Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Seleman Jafo, akizungumza wakati wa Hafla ya kuwapatia Vitambulisho Wazee wa Jiji la Dodoma.
Na. Atley Kuni-OR TAMISEMI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
Mhe. Selemani Jafo (Mb), amewaagiza Makatibu Tawala wa Mikoa
Tanzania Bara kuwasilisha taarifa za takwimu za wazee ifikapo 30, Juni
2018.
Waziri Jafo, alitoa kauli hiyo mapema leo alipokuwa akizindua zoezi la
kuwapatia vitambulisho maalum wazee wapatao 1,118 wa Jiji la Dodoma
kutoka kata za Mkonze, Mnadani, Uhuru, Madukani, Makole na Majengo.
Vitambulisho hivyo, pamoja na mambo mengine vitawawezesha wazee
hao kupata huduma za afya bure na kwa wakati.
“Ifikapo tarehe 15 Juni, 2018 kila kata iwe imetambua wazee na ifikapo
tarehe 22 Juni, 2018 kila Halmashauri iwe imeunganisha taarifa za wazee
kutoka katika kata zake zote” alisema Waziri. Aidha Waziri Jafo aliagiza
kuwa, “ifikapo Juni, 26, 2018 kila Mkoa uwe umeunganisha taarifa zote na
kuzituma kwa Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI”. Aliwaonyawale wote
watakaoshindwa kutimiza agizo hilo kuchukuliwa hatua kulingana na
miongozo, kwasababu watakuwa wameshindwa kutekeleza wajibu wao.
Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma akitoa salam za jiji muda mfupi kabla ya zoezi la ugawaji wa Vitambulisho kwa wazee halifanyika.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma Ndugu Godwin Kunambi
akizungumza katika hafla hiyo alisema shabaha ni kuwafikia wazee wote
kwenye Jiji hilo, na kubainisha kwamba, vitambulisho wanavyo vitoa kwa
wazee hao vitatumika pia kuwapa kipaumbele wazee sehemu zote za
kutolea huduma hususan ofisi za serikali.
“Mhe. Waziri tunataka vitambulisho hivi tunavyo wapatia wazee wetu leo
viwasaidie pia kupata huduma kwa haraka na kwa wakati pindi wanapofika
kwenye ofisi zingine za Serikali” alisema Kunambi.
Mbali na kutolea ufafanuzi wa matumizi ya vitambulisho hivyo, Mkurugenzi
Kunambi alisema juu ya Jiji hilo lilivyo jipanga katika suala zima la
makusanyo ya mapato ya ndani, ambayo ndio yamekuwa chachu ya
kuboresha huduma za afya kwa makundi maalum hususan wazee.
Mmoja ya Wazee akipokea kitambulisho mara baada yakuzinduliwa kwa zoezi lakuwapatia vitambulisho wazee Jiji la Dodoma.
“Mhe. Waziri, Jiji limepanga kukusanya Bil. 68 katika mwaka wa fedha ujao
ikilinganishwa na mwaka huu wa fedha ambapo tulijiwekea lengo la
kukusanya Bil. 20 nahadi kufikia mwezi Februari tulikuwa tumekusanya Bil.
14”. Kunambi ameongeza kuwa, katika mwaka ujao wa fedha wametenga
kiasi cha Mil. 58 kwaajili yakuwezesha huduma za wazee kwenye Jiji hilo.
Naye Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini ambaye pia ni Mkuu wa
Wilaya ya Kongwa Mhe. Deo Ndejembi, ametumia fursa hiyo kuwaonya
baadhi ya watendaji wanao waambia wazee kwamba hakuna dawa.
“Kumekuwepo na malalamiko mengi siku za nyuma kutoka kwa wazee
kuwa, baadhi ya watendaji wa afya wanawanyanyapaa wazee na
kuwaambia hakuna dawa wafikapo vituoni, sasa Mhe Waziri, mimi niliseme
kwa uwazi kabisa hatuta mvumilia mtu yeyote atakaye onekana ni kikwazo
kwa wazee hawa kadi zimetoka wazee wahudumiwe, sio mnajiwekea
vijiduka karibu na vituo halafu mnawaambia waende waka nunue” alionya
Ndejembi
Picha ya pamoja kati ya Mhe. Waziri Viongozi wa Halmashauri na wazee waliopatiwa vitambulisho.
Awali akitoa taarifa ya uandaji wa vitambulisho Mganga Mkuu wa Jiji la
Dodoma, Dkt. Mohamed Nyembea, alisema utekelezaji wa zoezi hilo
ulianza kwa hatua za awali kwa kuwatambua wazee katika Kata 41 za Jiji
la Dodoma, ambapo jumla ya wazee 15,885 kutoka kata 33 miongoni mwa
41 wamekwisha tambuliwa na miongoni mwao wanawake ni 9,132 na
wanaume ni 6,753 ambapo ni sawa na asilimia 80.5 ya kata zote 41 za Jiji
la hilo.
Utoaji wa vitambulisho kwa wazee ni utekelezaji wa sera ya Taifa ya wazee
ya mwaka 2003 ambapo inazungumzia mambo muhimu ya wazee ikiwepo
kutenga dirisha maalum katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Diwani wa Kata ya Mkonze akishukuru kwaniaba ya wananchi wa Mkonze.
No comments:
Post a Comment