HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Tuesday, May 29, 2018

MUDA WA KUSHUGHULIKIA MIZIGO MPAKANI RUSUMO WAPUNGUA

Na Veronica Kazimoto
Serikali ya Tanzania na Rwanda kupitia Mamlaka zake za Mapato zimefanikiwa kupunguza muda wa kushughulikia mizigo mpakani Rusumo mkoani Kagera kwa asilimia 73.

Hayo yamesemwa leo na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Charles Kichere wakati wa Mkutano wa kwanza wa Kamati ya Uratibu wa Pamoja wa Mradi wa Maendeleo wa Kuwezesha Biashara na Udhibiti wa Mipaka Afrika Mashariki uliofanyika katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania, Zanzibar.

Kichere amesema kuwa, baadhi ya mafanikio muhimu ya  mradi huu ni pamoja na uendeshaji wa Kituo cha Huduma za Pamoja Mpakani kwenye mipaka ya Rusumo na Namanga na maendeleo ya uwezo wa utendaji kazi wa maofisa wa forodha na mawakala.

"Mafanikio ya mradi huu yanaonekana wazi, kwa mfano tukichukulia mpaka wa Tanzania na Rwanda eneo la Rusumo, muda wa kushughulikia mizigo mpakani hapo umepungua kwa asilimia 73% yaani kutoka masaa manane na dakika 42 hadi kufikia masaa mawili na dakika 20 tu," alisema Kichere.

Mradi huu wa Maendeleo wa Kuwezesha Biashara na Udhibiti wa Mipaka Afrika Mashariki ni wa miaka mitatu na nusu ambao unafadhiliwa na Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA) na ulizinduliwa rasmi mwezi Desemba, 2017.

Mradi huu unatekelezwa  na Mamlaka tano za Mapato  za nchi za  Jumuiya ya Afrika Mashariki ambazo ni Tanzania, Burundi, Kenya, Rwanda na Uganda.
 Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Charles Kichere (katikati) akizungumza wakati wa Mkutano wa kwanza wa Kamati ya Uratibu wa Pamoja wa Mradi wa Maendeleo wa Kuwezesha Biashara na Udhibiti wa Mipaka Afrika Mashariki uliofanyika leo Zanzibar. Kushoto ni Mhe. Audace Niyonzima wa Mamlaka ya Mapato Burundi na kulia ni Bw. Toshio Nagase Mwakilishi Mkazi wa JICA.
 Baadhi ya wajumbe wa Mkutano wa kwanza wa Kamati ya Uratibu wa Pamoja wa Mradi wa Maendeleo wa Kuwezesha Biashara na Udhibiti wa Mipaka Afrika Mashariki ambao umefanyika leo Zanzibar.
 Baadhi ya wajumbe wa Mkutano wa kwanza wa Kamati ya Uratibu wa Pamoja wa Mradi wa Maendeleo wa Kuwezesha Biashara na Udhibiti wa Mipaka Afrika Mashariki ambao umefanyika leo Zanzibar.
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Charles Kichere (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Makamishna Wakuu kutoka nchi za Afrika Mashariki na wajumbe wa Mkutano wa kwanza wa Kamati ya Uratibu wa Pamoja wa Mradi wa Maendeleo wa Kuwezesha Biashara na Udhibiti wa Mipaka Afrika Mashariki ambao umefanyika leo Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad