HABARI MPYA

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, April 11, 2018

WAZIRI MKUU AKEMEA UPOTOSHAJI KUHUSU MUUNGANO

*Awataka waulinde, aonya sukari isiwe sababu
 WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waulinde Muungano baina ya Tanzania Bara na Zanzibar na akawaonya wasitumie Bunge hilo kuupotosha.

Ametoa kauli hiyo Jumanne, Aprili 10, 2018 Bungeni mjini Dodoma kwenye mkutano wa 11 wa Bunge, wakati akihitimisha mjadala wa mapitio ya utekelezaji wa kazi za Serikali kwa mwaka 2017/2018 na mwelekeo wa kazi za Serikali kwa mwaka 2018/2019.

Waziri Mkuu amesema mjadala ulioibuka jana kuhusu suala la Muungano haukuwa na afya na kwamba hatarajii kuona hali hiyo ikijirudia tena Bungeni kuhusiana na suala la Muungano.

“Mjadala wa jana sijaupenda kabisa na wala haukuwa na afya, ulikuwa ni malumbano baina waheshimiwa wabunge wawili. Hatuzuii Mhe. Mbunge kuuliza jambo ili apate ufafanuzi lakini pia haturuhusu mtu na mtu watumie Bunge kupotosha ukweli wa mambo,” alisisitiza.

Waziri Mkuu amelieleza Bunge kwamba kuna maboresho ambayo yanafanywa hivi sasa na Serikali za pande zote mbili lakini akatumia fursa hiyo kulihakikishia Bunge kwamba majadiliano bado yanaendelea kwenye vikao halali vya SMT na SMZ ambavyo vinaongozwa na Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Akitoa ufafanuzi kuhusu chanzo cha malumbano hayo, Waziri Mkuu alisema kiini cha malumbano hayo ni suala la uagizaji sukari kutoka nje ya nchi ili kufidia upungufu wa sukari uliopo nchini (gap sugar). Alisema katika kutimiza azma hiyo, Serikali haiangalii kama muagizaji ametoka Tanzania Bara au Tanzania Zanzibar.

Akitoa mfano, Waziri Mkuu alisema katika mwaka 2016, upungufu uliojitokeza ulikuwa tani 140,000 lakini waagizaji waliopewa vibali walikuwa wawili kutoka Zanzibar, watatu kutoka Bara na kiwanda cha sukari cha Mahonda kilipewa kibali cha kuagiza tani 390.

“Katika mwaka 2017, gap sugar ilikuwa tani 140,000 na waliopewa vibali walikuwa ni wawili kutoka Zanzibar na wawili kutoka Bara, lakini kwa mwaka huu (2018) gap sugar ni tani 135,000. Tofauti na miaka ya nyuma, safari hii tumewapa vibali wenye viwanda ndiyo waagize sukari kutoka nje. Kwa hiyo, jambo hili la sukari lisivuruge Muungano wetu,” alisisitiza.

Waziri Mkuu alisema nia ya Serikali ni kuzalisha sukari ya kutosha hapa nchini ili nchi ijitegemee na kawataka Mawaziri wa Biashara wa Zanzibar na Tanzania wawe makini ili sukari inayoagizwa nje isije kufurika soko la ndani kwa sababu gharama za uzalishaji sukari ya ndani ni kubwa.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akihitimisha Hoja ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu, bungeni mjini Dodoma, Aprili 10, 2018. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad