Na Karama Kenyunko, Blogu ya jamii
Vyuo Vikuu nchini vimetakiwa kuhakikisha vinafundisha kozi
zitakazozalisha wataalamu wengi watakaoendana na Sera ya Serikali ya
awamu ya tano ya uchumi wa viwanda.
Rai hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Chuo kinachotoa mafunzo ya Tehama
cha Power Computer LTD (PCTL), Avelin Malamsha, wakati akizungumza na waandishi
wa habari juu ya kozi mpya wanaotarajia kuitoa yenye lengo la kuwajenga vijana
kiajiliwa katika hadhi ya kimataifa na viwanda.
Amesema, wadau wa sekta ya elimu wanapaswa kujitafakari kwa
kuanzisha kozi zitakazozalisha wataalamu katika sekta ya viwanda na uwekezaji
nchini kwani elimu ni jambo kubwa kwa sasa na linashika kasi nchini ambayo
tunategemea itazalisha wasomi wengi watakaokuja kusaidia nchi.
Malamsha ameongeza kuwa, ili kuendana na Sera hiyo ya
Tanzania ya viwanda na upatikanaji wa ajira chuo hicho cha PCTL kimeanzisha
kozi mpya ya kimataifa ya Tehama (ICDL) itakayowajengea uwezo vijana kidigitali
na kuajiria sehemu yoyote duniani.
Amesema, Tanzania ya viwanda na ajira itakuwepo pale
ambapo kila mmoja akielewa mchango wake katika hili, pia itakuwepo kama
tutakuwa na rasilimali watu wa kutosha na sahihi, “PCTL kama chuo tukaona
kwamba tuna wajibu kuijenga Tanzania ya hiyo viwanda na kupunguza tatizo la
ajira kupitia kozi yetu mpya ya ICDL," alisema.
Naye Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Kimataifa linalotoa
Cheti cha kozi hiyo ya ICDL, Edwin Masanta alisema baada ya kuona mapungufu
yaliyopo nchini wameona ni vema kuileta kozi hiyo.
"ICDL inaongeza nafasi ya ajira kwa vijana kwani inatoa
wataalamu wengi katika masuala ya komputa kwenye vigezo vya kuajiliwa popote
duniani," alisema.
Mkuu wa Chuo cha mafunzo cha PCTL, Avelin Malamsha akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kuhusu program za kompyuta zinavyoweza kusaidia Tanzania kuimarika na kukua katika viwanda na kuongeza ajira kwa vijana. Kulia ni mkuu wa Itifaki kwa wanafunzi, Daniel Ngumbuke na Mkurugenzi wa PCTL nchini, Edwin Masanta.
No comments:
Post a Comment