Na Zainab Nyamka, Globu ya jamii
SHIRIKISHO la Mpira Kikapu Tanzania(TBF) imetangaza rasmi tarehe
ya mashindano ya kikapu ya FIBA Zone V U18 (Wanawake na
Wanaume ) kuwa yanatarajiwa kuanza June 17 hadi 22 2018 hapa
Jijini Dar Es Salaam, Tanzania.
Rais wa TBF Pharess Magesa amesema matarajio yao ni kuwa
mmoja kati viongozi wetu wakuu wa nchi ndyie atakuwa mgeni
rasmi wa mashindano hayo na yatarushwa mubashara (live) siku
zote za mashindano na vituo vyote vikubwa vya TV na Radio
ambavyo wametuma maombi.
Magesa amesema gharama za maandalizi ya timu zetu mbili za
Taifa na gharama za kuandaa mashindano haya ni kubwa, na tayari
kuna wadau wameshajitokeza kutoa ahadi na wengine
wameshasaidia.
"Hadi sasa hivi TBF ina upungufu wa takribani Sh.milioni 100, kati ya
hizo Sh.milioni 60 ni za kuandaa mashindano na Sh.milioni 40 ni za
kuweka timu zetu 2 za wanawake na wanaume kambini na kununua
vifaa vya michezo zikiwemo Jersey za kucheza na za mazoezi, truck
suits, viatu, socks, mipira na madawa,"amesema Magesa.
"Pia, tuna mahitaji mengi ili kufanikisha matengenezo ya uwanja wa
ndani wa Taifa (indoor) ukiacha kuvuja paa na kukatika kwa umeme
ambako kutadhibitiwa na msaada ulitolewa na Mkuu wa Mkoa wa
Dar es Salaam Paul Makonda,"amesema.
Katika uwanja huu wa Taifa bado kunahitajika matengenezo ya
mfumo wa taa na vifaa vya umeme, mabomba, vyoo na mfumo wa
maji, mabenchi ya kukalia, mfumo wa kutoa na kuingiza hewa
(ventilation), na rangi ya kupaka ndani na nje ili kuweka mazingira ya
uwanja yawe ya kuvutia.
Uwanja wa ndani wa Taifa utatumika kwa mashindano haya ya U18
June na pia baadae utatumika kwa mashindano ya kutafuta Klabu
Bingwa wa Kikapu FIBA Zone V yanayotarajiwa kufanyika mwezi
Septemba, 2018 hapa hapa Dar Es Salaam.
Ameelezea, kuna gharama za usafiri, posho na malazi ya Kocha wa
Kigeni ambaye anatoka Minneapolis, Marekani, Coach Matthew
McCollister ambaye anatarajia atafika nchini walau majuma 2 kabla
ya kuanza mashindano haya ili kuzinoa timu zetu 2 kwa kushirikiana
na jopo la makocha Wazalendo wakiongozwa na Coach Bahati
Mgunda.
"Tunatarajia mashindano ya FIBA Zone V U18 yatakayofanyika mwezi
ujao yatashirikisha timu za Taifa 24, za wanawake na wanaume,
kutoka nchi 12 za Misri, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Ethiopia,
Eritrea, Djibouti, Sudan, Somalia, Sudani Kusini na wenyeji Tanzania.
Bingwa wa mashindano haya atapata nafasi ya kushiriki
mashindano ya kutafuta bingwa wa Afrika (Afrobasket 2018) baadae
mwaka huu,"amesema.
Rais TBF amesema wanatarajia kutakuwa na wageni takribani 400
kutoka nchi mbali mbali ikiwa ni pamoja na maofisa kutoka FIBA,
waandishi na wadau kutoka nchi husika.
Ametoa mwito kwa wapenzi wote wa michezo nchini, Serikali, taasisi
za umma na binafsi, wafanyabiashara, wanasiasa, wafanyakazi na
wananchi wote kwa ujumla kujitokeza na kushirikiana na TBF
kufanikisha maandalizi mashindano haya ili ikiwezekana vikombe
vyote vibaki nchini na kuzipatia nafasi timu zetu za Tanzania kushiriki
Mashindano makubwa ya Kikapu ya FIBA Afrika.
Ameomba tumuunge mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. John Magufuli kwa kila mtu kuwajibika katika eneo
lake, kujenga Tanzania ya viwanda ili kusaidia ukuaji wa uchumi na
hatimaye kuifanya nchi yetu kuwa na uchumi wa kipato cha kati
haraka zaidi ya ilivyotarajiwa.
Ameongeza "Michezo ni moja ya viwanda vikubwa
vinavyotengeneza ajira nyingi za moja kwa moja na zisizo za moja
kwa moja kama tutafanya uwekezaji sahihi. Mchezo wa kikapu ni
mchezo pekee nchini unaopendwa na watu wengi wa rika na jinsia
zote kwa usawa. Hivyo basi kusaidia mchezo huu utakuwa umefanya
sehemu kubwa ya kusaidia jitihada za Serikali za kusaidia na
kuendeleza vijana wetu na kuchangia katika maendeleo ya Taifa letu
kwa ujumla,".
No comments:
Post a Comment