elijah Mwandumbya.
 Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (katikati), akitoa maagizo kwa Mhandisi wa mradi wa Ujenzi wa Jengo la Halmashauri ya  Mji wa Kasulu Mkoani Kigoma  Bw. Abubakari Basuka (kulia) kutumia nguvu kazi iliyopo Wilayani humo kuharakisha utekelezaji wa mradi.
 Mkuu wa Wilaya ya Kasulu, Kanali Simon Anange (kulia) akieleza jambo kwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (hayupo pichani), wakati wa ziara ya Naibu Waziri huyo ya kukagua Ujenzi wa Jengo la Ofisi za Halmashauri ya Mji wa Kasulu,  Mkoani Kigoma.
 Muonekano wa mradi wa Ujenzi wa Jengo la Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu Mji Mkoani Kigoma litakalo  gharimu takribani Sh. Bilioni 2.5.
 Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), akiagana na Mhandisi wa mradi wa Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Halmashauri ya Mji wa Kasulu Mkoani Kigoma  Bw. Abubakari Basuka (kulia) baada ya ukaguzi wa mradi huo.
(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Wizara ya Fedha na Mipango)

Na Benny Mwaipaja, Kasulu, Kigoma
Naibu Waziri wa Fefha na Mipango. Dkt. Ashatu Kijaji, ameiagiza Wakala wa majengo Tanzania-TBA, kutekeleza kwa wakati mradi wa ujenzi wa Ofisi ya Halmashauri ya Mji wa Kasulu Mkoani Kigoma ili kuiepusha Serikali kutumia fedha nyingi kutokana na kuongezeka kwa gharama za miradi husika kunakotokana na ucheleweshwaji huo.

Dkt. Kijaji ametoa kauli hiyo baada ya kukagua maendelelo ya ujenzi wa Ofisi mpya za Halmashauri ya Mji wa Kasulu zinazojengwa na Serikali kwa zaidi ya shilingi bilioni 2.5 na kutaarifiwa kuwa TBA, wamechelewa kuanza ujenzi huo kwa zaidi ya miezi 12 wakati fedha zilikwisha tolewa na Serikali.

Aliishauri TBA kujipanga kukamilisha miradi inayopewa na Serikali kwa wakati kwa kuongeza idadi ya wataalam wanaoweza kusimamia miradi mingi inayotekelezwa na wakala huo.

"Pesa zipo, Serikali haiwezi kuanza kutekeleza mradi wowote kama hakuna pesa, ni jukumu lenu kama TBA kuhakikisha mnawezesha mradi huu ukamilike kwa wakati ili tupate thamani halisi ya fedha za mradi" alisisitiza Dkt. Kijaji


Dkt. Kijaji alitoa wito kwa wakazi wa Mji wa Kasulu na Kigoma kwa ujumla kuchangamkia fursa za ujenzi wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali katika maeneo yao kwani lengo la Serikali kujenga miradi hiyo ni kuwawezesha pia wananchi kiuchumi.

Hatua hiyo inafuatia taarifa iliyotolewa na Mhandisi wa ujenzi wa Jengo hilo la Ofisi ya Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Bw. Abubakari Basuka, kwamba miongoni mwa changamoto inayoukabili mradi huo ni ukosefu wa mafundi mchundo na vibarua ambapo imeelezwa kuwa vijana wengi katika eneo la mradi hawajitumi kufanyakazi.

"Wakati tunatoa taarifa ya hali ya uchumi mwaka wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Tano  madarakani, utafiti ulionesha kuwa mkoa wa Kigoma miongoni mwa mikoa ya mwisho kwa umasikini na tukaamua kuipa kipaumbele kwa kuleta miradi kama hii ili wananchi wake wanyanyuke kiuchumi.

Alimwagiza Mkuu wa Wilaya ya Kasulu Kanali Simon Anange,  kukutana na wananchi wa wilaya yake ili awaeleze fursa za kiuchumi zinazoletwa na Serikali katika maeneo yao ili waondokane na umasikini kwa kushiriki katika kufanya kazi za kujenga miradi hiyo ukiwemo mradi wa Ujenzi wa Ofisi za Kisasa za Halmashauri ya Mji wa Kasulu

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Bi. Fatina Laay, amesema kuwa kuchelewa kukamilika kwa ujenzi wa Ofisi hizo kunasbabisha wafanyakazi wa Halmashauri yake washindwe kutekeleza majukumu yao kikamilifu kutokana na ufinyu wa nafasi kwenye jengo wanalolitumia hivi sasa.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, yuko mkoani Kigoma kwa ziara ya kikazi kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo inayopatiwa fedha na Hazina pamoja na kuzungumza na jumuiya ya wafanyabiashara.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad